Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Katiba na Sheria

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kwa unyenyekevu mkubwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Subhanahu-Wataala kwa kuniwezesha leo asubuhi kuwasilisha Mpango wa Makadirio ya Bajeti ya Wizara kwa mwaka 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kwa namna ya pekee namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwawezesha Waheshimiwa Wabunge kushiriki na kuchangia hotuba ya Wizara yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee nachukue fursa hii kukushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi ya kuwasilisha hotuba yangu na kwa umahiri wako katika uendeshaji wa Vikao vya Bunge na kwa kusimamia mjadala huu vizuri. Nimshukuru Mheshimiwa Dkt. Adeladus Lubango Kilangi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ushirikiano ambao ananipa katika kutekeleza majukumu yangu na kipekee kwa kuungana na mimi katika kujibu baadhi ya hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge wakati wa mjadala wa hotuba yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara nyingine naishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kwa maoni na ushauri ambao wanaipatia Wizara na Taasisi zake katika kutekeleza majukumu yetu vizuri. Napenda nikuhakikishie wewe binafsi, Kamati yako na Waheshimiwa Wabunge wote kuwa tumepokea kwa unyenyekevu na shukrani maoni, hoja na ushauri mliotupa wakati wa mjadala wa bajeti yetu. Kwa niaba ya Wizara tunaahidi kuyafanyia kazi masuala yote yaliyojitokeza katika mjadala huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mjadala wa hotuba aliyoitoa Mheshimiwa Waziri Mkuu na katika mjadala wa hotuba ya Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora, Waheshimiwa Wabunge walitoa hoja mbalimbali ambazo kwa namna moja au nyingine ziligusa Wizara yangu na Sekta ya Sheria kwa ujumla. Tumezipokea hoja zote zilizotolewa na tunaahidi kuzifanyia kazi na kuleta mrejesho wake Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia kwa kuongea na wale waliochangia kwa maandishi na kuichambua bajeti yetu kwa kina. Michango yenu ni nyenzo muhimu ya kuboresha utendaji kazi wa Wizara na taasisi zake ili sekta ya sheria ikidhi matarajio ya Watanzania na iwe na mchango chanya katika maendeleo yao ya kijamii, kisiasa na kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jumla wa Wabunge 40 wamechangia hotuba yetu, ambapo Wabunge 34 wamechangia kwa maandishi na Waheshimiwa Wabunge sita wamechangia kwa kuzungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa uniruhusu nianze kujibu hoja mbalimbali zilizotolewa na nitoe indhari tu kwamba hoja zote nyingine ambazo sitazijibu zitajibiwa kwa maandishi. Nianze na hoja zilizotolewa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ni kuhusu uhaba wa watumishi wa Mahakama wenye sifa zinazotakiwa katika kada mbalimbali. Napenda kusema kwamba upo uhaba wa watumishi katika kada mbalimbali kama Mahakimu, Wasaidizi wa Kumbukumbu na Makatibu Mahsusi. Hata hivyo, kwa mwaka wa 2017/2018 vibali vilipatikana na ajira kutolewa. Mfano, Majaji 12 na Mahakimu 194 wameajiriwa; Wasaidizi wa Kumbukumbu 90 na Makatibu Mahsusi 30 wameajiriwa pia. Aidha, watumishi 298 wa idara nyingine waliajiriwa. Kwa mwaka ujao wa fedha 2018/2019 ajira 513 za kada mbalimbali zinategemewa kutolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ya Kamati ni kwamba Watendaji wanawanyanyasa Majaji na Mahakimu na kujiingiza kwenye maamuzi ya kesi, lakini pia sheria ya uendeshaji wa Mahakama iboreshwe kudhibiti nidhamu na ikiwezekana kuwarejesha kwenye nafasi zao za awali. Wizara, Tume ya Utumishi wa Mahakama na Mahakama tumefanya mikutano ya pamoja na Kamati ya Katiba na Sheria mara kadhaa ikiwemo kupitia bajeti ya Wizara na taasisi zilizo chini yake. Kwa bahati mbaya hatukupata fursa ya kupewa hoja hii na kujadiliana na Kamati wala Mwenyekiti wala Kamati katika suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, suala hili lina historia ndefu kwa sisi tuliokuwepo na kushiriki kwenye maboresho ya Mahakama. Mapendekezo ya maboresho ya uendeshaji wa Mahakama na hatimaye kutungwa Sheria Na. 4 ya mwaka 2001 na muundo wake kupitishwa na Mheshimiwa Rais mwaka 2014 yana historia ndefu ya mapendekezo ya Tume za Mheshimiwa Msekwa, Mheshimiwa Jaji Bomani na Mheshimiwa Jaji Mroso.