Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Martin Alexander Mtonda Msuha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. MARTIN M. MSUHA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nichukue nafasi hii kuwapongeza Waziri na Naibu Waziri wa Wizara ya Afya kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya katika kuhudumia Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie katika maeneo yafuatayo:-

Kwanza ni uhaba wa vituo vya kutolea huduma za afya; Halmashauri ya Mbinga ina jumla ya kata 29, tarafa tano na vijiji 121, lakini kuna zahanati 42 tu na vituo vya afya viwili hivyo kufanya upungufu wa zahanati 79 na uhaba wa vituo vya afya 27. Pamoja na upungufu huo wa vituo vya afya Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga haikuletewa fedha za upanuzi/ujenzi wa vituo vya afya kama ilivyofanyika kwenye Halmashauri zingine. Hivyo basi niiombe Wizara iweze kutuletea fedha za upanuzi wa vituo vya afya vifuatavyo; Kituo cha Afya Mapera, Kituo cha Afya Kindimba Chini na Kituo cha Afya Matiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu uhaba wa watumishi; kwa idadi ya vituo vya kutolea huduma za afya tulizonazo Mbinga DC tuna mahitaji ya watumishi 324 wa kada mbalimbali za afya lakini waliopo ni 112 tu hivyo kufanya upungufu wa watumishi 212. Serikali ifikirie kwa haraka walau kutupatia watumishi 22 wanaohitajika ili vituo/zahanati mpya nne zilizokamilika hivi karibuni ziweze kufunguliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jengo la NACP/NTLP Joint Office; Programme za NACP/NTLP walikuwa na mradi wa ujenzi wa ofisi ya pamoja iliyopo Luthuli nyuma ya Ofisi za WHO. Jengo hilo lilikuwa linajengwa kwa ufadhili wa Global Fund. Tangu mwaka 2013 Global Fund waliacha kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi huo hivyo jengo hilo la ghorofa tatu limekwama na limeanza kuchakaa. Niiombe Wizara iangalie uwezekano wa kutenga fedha kwa ajili ya kukamilisha jengo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Hospitali ya Mloganzila, niipongeze Serikali kwa ujenzi wa hospitali hiyo. Niiombe Serikali kuipa jicho la pekee hospitali hiyo kwa maana ya kupeleka watumishi wa kutosha. Wananchi wamekwishaanza kutoa malalamiko kuwa ukipelekwa Mloganzila basi unapelekwa pahali ambapo hapana usalama na uhakika wa tiba, vifo ni vingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.