Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Sixtus Raphael Mapunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba iliyowasilishwa na Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi.
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, naomba niungane na wale waliochangia jana kumpongeza Waziri kwa jinsi anavyofanya kazi zake vizuri na tukijua kwamba Wizara hii ni kubwa na ndiyo iliyobeba uchumi wa nchi yetu. Kwa jinsi anavyofanya kazi zake, nimpongeze na nitakuwa miongoni mwa wale watakaokuwa wanakesha Makanisani kumwombea awe na nguvu hizo ili matumaini kwa Watanzania walio maskini yapate kufikia katika kiwango kinachostahili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze kwenye kuchangia hoja hii kwenye mambo matatu. Jambo la kwanza ni suala la ruzuku ya pembejeo. Waziri ameeleza vizuri na amefafanua changamoto zilizojitokeza. Nimwombe atakapofika kufanya majumuisho aweke mambo yafuatayo ili angalau wakulima wapate faraja na wapate ahueni waweze kuiona kesho yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaishukuru Serikali kwa kuweka ruzuku ya pembejeo lakini kimsingi ile ruzuku ukiitazama vizuri kuna maeneo haiwasaidii wakulima ambao wanatarajiwa. Ruzuku ile ya pembejeo kuna asilimia mkulima anapaswa kulipa ili apate ile seti ya mbolea ya kupandia, mbolea ya kukuzia, pamoja na mbegu, anatakiwa atoe hela wakati yeye hana hela. Ukiangalia kwenye tathmini nani ana sifa ya kupata ile ruzuku unajikuta yule ambaye anapelekewa hana uwezo hata wa kununua huo mfuko au nusu mfuko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Wizara ifanye mambo yafuatayo:-
Kwanza ipeleke ile ruzuku kama mkopo mapema, ipeleke mbolea ya kupandia, ya kukuzia na ipeleke mbegu. Baada ya mavuno sasa wale wakulima ndiyo walipe ile gharama ya pembejeo. Tukifanya hivi hali itakuwa nzuri sana kwa wakulima wangu wa mahindi kule Lipilipili, Luangai, Masimeli, Ruvuma Chini, Mpepai, Mzopai na Kikolo. Ukiyafanya haya Mheshimiwa Waziri utawafanya watoke kwenye mstari wa umaskini waende juu zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Mbinga na hususan Jimbo la Mbinga Mjini limegawanyika katika maeneo mawili. Eneo la kwanza ni milimani la wakulima wa kahawa na eneo la pili ni bondeni ambao ni wakulima wa mahindi. Hawa wote ni Watanzania ambao wanahitaji Serikali kwa namna yoyote ile iwasaidie. Huo mfumo wa ruzuku ya pembejeo umeelekezwa kwenye mazao ya kilimo cha mahindi tu hawajaelekeza kwenye zao la kahawa. Wale ndugu zangu wa milimani hawakupenda kuzaliwa kwenye maeneo ambayo hayastawishi mahindi, ni Mwenyezi Mungu aliwaumba wakakaa kule milimani ambako ukipanda mahindi hayawezi yakastawi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali itazame hili kwa jicho la upekee kidogo, itoe ruzuku vile vile ya dawa na mbolea kwenye mazao ya biashara hususan kahawa. Tukifanya hivi, ndugu zangu wa kule Miyangayanga, Mateka, Mundeki, Luwaita, Kagugu, Sepukira, Utiri, wataweza kupata ahueni ya maisha yao na wataiona kesho yao katika hali nzuri zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye sehemu ya pili ambayo wenzangu waliongelea jana kuhusu tozo nyingi zinazowakumba wakulima wa kahawa na wakulima wa mazao mengine. Kuwa specific, niliongelee zao la kahawa. Mnunuzi wa kahawa huwa analipia leseni kwenye Bodi ya Kahawa, analipa Dola 1,024 lakini akitaka kwenda kununua kahawa aidha amekwenda Mbinga, Mbozi au Kagera, akifika kule atakutana tena na leseni nyingine ya ununuzi wa kahawa kwenye halmashauri husika. Hizi gharama ambazo unampelekea mnunuzi wa kahawa zikisambaa zinakwenda kumuumiza mkulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiondoa gharama hii, kuna makato mengine hata ukiyatazama unashindwa kuyaelewa. Kuna gharama ya kulipia Tanzania Coffee Research Institute – TACRI ambapo kwa kila mkulima aliyeuza kahawa kwa kilo moja ya kahawa unailipia 0.075 kwenda kwenye kitengo hiki cha research. Vile vile wanakatwa kuna kitu kinaitwa Tanzania Coffee Development Fund ambayo ni 0.10 wanalipa kwa kila kilo ya kahawa.