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa, takwimu na hata viashiria mbalimbali vinaonesha kuwa Mahakama kwenye nyanja karibu zote inapiga hatua kubwa ya maendeleo ya uendeshaji pamoja na kazi yake ya msingi ya utoaji haki. Tume ya Utumishi wa Mahakama chini ya Mheshimiwa Jaji Mkuu na hata Wizara ama mimi Waziri hatujapokea malalamiko yoyote juu ya kunyanyaswa ama kunyanyasana kuingilia shughuli za kazi nje ya majukumu yao ya kiutendaji kwa watendaji husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, endapo kuna tatizo la mtu mmoja mmoja kama binadamu, ni vyema litolewe taarifa husika na suala husika kwenye mamlaka husika za kikatiba na kisheria, yaani Tume ya Utumishi wa Mahakama na ama niletewe mimi kama Waziri ili yashughulikiwe kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo. Serikali kwa maana ya Wizara, tutaendelea kushirikiana na Tume ya Mahakama kwenye kusimamia na kuendeleza maboresho ya Mahakama kwa manufaa ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ilikuwa ni kuwahamisha watumishi bila kulipwa stahili zao kwa kuzingatia umuhimu wa kujaza nafasi mbalimbali hasa za madaraka (duty post) watumishi wamekuwa wakihamishwa na kulipwa sehemu ya stahili zao kabla ya kuhama na sehemu inayobaki inamaliziwa baadae.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ushauri wa Mahakama kurudia kuezeka paa la Mahakama Kuu ya Kanda ya Shinyanga, ningependa kusema kwamba mradi wa Mahakama Kuu ya Shinyanga ulikamilika mwaka 2016, mara baada ya kukamilika kulikuwa na tatizo la kuvuja kwa maeneo machache ya paa hilo. Kwa kuwa mradi ulikuwa bado kwenye kipindi cha matazamio (defect liability period) mkandarasi alirekebisha na sasa tatizo hilo halipo tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu zabuni za ujenzi wa miradi ya maendeleo kwa Mahakama kwamba zitolewe kwa uwazi, kipaumbele kitolewe kwa makampuni ya ndani ya Wakandarasi yanayokidhi vigezo na uwezo wa kukamilisha mradi kwa wakati na kwa mujibu wa mikataba husika; napenda kusema kwamba Mahakama imekuwa ikitekeleza miradi yake kwa uwazi wakati wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto kubwa ya ukosefu, uhaba na miundombinu ya Mahakama na kwa kuzingatia uchache wa rasilimali fedha, ukilinganisha na mahitaji halisi ya Mahakama na gharama kubwa za ujenzi, Mahakama ilifanya utafiti wa kubaini teknolojia ya ujenzi yenye gharama nafuu iitwayo moladi ambayo inapunguza gharama kwa takribani asilimia 40 mpaka 45.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchambuzi wa zabuni za miradi ya Mahakama za Wilaya na za Mwanzo iliyotangazwa mwaka 2016/2017 ilionesha kuwa waombaji wa zabuni waliokuwa na gharama za chini kabisa zilikuwa ni shilingi bilioni 1.2 kwa Mahakama za Wilaya na shilingi milioni 898 kwa Mahakama za Mwanzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na gharama kubwa, Mahakama ilisitisha zabuni hizo na kutumia teknolojia mbadala ya moladi ambayo ni ya Watanzania japo ni teknolojia yenye asili ya Afrika ya Kusini na teknolojia hii imehuishwa na Chuo Kikuu cha Ardhi. Kanuni na taratibu zote za ununuzi wa umma zilizingatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mwenyewe nimefungua Mahakama Kigamboni ya utaratibu wa moladi, ni mahakama nzuri kwa gharama ambayo mtu hawezi kuamini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upungufu wa udahili katika Taasisi ya Mafunzo kwa Vitendo (Law School of Tanzania), ningependa nieleze kwamba hakuna upungufu wa wahitimu wa sheria katika vyuo vikuu nchini. Sasa hivi tuna vitivo vya sheria 17 nchini. Kwa hiyo, hakuna upungufu wa wahitimu wa sheria. Suala la kwenda Law School, zipo sababu nyingi kwa nini baadhi ya wanafunzi hawaendi Law School.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, wapo ambao wamesoma sheria lakini lengo lao siyo kuwa Wanasheria. Wamemaliza degree ya sheria na hawakutaka kuendelea na sheria, wamekwenda kufanya kazi nyingine. Na mimi namfahamu mwanafunzi mmoja ambaye amemaliza sheria, amemaliza na Law School, amekuwa Advocate, ameacha na sasa anajifunza u-pilot wa ndege. Aliniambia kazi ya sheria ilikuwa ya baba, Uwakili ulikuwa wa baba, nimemaliza ya baba, sasa nafanya mimi ninayotaka. Sasa hivi ninavyosema, anajifunza Urubani chini ya shirika fulani la ndege silitaji. Kwa hiyo, wapo ambao wakimaliza degree ya sheria hawana interest ya sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wapo wanaoangalia perspective ya soko. Ukiangalia katika private sector ya practice ya sheria, napenda niseme kwamba miongoni mwa maeneo ambayo watu hawatengi fedha kwa ajili ya huduma, ni sheria. Hakuna hata mtu mmoja humu ndani ya Bunge hili ambaye ana Family Lawyer ambaye amempangia bajeti kwa mwaka atam-retain amlipe kiasi fulani. Kwa hiyo, vijana wetu hawa nao ni mahiri