Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Hawa Abdulrahiman Ghasia

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mtwara Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye ameniwezesha afya njema na kuweza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu ili na niweze kuichangia bajeti ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia niipongeze Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya kwa pamoja na Makamu wa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa Majaliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Mwigulu Nchemba pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Olenasha kwa kazi nzuri waliyonayo katika kuiongoza Wizara hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi zangu, napenda nichangie katika maeneo yafuatayo:-
Eneo la kwanza ni eneo la kilimo, hususan zao la korosho. Ulianzishwa mfuko wa kuendeleza zao la korosho na madhumuni ya mfuko ule, pamoja na mambo mengine lakini pia kujenga viwanda vya korosho. Mfuko ulianza kwa kutuahidi kwamba tutaanza kujenga viwanda vitatu vya korosho, maeneo yakachaguliwa, lakini mpaka sasa hivi, imebaki ni hadithi, hatujui huo mfuko unapata shilingi ngapi na zinatumika vipi?
Kwa hiyo, tunaomba sana Mheshimiwa Waziri, huu mfuko ni lazima kwanza ukaguliwe na pia tuangalie, kwa sababu mara ya mwisho tumeoneshwa asilimia 41 tu ndiyo inayoenda katika kuendeleza zao la korosho. Kinachobaki kwa kweli hakieleweki, sana sana kinaenda kwenye utawala. Kwa hiyo, naomba uangalie sana katika eneo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili napenda pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kupunguza makato katika zao la korosho. Nimtahadharishe Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba kuna watu wamejipanga huko kuja kumwomba arejeshe baadhi ya makato.
Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba uendelee kuwa na msimamo wako huo huo, usibabaishwe wala usitetereshwe na baadhi ya watu wanaotaka kukuyumbisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni suala la uendeshaji wa minada, katika suala zima la Stakabadhi ya Mazao Ghalani. Huu mfumo ni mzuri sana na wananchi wanaupenda sana, tatizo uwazi hauko vizuri. Tumeelezwa katika kikao cha RCC kwamba korosho mwaka huu imenunuliwa mpaka shilingi 2,950 lakini kitu cha kushangaza, anakuja Afisa Ushirika anasimama anasema kwamba wanasiasa ndio wanaosumbua katika zao hili la korosho. Anasema kwamba sisi katika Wilaya yetu, koroshozimeuzwa kwa shilingi 2,060 tu. Sasa zile bei zinazotajwa kwenye RCC na ambazo wanatajiwa wananchi, kidogo kuna utata. Wakitafuta sifa, wanatutajia bei ya juu; wanapotaka kwenda kuwapa wananchi, wanashusha ile bei. Sasa tuelewe vipi?
Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka Mheshimiwa Waziri atakapokuja kutoa ufafanuzi, atuambie mwaka huu Korosho zimeuzwa kwa shilingi 2,950 au zimeuzwa kwa shilingi 2,060? Tupate ufafanuzi wa hilo ili wananchi wetu waweze kupata haki. Sasa hivi tunavyozungumza, Tandahimba vyama 149 wanadai zaidi ya shilingi bilioni 1.4 na hayo ni maelezo ya Mkuu wa Wilaya na Masasi pia wakulima wanadai pesa zao za korosho.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba wananchi wapate malipo yao. Wananchi wote wanaohudumiwa na MAMCU na TANEKU ambao wanadai malipo yao ya pili, walipwe ya mwaka huu na miaka mingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nilitaka kulichangia ni suala la wavuvi. Ukiangalia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri utakuta kuna pembejeo za wakulima na pia kuna pembejeo na jinsi ya kuendeleza wafugaji. Ukija kwa upande wa wavuvi, sana sana kuna mikakati ya kuzuia uvuvi haramu; hatukatai, lakini tungependekeza suala hilo liende sambamba na kuwawezesha wafugaji kwa vifaa; vitendea kazi. Wavuvi wetu wengi wanavua kwa kutumia zile zana za zamani.