Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na mimi niweze kuchangia kwenye bajeti ya Wizara hii ya Afya na Maendeleo ya Jamii. Kwanza kabisa naunga mkono mapendekezo ya Kamati maana na mimi ni Mjumbe wa Kamati hiyo ya Huduma na Maendeleo ya Jamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo kubwa kabisa ni upungufu na uchakavu wa zahanati na katika jimbo zima la Mikumi lenye kata 15 lina vituo vya afya viwili tu; yaani Kituo cha Afya cha Ulaya na Kituo cha Afya cha Kidodi ambacho tunashukuru sana tulipokea shilingi milioni 400 kwa ajili ya kukitanua na kukiboresha ili kiweze kuokoa maisha ya mama zetu na watoto pia kufanya upasuaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vituo viwili tu vya afya kwenye jimbo zima la Mikumi havitutoshi, Kituo cha Afya cha Ulaya kina hali mbaya sana, kimechakaa sana lakini pia kina upungufu mkubwa sana wa watumishi wa afya, wananchi wanateseka sana, wengi wanakimbilia hapo lakini kusema ukweli huduma zimekuwa mbaya sana na kuumiza sana wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, zahanati zetu katika Jimbo la Mikumi zina hali mbaya sana na mimi kama Mbunge nimeshirikiana bega kwa bega na wananchi wenzangu wa Kata ya Malolo (vijiji vya Chabi na Mgogozi) kujenga zahanati mbili na tupo kwenye umaliziaji, lakini pia kwenye Kata ya Masanze zahanati ya Kijiji cha Dodoma Isanga niliezeka kwa Mfuko wa Jimbo pia. Zahanati ya Kijiji cha Muungano na Nyali ambapo nimezikarabati pia kwa kupitia Mfuko wa Jimbo mwaka 2016/2017 lakini bado tuna changamoto kubwa sana kwenye Jimbo la Mikumi na tunaomba sana Mheshimiwa Waziri aweze kutusaidia kuunga mkono jitihada hizi za wananchi wa Jimbo la Mikumi.

Lakini pia Mji Mdogo wa Mikumi ambao kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2012 inaonesha kuwa kuna idadi ya watu wapatao 21,113 lakini Zahanati ya Mikumi imechakaa sana na ina uwezo mdogo sana wa kuhudumia wananchi hawa ambao wengi ni akina mama. Hivyo tunaomba sana Mheshimiwa Waziri na Serikali iweze kuboresha na kutanua ujenzi wa Zahanati ya Mikumi kuwa Kituo cha Afya ili kuondokana na adha ya huduma ya afya wanayoipata wakazi wa Mji Mdogo wa Mikumi; lakini pia Serikali iweze kusaidia ukarabati wa Zahanati za Uleling’ombe, Zombo, Kisanga, Tindiga, Vidunda, Mhenda, Ruhembe na Mabwerebwere na pia jiografia ya Jimbo la Mikumi ni mbaya sana hivyo tunaomba sana Serikali iweze kutusaidia magari ya wagonjwa ili tuweze kuokoa maisha ya akina mama na watoto ambao wengi sana wanapoteza maisha kwa sababu ya ukosefu wa ambulance na usafiri wa uhakika.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Mji Mdogo wa Mikumi una hopsitali ya taasisi ya dini ya St. Kizito ambayo imekuwa ikitoa msaada mkubwa sana kwa wananchi wa mji wa kitalii wa Mikumi, lakini pia watu wa mataifa mbalimbali wanatumia barabara kuu ya Tanzania mpaka Zambia mpaka Afrika Kusini.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na umuhimu wa hospitali hii ya St. Kizito, Serikali ilikuwa inatoa ruzuku na kulipa mishahara ya baadhi ya watumishi, lakini katika hali ya kusikitisha hospitali hii haijapata ruzuku hii kwa miaka kadhaa mfululizo na nilipokwenda kuzungumza nao walisema walikuwa wanapewa shilingi milioni 60 kwa mwaka ambazo kwanza zilikuwa hazitoshi. Lakini pia kwa sasa hawajazipata kwa miaka mitatu mfululizo, lakini pia kuna tetesi kuwa Serikali imeamua kusitisha mikataba na hospitali hizi muhimu za taasisi za kidini ambazo kwenye Wilaya yetu ya Kilosa zipo mbili yaani St. Kizito na Hospitali ya Berega ambayo ipo pia kwenye Wilaya yetu ya Kilosa. Tunaomba sana majibu ya Mheshimiwa Waziri ili tujue wameamua kuvunja mikataba yao na hospitali hizi za taasisi za kidini? Na kama jibu ni hilo Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wananchi wa Wilaya ya Kilosa hasa Jimbo la Mikumi ambao wengi ni maskini na gharama za huduma ya afya zimekuwa kubwa sana na wameshindwa kuzimudu kutokana na taasisi hizo kutoza pesa nyingi kwa wananchi ili ziweze kujiendesha.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna upungufu mkubwa sana wa Maafisa Maendeleo kwenye kata zetu nyingi za Jimbo la Mikumi, lakini pia kwa masikitiko makubwa sana nifikishe malalamiko makubwa sana kwa Afisa Maendeleo ya Jamii Wilaya ya Kilosa kwa kufanya kazi zake kisiasa zaidi na kushindwa kushirikiana na taasisi zinazotaka kuja Wilayani Kilosa hasa Jimboni kwangu Mikumi kwa kushindwa kutoa vibali kwa taasisi hizo zinazotaka kuja kutoa elimu kwa wananchi hasa vijana, akina mama na wazee ili waweze kujiunga kwenye vikundi na kushirikiana na Ofisi ya Mbunge na Serikali ya Wilaya ili waweze kujiletea maendeleo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna taasisi isiyokuwa ya Kiserikali ambayo inaitwa Tanzania Bora Initiative ambayo ilionesha nia njema ya kuja kutoa elimu na kuwaunganisha vijana kwenye Jimbo la Mikumi na Handeni na walifuata taratibu zote za Kiserikali ili waweze kusaidia wananchi wa maeneo hayo, lakini katika hali ya kusikitisha Afisa Maendeleo ya Wilaya ya Kilosa mpaka sasa anawapiga chenga kuwapa kibali cha kufanya kazi hii njema ya kuwafanya wananchi wajiunge pamoja na kujiletea maendeleo, tena kwa kushirikiana na Serikali bila sababu za msingi na wamefuatilia kibali hicho cha kuja kufanya shughuli hizo muhimu kwa wananchi wa Wilaya ya Kilosa, Jimboni Mikumi ili waweze kushirikiana na Serikali yao kujiletea maendeleo yao. Ahsante sana.