na wajanja, wakiona kwamba huku hakuna maendeleo mazuri, basi wanakwenda kwingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, ni kweli huko nyuma wanafunzi walikuwa napewa mikopo moja kwa moja, lakini sasa mikopo inatolewa kwa wale ambao wanastahili kwa kutumia means test na katika maeneo ya kipaumbele. Sheria siyo mojawapo ya eneo la kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kuanzisha matawi mbadala ya taasisi ya sheria, napenda kusema kwamba jambo hilo tumekuwa tunalifikiria na kulitafakari kwa makini, lakini jitihada yetu kubwa kwanza ni kuimarisha ubora wa taasisi hii pale ilipo na baada ya kuimarisha ubora ndipo tutaweza kufikiria mambo ya kupanua kwingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tufahamu kwamba sasa tuna vitivo 17 vya sheria. Mahali pekee ambapo wanasheria wote hawa wanakutana na kupikwa ni kwenye Law School of Tanzania. Kwa hiyo, kabla ya kuanza kufikiria kuanzisha matawi, ni lazima tufanye utafiti wa kutosha ili tuhakikishe wanasheria wote wana utamaduni, mila na desturi zinazofanana kwa sababu sasa wanatoka kwenye vyuo vingi tofauti na ilivyokuwa huko nyuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati imetushauri pia kuhusu Ofisi ya Taifa ya Mashitaka kwamba pawe na ushirikiano kati ya Ofisi ya Taifa ya Mashitaka, Mahakama, Polisi na vyombo vingine vya upelelezi ili kurahisisha utekelezaji wa majukumu ya ofisi pamoja na kuongeza wigo wa utoaji haki bila kuingilia uhuru wa vyombo vingine. Ushauri huu umepokelewa na utafanyiwa kazi. Ofisi ya Huduma ya Mashitaka itaendelea kuimarisha na kuboresha mahusiano na ushirikiano na taasisi na wadau wa haki jinai na ndiyo maana katika mabadiiko ya sheria ambayo tunategemea kuyaleta Bungeni, ni pamoja na kuanzisha Criminal Justice Forum ambayo itahusisha taasisi mbalimbali lakini pia kuwe na Government Legal Team ambayo itahusisha mambo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri mwingine wa Kamati ni kwamba Ofisi hii ya Taifa ya Mashitaka ihakikishe inafungua ofisi zake katika Mikoa na Wilaya zilizoainishwa katika taarifa ya bajeti kwa lengo la kuongeza wigo wa utoaji haki. Napenda kusema kwamba ushauri umepokelewa na utafanyiwa kazi. Ofisi imeainisha maeneo itakayofungua ofisi kuwa ni Mkoa wa Songwe, Wilaya ya Kinondoni, Wilaya ya Ilala na Wilaya ya Kigamboni na kwa kadri inavyowezekana, basi tutafungua katika Wilaya na Mikoa mingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Kamati ilizungumzia suala la Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, kwamba kuwepo kwa malalamiko mengi kuhusu uvunjwaji wa haki za binadamu, ukiukwaji wa misingi ya utawala bora nchini pamoja na tuhuma za kushikiliwa watu Magerezani, Polisi na sehemu nyinginezo nchini pasipo kuwepo utoaji haki au majibu yanayoridhisha. Kamati ilishauri Tume ifanye ukaguzi katika sehemu zote nchini zenye malalamiko hayo na kutoa taarifa kwa mujibu wa sheria ili kutatua changamoto hizo endapo zitabainika. Ushauri umepokelewa na utazingatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kwa mwaka wa fedha 2018/2019 Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora itatembelea sehemu zilizolalamikiwa zikiwemo Magereza na Vituo vya Polisi na taarifa itawasilishwa kwenye mamlaka husika kwa hatua stahiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Kamati imetoa maoni kuhusu Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania. Kamati imeshauri Tume ya Kurekebisha Sheria kufanya mapitio ya sheria mbalimbali kwa lengo la kuhakikisha kunakuwepo na mfumo wa sheria nchini unaozungumza lugha moja (uniformity of law) na hivyo kuondokana na mgogoro wa kisheria usio na lazima (unnecessary conflict of law) unaoweza kujitokeza wakati wa utekelezaji. Napenda niseme kwamba ushauri unapokelewa na utazingatiwa. Aidha, Tume katika kufanya mapitio ya mifumo ya sheria mbalimbali itahakikisha kutokuwepo kwa migongano baina ya sheria wakati wa kutoa mapendekezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Kamati ya Bajeti nayo ilikuwa na maoni yafuatayo; moja, bajeti iliyotolewa ya mwaka 2018/2019 haikidhi mahitaji ya msingi ya Mfuko wa Mahakama na kwamba Serikali ihakikishe inaongeza bajeti ya mfuko. Maoni ya Kamati yatazingatiwa, bajeti ya mfuko kwa fedha za matumizi ya kawaida na maendeleo kutoka Serika itaongezwa kadri mapato ya Serikali yanavyoongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Kamati ilitoa maoni kuwa kutokukamilika kwa utaratibu wa kuwezesha mifumo ya ukusanyaji maduhuli kielektroniki (E-pos machine), tunasema Serikali kupitia Mahakama tayari