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka wakati Mheshimiwa Rais Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, akiwa Waziri wa Uvuvi, kwa kweli alikuwa na mipango mizuri sana ya kuwawezesha wavuvi. Na mimi katika Wilaya yangu alikuja katika maeneo ya Msangamkuu, wakawawezesha wavuvi katika Kijiji kimoja tu, alitoa zaidi ya shilingi milioni 250. Sasa baada ya yeye kuhamishwa Wizara ile, mipango ile yote iliishia pale pale. Naomba Mheshimiwa Waziri Mwigulu Nchemba uangalie mipango ile, pamoja na kwamba ilikuwa inapitia MACEMP lakini ilisimamiwa na Waziri Mheshimiwa Dkt. Magufuli kipindi kile akiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi. Tunaomba wavuvi wawekewe mipango thabiti ya kuwaendeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, naomba niongelee suala la wafugaji. Wafugaji wanahangaika kwa sababu wanatafuta malisho na maji kwa ajili ya mifugo yao. Tunaomba katika bajeti yako ioneshe mnajenga majosho mangapi na mnawatengea maeneo gani waende lakini pia wapatiwe maji, kwa sababu kitu kikubwa kinachowafanya wanahangaika wanaende kugombana na wakulima ni kutafuta maji na malisho.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba maeneo yatengwe ya wakulima yajulikane na ya wafugaji yajulikane, lakini ya wafugaji, tunaomba mwongeze kuwawekea majosho pamoja na maeneo ya kunyweshea mifugo yao, hapo ndipo mtakapoweza kuwafanya wafugaji wasihame eneo moja hadi lingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hii naomba wasiachiwe Halmashauri peke yao, Halmashauri wana majukumu mengi sana ya kutekeleza katika ngazi zao zile. Tuiombe Wizara mama ndiyo itoe mchango wa kuziwezesha Halmashauri kule chini ili ziweze kujenga majosho. Tukiwaachia Halmashauri peke yao kwamba watenge maeneo wao, wao wajenge majosho, kwa kweli tutakuwa tunawaonea.
Wizara itenge pesa kwa kushirikia na hizo Halmashauri ili kujenga majosho pia na kujenga maeneo ya kunyweshea hiyo mifugo. Napenda nimalizie kwa kuwashukuru sana wapiga kura wangu wa Jimbo wa Mtwara Vijijini kwa kuniamini kwa kipindi cha tatu, kuwa Mbunge wao. Napenda niwahakikishie kwamba sitawaangusha, nitafanya kazi na wao bega kwa bega, kwa maendeleo ya Jimbo letu la Mtwara Vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nasisitiza tena suala la wavuvi kuwezeshwa, si suala tu la kwenda kuwakamata kuchoma nyavu zao na uvuvi haramu. Hakuna mtu anayependa kuvua kwa kutumia baruti, vijana wetu wanakufa; lakini wanafanya vile kwa sababu hawana mitaji, hawana zana za kuwawezesha kupata nyavu za kisasa, boti za kisasa na kupata injini za kuwawezesha kwenda kuvua katika kina kirefu. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja atueleze, wavuvi ametutengea kiasi gani na za kufanyia nini? Maana yake siku zote tunasikia doria.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia wavuvi na wenyewe wanatozwa tozo nyingi sana kwenye leseni; akitoka Mtwara anatozwa, akienda Kilwa anatozwa, akienda Msumbiji anatozwa. Tunaomba akilipia leseni, basi iwe ni hiyo hiyo, lakini kuna tozo nyingi sana; kila anachokwenda kukivua kule baharini kinatozwa. Kwa hiyo, nasema kabisa na lenyewe tuliangalie.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa upande wa wakulima wetu hasa wa zao la Korosho, tumesikia sasa hivi kuna suala commodity exchange, lakini sisi kama Wabunge hatujapata hata maelekezo, huo mfumo unaendaje ili tukawe wapambe wa kukusaidia mfumo huo kufanya kazi.
MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.