Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua nafasi hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kuanzia kwa Mheshimiwa John Pombe Joseph Magufuli, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Makamu wa Rais na Waziri wetu mama yetu mpendwa Ummy Mwalimu, Naibu Waziri Mheshimiwa Faustine Ndugulile na watendaji wote wa Wizara na ngazi zote kwa kutatua changamoto ya upungufu wa miundombinu ya majengo, dawa, vifaatiba na rasilimali watumishi kwa ujumla; kuendelea kuboresha sera yetu ya afya nchini na kusimamia utekelezaji wa Ilani ya CCM 2015 hadi 2020.

Aidha, naungana na Watanzania wenye nia njema pamoja na wananchi wa Jimbo langu la Mbulu Mjini kwa maombi na mapenzi makubwa kwa Serikali ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kutoa ushauri wangu kwa Serikali kuhusu bajeti inayowasilishwa ya Wizara hii kwanza, kuendelea kutoa nafasi kubwa ya ajira kwa sekta hii ya afya kupitia mipango yetu ya ikama kila mwaka. Pili, kuongeza uwezekano wa mashine za x-ray katika Hospitali za Wilaya na vituo vya afya ili kuleta tija zaidi, tatu, kusimamia matumizi ya mashine za kielektroniki katika vituo vya afya, zahanati, hospitali za wilaya, rufaa kote nchini ili kuongeza mapato na nne, kusimamia mpango wa kila Mtanzania anaetaka Bima ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika tano, kufufua bodi za afya za zahanati, vituo vya afya na hospitali za wilaya kulingana na muda wa ukomo wao wa uteuzi; sita, kuendelea kuhamasisha kliniki ya wanaume na wajawazito ili kujenga ushawishi wa uzazi wa mpango; saba, kuitaka MSD kutumia dawa zenye muda mrefu katika hospitali zetu; nane, kuona na kutathmini mpango wa PPP katika hospitali binafsi unanufaisha jamii au wapokee huduma kwa kiasi gani badala ya kuboresha hospitali zetu, hata hivyo, mpango huu wa ubia wa sekta binafsi haumpunguzii mpokea huduma gharama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa kuna madeni makubwa ya malipo ya masaa ya ziada katika Halmashauri za Mji wa Mbulu, hospitali hiyo iliyokuwa ya Wilaya hapo awali inakabiliwa na upungufu wa watumishi hivyo basi naomba sana OC inayotolewa itumike kwa vigezo vya bajeti kinyume na matumizi mengine.

Pia naomba Serikali ione umuhimu wa kuona inafanya maandalizi ya watumishi wapya kwa vituo vya afya vya Daudi, Thawi na Dongobeshi kwani mahitaji hayo mapya ya miundombinu yanaweza kufanya majengo hayo yasitoe huduma. Kwa sasa hospitali ya Wilaya ya Mbulu iliyoko Mbulu Mjini inatoa huduma asilimia 30 kwa wananchi wa Jimbo la Babati Vijijini, Mbulu Vijijini na Karatu hivyo kupewa mgao wa dawa kwa kuangalia takwimu za sensa ya mwaka 2012 haitakidhi haja ya huduma bora. Hata hivyo Halmashauri ya Mji ya Mbulu kupitia Baraza la Madiwani walishatuma taarifa hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa idadi ya watoto walemavu ni kubwa, Serikali ione kila Halmashauri inateua shule moja ya msingi na sekondari na kufanya marekebisho ya miundombinu yake ili kundi hili lipate elimu kwa maisha ya baadae katika jamii yetu na kizazi kijacho.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa katika Hospitali ya Wilaya, baadhi ya vifaatiba havipewi vipaumbele mfano shule, blanketi, vifaa vya matibabu ya macho na meno kitendo kinachofanya wataalam hao kutokutoa huduma na katika vikao vya Baraza la Madiwani ukihoji wakati wa bajeti kauli ni kwamba ukomo wa bajeti hauruhusu, mfano ni Hospitali ya Wilaya ya Mbulu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho Mheshimiwa Waziri wa Afya nimemuomba atembelee Hospitali ya Wilaya ya Mbulu kwa kuwa ni mali ya Serikali na kwa kuwa tayari mwaka jana alitembelea Hospitali ya Rufaa ya Hydom na kituo cha afya katika mwezi wa Juni. Pia ziara hii ni ahadi yake, Mungu akitujaalia hasa siku ya Jumamosi moja ili Jumapili Mheshimiwa awahi kwenye majukumu yake. Katika ziara hiyo aweze kutembelea Tarafa ya Nambis ambako tarafa hiyo haina kituo cha afya hata kimoja na ina akina mama wengi sana kwa maelezo nitatoa maelezo zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho ninawatakia kazi njema na majukumu mema katika kutumikia Wizara hii muhimu sana kwa mustakabali wa maisha yetu na Taifa kwa ujumla. Ahsante sana.