imeanza kutumia mfumo wa kielekroniki (Pos machine) ambapo Mahakama zote za Mkoa wa Dar es Salaam zinatumia mfumo huo. Utaratibu utafanyika pia mikoani kwa kuongeza mashine hizo kama Kamati ilivyoshauri. Aidha, mawasiliano yanaendelea kufanyika kati ya Wizara na Wizara ya Fedha ili vifaa hivyo viweze kupatikana kwa bei nafuu na kwa wakati ili kuongeza mapato ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wale waliochangia kwa mdomo, nianze na Mheshimiwa Kombo. Niseme kwamba suala la Joint Finance Commission na suala la Joint Account lilitolewa maelezo mazuri sana jana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira na Muungano) na majibu ya Serikali ni hayo hayo kwamba jambo hilo ni kama lilivyokuwa limeelezwa kwenye Wizara hiyo. Tume ipo na mchakato wa kuanzisha akaunti hiyo unaendelea kwa taratibu za kiserikali na hapo utakapokamilika, basi mambo hayo yatatekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kutekeleza matakwa ya Katiba, lakini ni jambo ambalo utekelezaji wake unahitaji maandalizi ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la mwingiliano kati ya Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoshughulikia mambo yasikuwa ya Muungano ya Tanzania Bara na Mahakama Kuu ya Zanzibar, napenda kukubaliana nawe kwamba Mahakama zote hizo zina mamlaka sawa (concurrent jurisdiction) lakini pamoja na kuwa na concurrent jurisdiction, yapo mashauri ambayo yanaweza kuwa yamefanyika Tanzania Bara yakalazimika kujadiliwa na Mahakama Kuu ya Zanzibar ikiwa yatakuwa na uhusiano na Mahakama Kuu ya Zanzibar na vivyo hivyo yapo ambayo yatafanyika Zanzibar, lakini yakasikilizwa na Mahakama Kuu ya Tanzania kutegemea ni wapi palipokuwa chanzo cha mgogoro au kesi hiyo, mtandao unaohusika na nyezo zilizotumika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pamoja na hizo mahakama kuwa na concurrent jurisdiction, lakini upo wakati ambapo moja inaweza ikasikiliza mashauri yaliyotoka upande mwingine kwa kutegemea muktadha na aina ya tatizo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la OIC, tarehe 4 Aprili, 2018 Wizara ya Mambo ya Ndani ilijibu na kutoa maelezo mazuri kuhusu suala la OIC na nadhani majibu hayo yanakidhi suala hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mashehe wale wa Uamsho na wale wa Zanzibar, suala hili lipo Mahakamani na Wizara iahidi tu kwamba itazidi kuhamasisha uchunguzi ukamilike ili kesi hiyo iendelee. Kesi za namna hii ni very complex na wakati mwingine ushahidi wake kuukusanya unahitaji muda na umahiri na wakati mwingine unahitaji ushirikiano na taasisi na vyombo vilivyo nje ya nchi ambako pia tunalazimika kuomba ushahidi kwa njia mbalimbali. Ni imani yangu kwamba jambo hili litapata muafaka na litapata suluhisho wakati uchunguzi utakapokuwa umekamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Mheshimiwa Kiteto kuhusu Mabaraza ya Ardhi; Tume ya Marekebisho ya Sheria ilifanya utafiti kuhusu Mabaraza ya Ardhi. Taarifa hiyo ilifikishwa kwa Waziri na nimetoa maelekezo, kuna maeneo ambayo nimeomba yafanyiwe utafiti zaidi. Kwa hiyo, mara baada ya maeneo hayo ya nyongeza ambayo nimewarudishia Tume ya Kurekebisha Sheria yatakapokamilika, basi Serikali itashauriwa ifanye nini kuhusu Mabaraza haya ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mabadiliko ya Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971, Serikali ilitoa ahadi hiyo Septemba ya mwaka 2016, lakini baada ya kutafakari kwa makini suala la mabadiliko ya Sheria ya Ndoa linahitaji umakini mkubwa sana. Wewe unafahamu vyema ni sisi Tanzania peke yetu tuliofanikiwa mwaka 1971 kutunga Sheria ya Ndoa. Uganda ambao walikuwa wa kwanza kuanza mchakato huu mwaka 1966 chini ya Ripoti ya Kalema mpaka leo wameshindwa kuwa na sheria moja ya ndoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kenya ambao walianza juhudi za kuwa na sheria moja ndoa ya mwaka 1968 hawakufanikiwa mpaka baada ya mauaji yaliyotokea. Wametunga sheria, sheria imepita na baadhi ya mambo ambayo sheria imeyakataza, sasa watu wameanza kuyadai na moja ya mambo ambayo sheria ya Kenya ya sasa ya ndoa inayakataza na sasa yameanza kudaiwa, tena wanaodai ni wanawake, ni kufuta talaka. Hii ni kwa sababu Sheria ya Ndoa ya Kenya imefuta talaka, lakini wote tumeona sasa jitihada kubwa tena ya hadharani na inaongozwa na wanawake kudai sheria ya kuwaruhusu talaka irejeshwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema nini? Mashauri ya ndoa, mirathi, mashauri yanayogusa mila na destruri, yanayogusa dini na itikadi, ni vyema kuyaendea kwa uangalifu mkubwa. Najua kabisa na niseme tu kwa unyenyekevu, somo hili la ndoa nimelifundisha kwa miaka 19, siyo eneo jepesi. Kuhusu kwa mfano, umri wa mtoto kuolewa mpaka ninavyozungumza sasa umri wa mtoto wa kike kuolewa Uingereza ni miaka 16. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, zipo sababu kubwa na mukhtadha wake tuambiane, mwaka 1971 wakati sheria hii ya ndoa inapitishwa, elimu ya mwisho ya mtoto ilikuwa darasa la saba. Asipoendelea kwenda form one, ina maana amekaa nyumbani na turudi twende kwenye jamii na kila mmoja nyumbani kwake. Hivyo, mtoto wa kike aliyevunja ungo, kipi chema, aolewe azae katika ndoa au azuiwe kuolewa mpaka afike miaka 15 wakati huko kwingine hakujafungwa na anaweza akapata ujauzito? Atakapoupata ujauzito huo akazaa huyo mtoto, kama ni mkatoliki hatabatizwa mpaka aende akafanye maungamo na maungamo hayo ya kikatoliki ni ya yeye mama, sio baba aliyemzalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 ukiifumua leo, kuipitisha ndugu zangu ni ngumu. Yapo mambo matatu ndani ya hii Sheria ya Ndoa ambayo kwa Kanisa Katoliki hayakubaliki. Moja, hawakubali kubadili ndoa ingawa Sheria ya Ndoa ya mwaka 1971 inaruhusu kubadili ndoa ya mke mmoja kuwa ndoa ya wake wengi. Baraza la Maaskofu Katoliki lilipinga, lakini Mwalimu ambaye alikuwa ni mkatoliki aliwaambia, situngi sheria ya wakatoliki, natunga sheria ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya Sheria ya Ndoa ya sasa inaruhusu kubatilishwa na ndoa na Mahakama za kawaida. Kanisa Katoliki halikubali. Mimi sio Mkatoliki, lakini kwa Kanisa Katoliki ndoa inabatilishwa tu na Askofu baada ya kushauriwa na Judicial Vicar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakapofungua hii, we are opening a pandora box. Ukiangalia tuna tafsiri tofauti ya ndoa. Zipo ndoa ambazo kwao ni sakramenti; wapo ambao ndoa kwao ni covenant. Kwa hiyo, unapokuwa na mchanganyiko huo mkubwa kiasi hicho ni vyema ukafanya mambo kwa tahadhari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo ndani ya sheria hii bado yana vikwazo kwa Waislam, ni compromise. Sheria yoyote iliyofikiwa kwa compromise, be careful when you want to change it. Sheria hii ni very progressive katika maeneo mengine. Ndiyo sheria ya kwanza duniani kuwaruhusu wanawake kuwa na nguvu hasa wanawake wasomi na watalaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chini ya Sheria ya Ndoa ya Uingereza, cohabitation maana yake mke na mume waishi ndani ya nyumba moja muda wote. Ndiyo maana wanawake wa Kiingereza hawakuweza kupanda vyeo kwenda kufanya kazi nje ya maeneo ambayo waume zao wanafanya kazi. Mwaka 1971 Sheria ya Ndoa, cohabitation maana yake siyo kuishi ndani ya nyumba moja, mnaweza kuishi sehemu mbali lakini kwa makubaliano, kwa simu na kwa barua. Tafsiri hiyo ni cohabitation. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya hii Sheria ya Ndoa ya kwetu, malipo ni jukumu la mwanaume kuitunza familia (the necessity of life). Kwa hiyo, yapo maeneo mengi ambayo sisi tumepiga hatua ambayo nchi nyingine bado hawajapiga hatua. Hiyo haina maana tusiangalie yaliyopungua. Niliwaeleza hapa na ninarudia, mpaka leo Ulaya Wabunge wanawake wanapata mshahara mdogo kuliko Wabunge wanaume kwa sababu ni wanawake. Kwa hiyo, sihalalishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kusema, kila nchi ina sababu ya kutokufanya mambo fulani na yanahitaji muda; na moja ni Sheria ya Ndoa. Tukiindea kwa haraka tutavuruga zaidi kuliko kujenga. Kwa hiyo, tujenge muafaka wa taratibu, kwa sababu Sheria ya Ndoa ni jamii sio mtu. Ndiyo maana Sheria ya Ndoa ya sasa kuhusu ugoni (adultery) niwaambie, ndani ya sheria ya sasa ya ndoa adultery inaweza kuwa evidence; the marriage has broken down irreparably and therefore the Court can grant divorce. Humo humo adultery kwa kutambua yako makabila hapa ambayo adultery siyo sababu ya kuvunja ndoa, sheria hii ya ndoa inatoa kibali cha compensation.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nayafahamu makabila mawili ambayo bila kumfumania mke wako ugoni, unaona hujaoa. Kwa hiyo, mambo haya yanahitaji umakini. Kwa hiyo, mtanifuata baadae nitawaambia. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuliendee kwa utaratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa Serikali imekata rufaa kuhusu Sheria ya Umri wa Mtoto Kuolewa, lakini tunapokata rufaa, hatukati rufaa kwenye Mahakama ya Rufaa on matters of facts. Tunakata rufaa on points of law. Ule uamuzi bahati mbaya sana tunaangalia matokeo, hatuangalii hoja za uamuzi ule. Ukizifuata hoja za uamuzi ule, hakuna sababu ya kuwa na Viti Maalum.

