Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali za kuboresha huduma za afya nchi nzima. Wilaya yetu ya Mbogwe tumebahatika kupatiwa jumla ya shilingi milioni 800. Kituo cha Afya Masumbwe kimepatiwa shilingi milioni nne na Kituo cha Afya Iboya shilingi milioni 400; fedha hizi zimetengwa mahususi kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya upasuaji, nyumba za waganga, nyumba kwa ajili ya maabara na famasia na majengo kwa ajili ya kuhifadhia maiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaipongeza Serikali kwa mikakati yake pia ya usambazaji wa dawa muhimu za binadamu kupitia MSD.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu ya Awamu ya Tano inafanya kazi kubwa sana katika kuhakikisha kuwa tunapata magari kwa ajili ya kuhudumia wagonjwa (ambulances).

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali kwa kutupatia magari ya kubebea wagonjwa katika vituo vyetu viwili vya afya vya Iboya na Masumbwe. Hongera sana Serikali kwa kazi nzuri. Aidha, nashauri Serikali iendelee na mkakati wake wa kuunga mkono jitihada za wananchi kujenga na kumalizia majengo ya vituo vya afya na zahanati katika vijiji na kata mbalimbali Wilayani Mbogwe. Wilaya ya Mbogwe inakabiliwa na changamoto ya kutokuwa na Hospitali ya Wilaya. Naomba sana Serikali itoe fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali hii ya Wilaya ili kusaidia utoaji wa huduma za afya zinazotolewa na vituo vya afya na zahanati Wilayani Mbogwe ili kupunguza utegemezi wa wagonjwa wa Wilaya yetu kutibiwa katika Hospitali za Wilaya za Bukombe, Kahama na Geita.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninajua Serikali yetu inafanya kazi kubwa sana kuhakikisha afya za Watanzania walio wengi zinaboreshwa. Ninaamini wazi kuwa siku za usoni Taifa letu la Tanzania litakuwa likitoa huduma bora zaidi katika ukanda huu wa Afrika Mashariki, Kati na Kusini mwa Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali zetu za Jakaya Kikwete, Hospitali ya Taifa ya Rufaa ya Muhimbili zimepata sifa kutokana na utoaji wa huduma bora kabisa za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania ya viwanda itajengwa na Watanzania wenye afya bora na kwa hakika Wizara ya Afya imejipanga vyema kuhakikisha nchi yetu inakuwa na Watanzania walio na afya bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe Serikali iendelee kutoa kipaumbele katika kutoa fedha kwa wakati ili kuhakikisha miradi ya maendeleo katika sekta ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto za uhaba wa watumishi, vifaatiba na madawa zinapaswa kushughulikiwa ili kuhakikisha huduma za afya zinapatikana karibu kabisa na wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.