Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Omari Mohamed Kigua

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watumishi wote wa Wizara kwa hotuba yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitachangia maeneo yafuatayo nikianza na kuongezeka kwa madai na kutokuwepo kwa ukusanyaji wa madeni kwa Hospitali yetu ya Muhimbili kwa mujibu wa taarifa ya CAG ya tarehe 30 Juni, 2016 yalifika shilingi bilioni 30.8 ilikilinganishwa na mwaka uliopita ya shilingi bilioni 17 sawa na ongezeko la asilimia 45. Hali hii si nzuri hata kidogo na hii inaashiria kwamba uongozi wa Hospitali ya Muhimbili hausimamii vyema eneo hili, je, tatizo ni Kitengo cha Fedha? Wizara lazima ihakikishe madeni yote yanakusanywa kwa sababu fedha ndio ikakayosaidia kuimarisha huduma za afya ukizingatia hii ni hospitali inayotegemewa na Watanzania wengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo lipo tatizo la madai ya bima za afya yaliyokataliwa ya shilingi bilioni 1.86; kiasi hiki kimekataliwa kulipwa na makampuni ya bima eti kwa sababu ukaguzi ulibaini, mfano NHIF ilikataa madai ya shilingi milioni 241.97 ya Hospitali ya Muhimbili ikidai ni madai ya madawa ambayo NHIF ilibaini hayakutolewa kwa waganga. Udanganyifu huu ulifanywa na watumishi je, hatua zipi zimechukuliwa na Serikali kwa watumishi hawa? Mheshimiwa Waziri naomba majibu ya kina juu ya mapungufu ambayo kwa hakika hayapaswi kufungiwa macho hata kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ukarabati wa vyuo vya CDIIS na fedha za maendeleo; changamoto ya kukarabati vyuo vya maendeleo (CDIIS) ni suala linalopaswa kutupiwa macho sana, nipongeze juhudi ambazo Wizara mmeonesha kufanya ukarabati kwa baadhi ya vyuo hivi, vyuo hivi ni muhimu sana, vimesaidia vijana wetu kuzalisha wataalam katika sekta ya ujenzi na ufundi, kuna umuhimu mkubwa kwa Wizara kuhakikisha inaweka msisitizo wa kufuatilia fedha za maendeleo kukarabati vyuo hivi kwani itasaidia kupunguza tatizo la ajira nchini. Waasisi wa nchi hawakufanya makosa kuvianzisha vyuo hivi, nikuombe Mheshimiwa Waziri na uongozi mzima wa Wizara jitahidi pia mtoe mafunzo ya kutosha kwa walimu (lectures) ili watu kuongeza ujuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi la kupandisha Kituo cha Afya Songe kuwa Hospitali ya Wilaya; niipongeze Serikali kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kutupatia kiasi cha shilingi milioni 500 kukarabati kituo chetu cha afya Songe. Wizara ya Afya ndio wenye dhamana ya Hospitali za Wilaya, kituo hiki kina sifa zote za kupandishwa kuwa Hospitali ya Wilaya baada ya ukarabati huu kwa sababu tumepatiwa pia shilingi milioni 220 kwa ajili ya vifaatiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, jitihada hizi zinatoa fursa kwa kituo chetu kuwa na sifa zote za kuwa Hospitali ya Wilaya, nimuombe Mheshimiwa Waziri atume timu kwenda Wilayani Kilindi kufanya tathimini ya kitaalamu na wakiridhika kituo hiki kipandishwe hadhi, Wanakilindi wanauhitaji mkubwa wa Hospitali ya Wilaya tunayo Hospitali ya Rufaa ya KKKT lakini yapo malalamiko makubwa kwa gharama kubwa na huduma dhaifu inayotolewa na hospitali hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.