Mheshimiwa Naibu Spika, najiuliza haya makato yakishatokea na ikatokea labda sehemu fulani wakulima wamepata magonjwa ya mlipuko, sijawahi kuona sehemu yoyote pesa inatoka kwenye hii Mifuko kwenda kuwasaidia wakulima. Matokeo yake wakulima wanatafutiwa mfumo mwingine wa kulipwa, wanakuwa double charged! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri, hebu aangalie huo Mfuko kwa ajili ya maboresho ya kilimo cha kahawa unafanya kazi gani? TCDF, ile 0.10 anayokatwa kila mkulima kwenye kilo yake ya kahawa inaenda kufanya nini? Sisi kule Mbinga tumepata ugonjwa wa vidung’ata, kule wanauita viporomba, ukashambulia kahawa matokeo yake wale wakulima wakakatwa kila mkulima kwenye kilo yake kulipia hiyo na wakati walikwishalipa wakijua kabisa kuna Mfuko ambao utawasaidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni ushuru. Kwa mujibu wa sheria mkulima atapaswa kulipa 0% - 5% kwa kila kilo kwa ajili ya ushuru wa halmashauri. Hii range ya 0% - 5% imewekwa kwa halmashauri kuamua waweke wapi. Nimejaribu kuuliza hata kwa wenzangu wa Mbozi nao kule ni 5% haishuki, imebaki kwenye 5% pale pale nao wanaumia kama tunavyoumia sisi Mbinga.
Mheshimiwa Naibu Spika, haya yote yanasababishwa na hizo tozo nyingi ambazo huko juu wanazichukua. Wakizichukua hizi tozo huko juu wanasababisha halmashauri zishindwe kuendeshwa na kwa sababu watu wa karibu ni wale wakulima, watawabana tu wakulima, hali hii haitaweza kuondoka hata siku moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho ni uhakika wa masoko na bei kwa mazao yote, mazao ya kilimo na mazao ya biashara katika ujumla wake. Kuna jambo nadhani hatujalifanya vizuri katika kutazama. Hivi tatizo la mkulima ni bei, uzalishaji au gharama za uzalishaji? Maana haya mambo matatu usipoyaweka katika level zake unaweza ukatatua tatizo ambalo si tatizo. Ukitizama kila mkulima analalamika, tumelima soko hakuna. Sisi tunakwenda ku-address soko na wakati tatizo ni gharama za uzalishaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kinachomfanya mkulima alalamike na anung‟unike ni ile pesa ambayo inaitwa mtaji, kaenda kuichukua kwenye SACCOS, VICOBA, UPATU, akaiingiza kwenye matuta yake mawili, mwisho wa siku anapata kidogo kuliko kile alichokiweka. Niiombe Serikali ijaribu kuangalia namna nzuri itakayowezesha kupunguza gharama za uzalishaji kwa mkulima ili azalishe katika hali nzuri. Hata kama soko likiyumba badaye maumivu yanakuwa madogo sana kwa sababu, gharama ya uzalishaji ilikuwa ni ndogo kuliko ile gharama ya kuuzia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii tena kurudia kwanza kumshukuru na kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri aliyoifanya na anayoendelea kuifanya. Pili, nimshukuru na kumpongeza Waziri Mkuu kwa hotuba yake iliyoonesha uelekeo na kuonesha Serikali ya Awamu ya Tano itakwenda kufanya nini. Mwisho kabisa, nimshukuru kaka yangu Comrade Mheshimiwa Mwigulu Lameck Nchemba kwa kazi anayoifanya. Nikuombe kaka yangu wewe pigana, pambana kweli kweli lakini katika kufanya shughuli zako usisahau kutenga siku kadhaa twende Mbinga ukaone jinsi gani wakulima wanavyosulubika kule. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.