Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi mchana huu wa leo na mimi nichangie kwenye hoja iliyo mbele yetu.

Awali ya yote kama ilivyo ada na mimi nitoe shukrani zangu za dhati kwa wahudumu wanaohudumu kwenye Wizara hii hasa Mawaziri, lakini siyo Mawaziri peke yao kwa sababu hizi sifa ambazo Mawaziri wanazipata ni kwa sababu ya wale wanaowa-support. Kwa hiyo, nao wanastahili sifa nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli Wizara hii wanaitendea haki, nami nawaombea kwa Mwenyezi Mungu waendelee kuifanya hii kazi kama ambavyo Mwenyezi Mungu atawajalia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba tu Serikali ya Awamu ya Tano, mara zote ninapoanza kuchangia pengine naweza kuonekana kama mlalamishi, lakini ni lazima ukweli usemwe. Nini Kanda ya Kusini tunaikosea nchi hii? Kwa sababu kila ninaposimama kwenye bajeti, ukiangalia Kanda ya Kusini inavyotendewa na kanda nyingine ni tofauti. Kwa nini nasema hivyo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Kanda ya Kusini hatuna Hospitali ya Kanda ya Kusini, lakini kuna Kanda nyingine tayari zina Hospitali za Kanda. Kanda ya Kusini ukiangalia kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri, pesa iliyotengwa haina tofauti na pesa ambazo zimetengwa kwenye Hospitali za Wilaya nyingine, kwenye sehemu nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Kanda ya Kusini tumetengewa shilingi bilioni moja, lakini iko mikoa au wilaya zimetengwa zaidi ya shilingi bilioni mbili mpaka shilingi bilioni nne kwenye Hospitali za Mikoa. Kwa nini Kanda ya Kusini mnatusahau kwa kiwango hicho? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ukiangalia hospitali yetu ya kanda yenyewe kwanza haipo na wanasema ile Hospitali ya Ligula ndiyo ambayo wanaiandaa kuwa Hospitali ya Kanda, lakini hizi shilingi bilioni moja kwanza hatuna uhakika kama zitafika. Tunaomba Serikali ya Awamu ya Tano mwiangalie Kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mzuri tu, maana nikisema lazima nitoe mifano. Kuna huu Mkoa wa Geita umetengewa zaidi ya shilingi bilioni nne, lakini Mkoa wa Geita uko Kanda ya Ziwa. Kanda ya Ziwa wana Bugando, Kanda ya Kaskazini wana KCMC; sisi Kanda ya Kusini hatuna Hospitali ya Kanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana Mheshimiwa Waziri unayehudumu kwenye hii Wizara uiangalie sana Kanda ya Kusini. Sasa naomba nirejee kwenye nafasi ya utumishi.

T A A R I F A . . .

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naipokea taarifa hii hundred percent. Nafikiri hata mimi nili-overlook tu pale. Kwa hiyo, Geita ni shilingi bilioni tano. Kanda ya Kusini shilingi bilioni moja.

T A A R I F A . . .

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, hapana. Taarifa hii haiwezi kupokelewa kwa sababu mimi nimetoa mfano. Ningeweza kutoa mfano mkoa wowote ule, lakini kwa sababu Mkoa wa Geita ni Mkoa wa watani zangu, ni watoto wangu na wajukuu zangu, nikautolea mfano huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naongelea suala la wahudumu. Suala hili naweza kuliona kama ni janga la kitaifa kwa sababu tatizo hili ni kubwa sana. Pamoja na juhudi kubwa ya Serikali ya kujenga miundombinu ya afya, lakini kama hatujaliangalia suala la watumishi, itakuwa hizi juhudi zote tunazozifanya haziwezi kutuzalia matunda yaliyotegemewa. Kwa mfano, nataka niwaambie kwamba jambo hili kwanza linaweza likapunguza hata ufanisi wa wale watumishi wachache na vilevile kuweza kuwaletea madhara mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kuna hospitali moja, nurse mmoja alipigwa makofi na mgonjwa. Sababu ilikuwa ni nini? Yule nurse alikuwa peke yake kwenye wodi, kuna akina mama wawili wanajifungua, mmoja akajifungua mapema kuliko yule mwingine. Wakati anamhudumia yule mama, hajamaliza hata kufunga kitovu, yule mama mwingine na mtoto ameshatoka anataka kudondoka. Sasa yule nurse alichokifanya, kuogopa yule mtoto asije akadondoka akafa, mama akapoteza mtoto, aliamua kumwacha yule mwingine kabla hajamfunga kitovu akamhudumia yule mwingine bila kubadilisha gloves. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa yule mama kwa sababu aliona kile kitendo cha kumpokelea mwanae mama ambaye hajabadilisha gloves zenye damu za mama mwingine kwa kuogopa maambukizi ya UKIMWI, akamzaba makofi. Hata hivyo yule nurse alikuwa na mambo mawili ya kuamua, amwache mtoto aanguke afe au ampokee mtoto apate maambukizi aweze kutibiwa. Kwa hiyo, hili suala tunaweza kuliona dogo, lakini ni kubwa sana. Uhaba wa ma-nurse na madaktari ni mkubwa sana. (Makofi)

Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri ulichukulie katika muktadha huo kwamba hili jambo ni la muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nilitaka niongelee kwenye hospitali yangu ya Wilaya ya Liwale. Hospitali ya Wilaya ya Liwale ina wodi tano kama juzi nilivyosema. Wodi moja ya wazazi, moja ya wanaume na nyingine ya watoto. Pia kuna wodi mbili za grade II, lakini kwa night shift panaingia nurse mmoja tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hebu just imagine nurse mmoja anahudumia wodi tano, ufanisi wake utakuwa wapi? Siyo kwamba anakwenda night atapata off, hakuna off kwa sababu ya uhaba wa watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, niko chini ya miguu yake aiangalie Hospitali ya Wilaya ya Liwale, hali ni mbaya sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba nijielekeze kwenye upande wa lishe. Na mimi nitoe utaalam wangu kidogo, ni-declare interest, mimi ni msindikaji wa nafaka kwa taaluma. Tanzania hatuna Sera ya Ulaji na ndiyo maana ulaji wetu unakuwa wa hovyo hovyo na ndiyo maana tunapata magonjwa hayo yasiyoambukiza na mengine yanayoambukiza kama vile kisukari, kwa sababu tunakula hovyo hovyo. Nitolee mfano kwenye nafaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, National Milling wakati ule tunasindika nafaka tulikuwa tunakoboa mahindi asilimia 80, tunatoa unga kwa asilimia 80, lakini leo hii Tanzania tunatoa kwenye hizi coat meal tunatoa asilimia 55 mpaka 60. Maana yake ni nini? Tunakoboa mpaka vitamini zote tunaziondoa, baadaye sasa tukirejea kwenye mahospitali, mtu akipata sukari akienda hospitali ndiyo anaenda kuambwa kwamba ukale dona.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini Serikali isiweke sera tukajua kwamba standard ya sembe ni standard inayokobolewa kwa kiwango gani au mchele, unakobolewa, unapigwa polish mpaka unakuwa mweupe unapoteza kila kitu. Kwa nini Tanzania hatuna sera? Ukienda kwa wenzetu hapo Nairobi maximum rate percent kwamba kukoboa ngano, kwanza tunapoteza nafaka. Kwa mfano, kama asilimia 60 ndiyo flour ambayo inatumika, ina maana asilimia 40 zote unawaachia mifugo. Sasa hata nafaka yenyewe tunapunguza. Ina maana kwamba hata njaa nayo tunaiendekeza sisi wenyewe kwa sababu ya ulaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tukiingia kwenye suala hili la lishe, naomba Serikali waje na sera, ijulikane standard ya ulaji kwamba chakula gani kinaliwa kwenye standard gani na TBS wawe wanafuatilia hizi standard ili kuhakikisha watu wetu wananufaika na masuala haya ya lishe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba niongelee kwenye hii Taasisi ya JK na ya MOI. Ukiangalia kwenye jedwali hapa, kamati walishasema hapa kwamba mwaka 2017 wametengewa fedha lakini zilizoenda ni zero. Kwenye Taasisi ya JK ni zero, kwenye Taasisi hii ya MOI ni zero. Sasa pamoja na sifa kubwa, Mheshimiwa Rais juzi alikwenda kwenye Taasisi akawasifia, lakini kwa trend hii ya kutowapelekea pesa mnataka wafanye nini? Kwa nini basi tunatenga hizi fedha wakati hamko tayari kuzipeleka?

Mheshimiwa Naibu Spika, hili jambo nalisema kwenye Wizara hii, lakini linahusu sana Wizara ya Fedha. Kwa sababu Kamati zote zinazokuja mbele yetu hapa, malalamiko makubwa kwenye fedha za maendeleo haziendi. Sasa Taifa gani hili ambalo tunataka kulijenga kwamba tunakusanya pesa kwa ajili ya kulipa mishahara tu, lakini hatutengi fedha za maendeleo? Tunakusudia nini? Hivi tunataka kujenga Taifa la namna gani? Kwa sababu kila Wizara itakayokuja hapa, kila Mwenyekiti anayekuja hapa anasema fedha za maendeleo haziendi.

Mheshimiwa Naibu Spika, afya, fedha za maendeleo haziendi; Taasisi hizi, fedha ya maendeleo haiendi. Sasa ina maana pamoja na kujinasibu kwamba Serikali ya Awamu ya Tano makusanyo yamepanda, hivi tunakusanya kwa ajili ya kulipa mishahara? Kama hatutaki kuwekeza kwenye hizi taasisi kwa kutoa fedha za maendeleo, sidhani kama tunaweza tukafanya kile tunachokusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba niende kwenye sera za wazee. Hapa tumeshaweka sheria nyingi sana; kuna dirisha la wazee, sijui kufanyaje wazee, kuna matibabu sugu ya wazee, lakini hawa wazee ni wapi? Kwa sababu hatujapata sheria hapa inayowatambua wazee. Ikiletwa sheria hapa, itaweza kuainisha hawa wazee tunaowakusudia ni wazee wa namna gani?

Mheshimiwa Waziri, kila mwaka tunakuomba utuletee sera hii ya wazee ili hawa wazee tuweze kuwatambua.

Nini tatizo? Kigugumizi ni cha nini cha kuwaletea sheria hawa wazee ili watambuliwe? Mpaka leo hii tunaongelea wazee, lakini wazee wenyewe tunaowaambia tunawatengea madirisha, tunawatibu bure, bado hatujawatambua kwa mujibu wa sheria ni wazee wa aina gani?