Ndiyo. Ukifuata hoja ya uamuzi ule, hakuna sababu ya kuwa na Viti Maalum, kwa sababu huo pia ni upendeleo ambao hauruhusiwi na Katiba kwa Ibara ya 13. Maana yake nini? Ndiyo maana Katiba inaruhusu positive discrimination, affirmative action. Ni affirmative action inayoruhusu Viti Maalum. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa historia ya Tanzania, bila affirmative action, idadi ya Wabunge wanawake humu wengi watatoka Mtwara na Lindi, kwa sababu ni matrilineal na ndiyo wamekuwa wanaleta Wabunge wengi wa kuchaguliwa. Suala la Tarime, ni ajali kwa mila na desturi. Ninapenda niliweke vizuri, kwa mila na desturi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lengo kubwa la sheria hiyo…

KUHUSU UTARATIBU . . .

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: MheshimiwaMwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na ndiyo maana nasema kwamba lengo la Serikali kwenda Mahakama ya Rufaa ni kubakiza principle ya positive discrimination, principle ya affirmative action ili kwa kuangalia hali halisi ya Tanzania wanawake waendelee kupata nafasi katika vyombo vya maamuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na lengo lake sio suala la umri wa mtoto kuoa au kuolewa, someni arguments za yule Jaji ninayemheshimu sana kwa sababu tumesoma darasa moja, hoja ni ile ya argument. Ni sawasawa na hesabu, unaweza ukasema jibu ni nne, lakini mwalimu hasahihishi jibu, mwalimu mzuri wa hesabu anaangalia method uliyotumia, sasa kama method mbaya itavuruga. Ndilo ninalotaka kuwaambia, itavuruga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyuo vikuu ina maana wasichana watapungua idadi yao, si ni usawa tu, kila usawa una mipaka yake kwa hali halisi ya nchi yenyewe. Ndiyo maana mwanamke ni mwanamke na mwanaume ni mwanaume ingawa wote ni binadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Dkt. Damas Ndumbaro ameleta suala la bajeti ya Law School of Tanzania, suala hilo litaangaliwa. Kuhusu Mjumbe kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuwa ndio Mjumbe wa Governing Council, nakubali viko vyuo vingine 17 ambavyo pia naviheshimu sana.

Kwa hiyo, jambo hilo ni jambo la kujadiliwa, lakini wakati Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kinawekwa pale, ni kwa sababu ndicho ambacho kwa lugha ya Kilatini, primus inter pares. Huo ukweli pia hautafutika, kwamba Kitivo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika vitivo vyote vya sheria, siyo Tanzania tu, Afrika ya Mashariki ni primus inter pares.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana na wewe unafahamu, umekwenda mara nyingi Kenya. Nikifika Kenya huwa lazima niwatambie, tumewapa Kenya Majaji Wakuu watatu kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam; Jaji Chesoni, Jaji Gicheru na Jaji Mutunga. Tumewapa Uganda Jaji Mkuu Benjamin Odok; sasa hivi Jaji Mkuu wa Gambia Jalo ametoka Dar es Salaam. Kwa hiyo, kitabaki kuwa primus inter pares, kwa lugha ya kawaida first among equals (wa kwanza kwa walio sawa). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuvumilie tu, lakini hawazuiwi kubadili kama wakiona hawataki huyu wa kwanza kwa walio sawa aendelee kuwawakilisha. Ni hiari ya vituvo vya sheria. Na mimi kwa sababu pia nina conflict of interest, nitaacha jambo hilo liamuliwe na watu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uandikishaji wa watoto, Mkoa wa Ruvuma nao utafikiwa. Tulianza na pilot, sasa tutasambaza mikoa yote. Hii ilikuwa ni pilot scheme kuona ni jinsi gani itafanya kazi, lakini sasa itagusa watoto wa nchi yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la Kituo cha Kimataifa cha Utatuzi wa Migogoro ya Kibiashara, wazo hilo limechukuliwa linafanyiwa kazi na Tume ya Kurekebisha Sheria imeshakamilisha utafiti kuhusu Sheria mpya ya Usuluhishi, yaani Sheria mpya ya Arbitration na itakapoletwa tutashukuru sana kupata mchango wako ni jinsi gani ndani ya sheria hiyo tuwe na vifungu vya kuanzisha hii International Commercial Arbitration.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maoni mengi ya ndugu yangu, Mheshimiwa Lema, nimeyapokea. Amesema nisiwe muoga, inategemea nisiwe mwoga wa nini? Ninachoogopa ni kutenda dhambi na kuikosa pepo. Uoga huo wa kuogopa dhambi na kuikosa pepo, nitakuwa nao, lakini pia siwezi kuwa jasiri katika mambo ambayo hayahitaji ujasiri. Kwa hiyo, nimeyazingatia yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu matumizi ya Sheria ya Money Laundering, tutayafanyia kazi maoni haya yote aliyoyatoa. Kama kweli wako watu ambao wako ndani kwa money laundering ya dola 1,800 au kiasi fulani, basi ni suala la kupitia na kuona je, sheria ifanyiwe marekebisho?