Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Wizara hii ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kunijalia afya na nguvu na mimi niweze kuchangia katika Bunge lako hili Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimpongeze Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, kwa kazi kubwa anayoifanya kwani mwenye macho haambiwi tazama. Pia nimshukuru Waziri wangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Ndugulile na watendaji wote, kwani kazi wanayoifanya Watanzania hakika wanaiona. Mimi naamini hakuna cha kuwalipa ila Mwenyezi Mungu mwenyewe ndiyo atajua cha kuwalipa ninyi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwenye vituo vya afya. Kwanza nimshukuru Waziri, Serikali yangu tukufu kwa kunitengea shilingi milioni 700 kwa ajili ya Kituo cha Afya Mlola, sasa hivi naamini mambo ni mazuri kabisa, tumetengewa shilingi milioni 700 kwa maana hiyo shilingi milioni 400 kwa ajili ya majengo na milioni 300 kwa ajili ya vifaa tiba, kwa hiyo naishukuru Serikali yangu Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wilaya ya Lushoto, Halmashauri ya Lushoto, Jimbo la Lushoto lina kituo cha afya kimoja tu ambacho kiko Mlola. Kwa hiyo, kituo kile hakitoshelezi kabisa mahitaji ya wananchi. Kwa hiyo, niiombe sasa Serikali yangu kwa kuwa wananchi wa Gare, wananchi wa Ngwelo wamejitahidi wenyewe wamejenga vituo vya afya mpaka kufikia mtambaa wa panya na majengo mengine yamepauliwa, niiombe Serikali sasa safari hii itenge pesa za kutosha kwa ajili ya kumalizia vituo vile kwa maana ya Kituo cha Gare na Kituo cha Ngwelo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hayo, hospitali yetu ya Wilaya imeelemewa. Wilaya ya Lushoto ina takribani Majimbo matatu, Halmashauri mbili, kwa maana ina wakazi zaidi ya 600,000, ultra sound na x-ray ya Lushoto ni ndogo sana haikidhi mahitaji. Kwa hiyo, tunakosa wananchi wengi sana pale, wanapoteza maisha kwa sababu ya x-ray ile ni ndogo sana, ikihudumia watu watano tu inakufa. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu tukufu na sikivu ipeleke x-ray yenye uwezo ili kuweza kuhudumia wananchi wale, hususan kuokoa maisha ya mama na mtoto pamoja na wananchi wengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, gari la wagonjwa niiombe Serikali, Mheshimiwa Ummy anajua kwamba Wilaya ya Lushoto jiografia yake ni mbaya sana, ni ya milima na mabonde. Kwa hiyo, chondechonde, kwa kweli hali ni mbaya. Juzi nikiwa niko Jimboni nilishuhudia vifo vya akina mama watatu wamekufa kwa ajili ya kifafa cha mimba kwa sababu ya kukosa usafiri kufika katika Hospitali ya Wilaya. Kwa hiyo, nimuombe dada yangu Mheshimiwa Ummy, naomba Land Cruiser, siyo vile vigari vidogo maana naamini anajua barabara za kwetu, nimuombe atupatie Land Cruiser ili kuweza kuhudumia hususan wananchi wa Mlola, Makanya, Bwelo, Mlalo, Mbwei, Malibwi pamoja na Kwai. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni suala zima la walemavu. Kule kwetu ni vijijini mno kiasi kwamba walemavu hawapati huduma. Kwa hiyo, niiombe Serikali sasa ipeleke hususan vifaa kwa walemavu hususan walioko vijijini, hasa kule Lushoto maeneo ya Makanya, Mavului, Manolo pamoja na Mbwei, kwani ukiangalia hali halisi ilivyo takwimu zinazoletwa na wataalam kutoka Halmashauri ni potofu siyo sahihi, kwa hiyo niiombe Serikali yangu sasa ipeleke vifaa vya kutosha hususan vya walemavu katika maeneo yale ya Lushoto.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.