Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora

Hon. Mboni Mohamed Mhita

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Handeni Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa Fedha 2018/2019 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora

MHE. MBONI M. MHITA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naomba kutumia fursa hii kwanza kuwapongeza sana Waheshimiwa Mawaziri pamoja na Naibu Mawaziri kwa kazi nzuri ambayo wameendelea kuifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nitumie fursa hii kumshukuru sana kaka yangu Mheshimiwa Jafo kwa kiasi cha shilingi milioni 400 ambacho wametuletea Handeni Vijijini kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya kwenye Kata ya Kabuku. Pia ninashukuru sana maana nimeona tumetengewa bilioni moja na milioni mia tano kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya Mkata katika Jimbo la Handeni Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri tuna changamoro kubwa sana, naomba nikupe taarifa kwamba Wilaya ya Handeni kwa sasa ina Halmashauri mbili, Halmashauri ya Mji na Halmashauri ya Handeni Vijijini, kwa maelekezo ambayo tulikuwa tumepata ni kwamba Halmashauri ya Handeni Vijijini iondoke kwenda kuanza Ofisi mpya na zile Ofisi ambazo tulikuwa tukichangia na wenzetu wa Halmashauri ya Mji tuwaachie wenzetu wa Halmashauri ya Mji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa zaidi ni kwamba tulikuwa tunategemea pesa kutoka kwenye Serikali ili Handeni Vijijini tuweze kuhama na kuanzisha ofisi mpya. Kwa mshangao mkubwa zimeingia fedha kiasi cha bilioni 3.3 kwa maelekezo kwamba zile fedha ziende kwenye Halmashauri ya Mji ambao wao tayari wana ofisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba na hili nilishaongea na kaka yangu Mheshimiwa Jafo na nikamweleza mshangao mkubwa ambao nimeupata, kwa sababu nilitegemea hizi fedha zioweze kuja kwenye Halmashauri ya Handeni Vijijini ili ambao hatuna ofisi tuweze kuhama, lakini kwa mshangao mkubwa ni kwamba hizi fedha sasa zimekwenda kwenye Halmashauri ya Mji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa zaidi ni kwamba hizi fedha za miradi ambazo zimekuwa zikija katika maeneo yetu ni fedha nyingi ambazo kwa namna moja ama nyingine zinahitaji uangalizi wa hali ya juu na ndiyo hapa sasa nitaingia upande wa baba yangu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na nitajikita zaidi kwa Prevention and Combating of Corruption Bureau (TAKUKURU).

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiofichika kwamba rushwa inachangia umaskini kwa kasi ya juu sana. Ni dhahiri kwamba unapodhibiti upotevu wa fedha kwenye maeneo mbalimbali basi ni hakika kwamba unapunguza umaskini. Nayasema haya kwa sababu mimi ni mwanamke na nimeona ni jinsi gani ambavyo wanawake na akinamama wa Jimbo la Handeni Vijijini wamekuwa wakitembea umbali mrefu, wakihangaika kwenda kutafuta maji na siyo kosa lao na wala siyo kosa la Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imetuletea pesa kwa ajili ya miradi ya maji, lakini nasikitika kusema kwamba miradi yote ya maji ambayo ililetewa fedha katika Jimbo la Handeni Vijijini hakuna hata mradi mmoja ambao tumeona matokeo yake, kwa nini? Kwa sababu kumekuwa na ubadhirifu mkubwa sana wa fedha na kuna harufu ya rushwa katika miradi yote. Kuna mradi mmoja wa mabwawa ambao uliingiziwa bilioni nne na zile fedha mpaka leo zimeingia kwenye huo mradi, lakini mradi ule mpaka leo hakuna ambacho tumekiona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa na mradi wa visima ambao mpaka leo wananchi wa Jimbo la Handeni Vijijini hakuna ambacho wamenufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini sasa kifanyike? Naomba Serikali iweze kwa namna moja ama nyingine kuwawezesha wenzetu wa PCCB ama TAKUKURU kwa namna zifuatazo:-

Kuna maeneo mengine ambayo tumejionea kabisa kwamba Ofisi za TAKUKURU haziko katika kiwango ambacho kinatakiwa ama zile basic needs za ofisi, pia wawezeshwe kwa vitendea kazi kama magari. Nasema haya kwa sababu wangekuwa na vitendea kazi ambavyo viko imara hakika wanaweza kufanya kazi zao kwa umahiri na kufika kwenye maeneo hayo na kuepusha upotevu mkubwa sana wa fedha ambazo kuna baadhi ya Watumishi wamekuwa siyo waaminifu sana, wamekuwa wakitumia zile fedha kwa manufaa yao wenyewe na matokeo yake wananchi wetu wameendelea kuteseka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu yangu, naomba nitoe reference kwa wenzetu wa Luxemburg, wenzetu wa Sweden ambao wao wana National Anti-Corruption Unit, wenzetu wa Finland ndiyo Mashirika makubwa ama taasisi kubwa za uzuiaji wa rushwa duniani zinazoongoza. Kigezo kikubwa ambacho kimefanya hizi taasisi katikan hizi za Sweden na Finland kuongoza ni kwa sababu ya transparency na access to information ama uwazi na upatikanaji wa taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali ofisi zetu ziwe na ushirikiano na wenzetu hawa wa TAKUKURU ili taarifa ziweze kupatikana, kwa sababu kama tunavyoona hawa ni prevention and combating, lakini tumezoea kuona kwamba wao wanafanya combating zaidi siyo prevention. Kwa hiyo, naamini kwamba wakiwa na access ya kupata taarifa basi wataweza kuepusha matumizi mabaya ya fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niokoe muda wako, naomba nihitimishe kwa kusema tu:-

Moja; naomba sana Serikali itusaidie kuweza kuona nini ambacho kimetokea katika Wilaya ya Handeni hasa kwenye hizi bilioni tatu na milioni mia tatu. Mbili; Uwezeshwaji wa wenzetu wa TAKUKURU. Tatu; Waweze kupata ushirikiano hasa kwenye access to information na transparency ambayo ni uwazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutumia fursa hii kukushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuongea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.