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Mheshimiwa Lema amesema tumeongea, niseme katika kesi hiyo ya Mwale, wale wawili wengine ni ndugu zangu, lakini sasa mimi ni Waziri wa Katiba na Sheria, lazima niheshimu utaratibu. Sikupenda kulisema, lakini ni vyema niseme kwamba kati ya wale wawili walioshtakiwa na Mwale, wawili ni ndugu zangu. Sasa tuache sheria iende na ningependa jambo hilo lishughulikiwe kwa mkondo wa sheria ili baadaye haki itendeke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Ndassa, masuala yako yamechukuliwa yote na yatazingatiwa kuhusu Mahakama hizo kumi na Mahakimu wanne tu, lakini pia ukarabati wa majengo ya Mahakama hizo katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Sabreena nakushukuru sana kwa uliyoyasema. Jambo lolote linaloondoa uhai wa binadamu linahitaji liangaliwe kwa umakini. Nchi yetu ilipita katika kipindi kigumu. Mauaji yale ya Rufiji na Kibiti hayakuwa ya kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme wakati mwingine Watanzania ni vyema tukakumbushana, nchi moja ya Ulaya ilipokabiliwa na aina hiyo ya matukio ilitoa amri kwa askari wake to shoot on sight, sitaitaja humu ndani ya Bunge kwa sababu siyo vizuri kuitaja nchi nyingine, lakini Balozi wa nchi hiyo alipokuja kuniona kwa mambo hayo nilimkumbusha, kwa sababu kipindi hicho nilikuwa naishi huko. Ilitoa amri ya ku-shoot on sight na Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe anajua. Sisi hatujafikia mahali, pamoja na matukio hayo ya idadi kubwa ya askari polisi kuuawa kutoa amri ya ku-shoot on sight. Kwa hiyo, nilimkumbusha Balozi yule kwamba hata ninyi mlipopita katika kipindi kigumu, mlifikia hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tujitahidi kuyakabili mambo hayo, tuombe Mwenyezi Mungu atusaidie kuepuka hayo. Kwa sababu mwanadamu akiondolewa hekima, busara na kiasi, anakuwa hayawani. Usimwite mwanao hayawani, kwa sababu hayawani ni lahaja ya kimvita kwa maana ya mnyama. Mwanadamu akishakosa hiyo, anakuwa hayawani. Kwa hiyo, tumwombe Mwenyezi Mungu atuepushe kuingia katika uhayawani ili tusiuane hovyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Mabaraza ya Ardhi, nichukue tahadhari hiyo niliyosema, tumeshaiagiza Tume ya Kurekebisha Sheria ili ituletee mapendekezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepokea maoni mengi ya maandiko ambayo mengi tumeshayajibu na tutawapa Waheshimiwa Wabunge wahusika ili wapate majibu tuliyowapa na mengine yanafanana na haya ambayo yameletwa na Kamati, kwa hiyo, ili tuweze kuwatendea haki wale wote waliotuletea maoni yao kwa maandishi, wote tumehakikisha kuwa wanajibiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mengi yamehusu Law School of Tanzania ambayo tayari nimeshayaeleza, mengine yamehusu Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuhusu kuboresha utendaji wao ambayo tayari Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameyajibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mengine yamehusu Tume ya Haki za Binadamu ambapo pia tumeeleza kwamba Tume ya Haki za Binadamu itatembelea sehemu zinazolalamikiwa yakiwemo Magereza na Vituo vya Polisi na taarifa itawasilishwa kwa wahusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo ambao wameomba Mahakama za maeneo yao, nao pia tutahakikisha tunatekeleza kwa sababu tulitoa ahadi. Kwa mfano, Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi ambaye alikuwa ameomba ile Mahakama ya Mtae ambayo imejengwa mwaka 1926 ifanyiwe ukarabati. Tutahakikisha katika mwaka huu wa fedha Mahakama hiyo ya Mtae huko Mlalo ambayo ina umri wa miaka mingi inafanyiwa marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Zainab Mndolwa Amir wa Viti Maalum CUF, naye amezungumzia kuhusu ukarabati wa majengo ya Mahakama, tutaendelea kuyafanyia kazi. Swali hilo hilo pia limeulizwa na Mheshimiwa Lucy Fidelis Owenya kuhusu ukarabati wa Mahakama, tutayafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najaribu kuangalia maswali ya upande wa pili ili nihakikishe nimeyagusia pia. Mheshimiwa James Millya wa Simanjiro, Mbunge wa CHADEMA kuhusu Tume ya Utumishi wa Mahakama Tanzania kumshauri Mheshimiwa Rais kufanya teuzi kutoka ndani ya mfumo wa Mahakama kwamba kitendo cha kuteua Majaji kutoka nje ya mfumo wa Mahakama kutawakatisha tamaa watumishi walio ndani ya Mahakama kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka tu kumjibu Mheshimiwa Millya kwamba sifa za mtu anayefaa kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu zimeainishwa kwenye Ibara ya 109(7)(a) mpaka (c), hizo ndiyo sifa. Na mimi niseme toka Majaji waanze kuteuliwa kutoka katika sehemu mbalimbali, imeleta tija kubwa katika Mahakama. Kwa hiyo, hii mixing ya watu kutoka ndani na nje ya Mahakama kwenye private practice na kwenye taasisi nyingine ambayo haivunji Katiba ya nchi, maadamu inazingatia sifa na inazingatia recommendations za Judicial Service Commission, utaratibu huo ni vizuri ukaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Mbunge wa Viti Maalum CHADEMA aliuliza kesi kuchukua muda mrefu Mahakamani. Napenda tu kumjibu kwamba hatua mbalimbali zimekuwa zikichukuliwa ili kukamilisha kesi na kuhakikisha hazichukui muda mrefu. Hii ni pamoja na kesi katika kila ngazi ya Mahakama kuwekewa muda maalum wa kukaa Mahakamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kila Hakimu na kila Jaji amepangiwa idadi maalum ya mashauri anayopaswa kumaliza kila mwaka na tatu, kila ngazi ya Mahakama iliyo na mashauri yasiyozidi umri uliowekwa katika ngazi inayoendeshwa, zoezi maalum la kuziondoa na kumaliza mlundikano, lakini pia kuendesha vikao vya case flow management na Bench-Bar Meetings zimesaidia sana kumaliza huo mlundikano wa kesi na kuupunguza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kesi ya Mwale ambalo liliulizwa na Mheshimiwa Lathifah Hassan Chande, Mbunge wa Viti Maalum CHADEMA; Mheshimiwa Lucy Fidelis Owenya, Mbunge wa Viti Maalum CHADEMA; Mheshimiwa Risala Saidi Kabongo, Mbunge wa Viti Maalum CHADEMA; na Mheshimiwa Juma Othman Hija, Mbunge wa Tumbatu CCM; majibu yameshatolewa. Kwa taarifa yenu, tarehe 20 Aprili, keshokutwa, Mahakama ya Rufaa itatoa uamuzi kuhusu appeal ya akina Mwale na hao jamaa wawili kuhusu suala zima la nolle prosequi. Kwa hiyo, tusubiri Mahakama ya Rufaa kesho kutwa itoe uamuzi kuhusu suala hilo ili tujue kesi hiyo inaendelea vipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la Serikali kuweka ukomo wa upelelezi wa kesi, swali ambalo liliulizwa na Mheshimiwa Lucy Fidelis Owenya, Mbunge wa Viti Maalum CHADEMA, napenda kusema kwamba kesi zinatofautiana. Kuna kesi zinazohusisha maslahi ya umma na nyingine huhitaji ushahidi kutoka nje ya nchi na hivyo kuchukua muda mrefu. Hivyo, siyo rahisi kuweka ukomo wa upelelezi wa kesi kwa sababu inaweza kuwa na athari kwa mhanga mwenyewe na mhalifu. Ni muhimu kuwa na mizania kwa pande zote. Kwa hiyo, siyo rahisi kusema upelelezi ukome lini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kuchanganya watuhumiwa wa makosa madogo, swali lililoulizwa na Mheshimiwa Lucia Michael Mlowe, Viti Maalum, CHADEMA, niseme kwa kweli uhalifu wote ni sawa na Penal Code yetu ilikuwa amended kuondoa tofauti kati ya felony na misdemeanor.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani palikuwa na tofauti ya felony na misdemeanor, lakini Penal Code Bunge hili hili liliondoa tofauti ya felony na misdemeanor. Kwa maana hiyo Tanzania leo hakuna kosa dogo wala kubwa, makosa yote yako sawa. Tukitaka turudi kwenye utaratibu wa felony na misdemeanor basi tubadili sheria hapa Bungeni ili tuwe na makosa ya misdemeanor ambayo ni makosa madogo na felony ambayo ni makosa makubwa. Bila kufanya hivyo, sasa Tanzania makosa yote yako sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mrundikano wa mahabusu Magerezani, hilo nalo limetolewa maelezo na litatolewa maelezo zaidi wakati wa Hotuba ya Wizara ya Mambo ya Ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lililoulizwa na Mheshimiwa Ritta Kabati kuhusu vitendo vya ukatili kwa wanawake, Tume inajitahidi kuchukua hatua za kushughulikia suala hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lililoulizwa na Mheshimiwa Risala Saidi Kabongo, Mbunge wa Viti Maalum CHADEMA, kuhusu Tume ina jukumu la kuchunguza uvunjwaji wa haki za binadamu na msingi wa utawala bora, mfano wananchi kukutwa kwenye viroba kando ya fukwe za bahari na kutekwa.

Napenda kusema kwamba kwa mujibu wa kifungu cha 33 cha Sheria ya Tume, Sura ya 391, taarifa zake za mwaka zinawasilishwa kwa Mawaziri wenye dhamana ya masuala ya haki za binadamu na utawala bora Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar. Tume imekamilisha taarifa zake hadi mwaka 2015/2016 na zitawasilishwa Bungeni mwaka ujao wa fedha. Aidha, taarifa za mwaka 2016/2017 ziko tayari na zinasubiri Taarifa ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema michango ya maandishi ni mingi na wote tumeijibu na tutahakikisha Wabunge wote wanapewa majibu yao kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja.