Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia. Nitangulie kwa kuunga mkono hoja na kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri na namshukuru Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu na watendaji wa wizara kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa 81 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri umetupa faraja sana sisi watu wa Bagamoyo, lakini tuseme kwa Taifa zima la Tanzania kwamba sasa majadiliano yanafikia ukomo. Mwezi Juni mwaka huu mkataba utasainiwa kwa ajili ya ujenzi wa bandari kubwa ya Bagamoyo. Hii ni bandari ya ukombozi kwa dhana (vision) ya China Merchant na Serikali ya Oman kwamba hili ndilo lango kuu la uingiaji katika nchi za Afrika Mashariki, ni ukombozi kwa ajili ya uchumi wetu na 2025 bila shaka tutaweza kufika katika hali nzuri zaidi tukiwa na bandari hii kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani majadiliano yamechukua muda mrefu, sasa ni miaka sita na kwa maana hiyo naiomba Serikali yangu ijitahidi sasa katika utekelezaji wa mradi huu kwa sababu miaka sita ni kipindi kirefu. Kipindi hicho sisi tulikuwa tunafanya majadiliano lakini China Merchant wamejenga bandari Djibouti, Tin Can Island, Nigeria; Abidjan, Ivory Coast; Colombo Sri Lanka kwa hiyo, kipindi hiki tumepitwa na mambo mengi sana. Nadhani sasa niiombe Serikali yangu kufanya haraka sana katika kuhakikisha kwamba utekelezaji unaenda kwa haraka zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili utekelezaji huu sasa, mwekezaji aweze kuanza kazi, wananchi wangu wale 687 ambao hawajalipwa fidia walipwe fidia. Fidia ya jumla ambayo ilikuwa bilioni 57 na ikalipwa 45, ile tofauti nayo sasa ilipwe ili ardhi hii iwe free mwekezaji aweze mara moja kuanza kuweka miundombinu ya bandari katika eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiweza kumaliza tatizo hilo litakuwa jambo zuri sana, lakini wananchi hawa kilio chao kikubwa zaidi ni wapi wanaenda kuishi. Wananchi hawa ambao wanapisha bandari waliahidiwa na Serikali. Naomba niweke mezani barua hii ya EPZ ambayo iliwaahidi wananchi hawa kupewa sehemu ya kuweza kwenda kujenga makazi yao na eneo lilikuwa limeshatengwa na hivi sasa mpango huo upo kwenye mtihani haieleweki kama watapewa makazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ni kaya 460, Kijiji kizima cha Pande kinaondoka kwa ajili ya mradi huu; kaya 460, wananchi 1,670, tunapowaambia tu ondokeni nendeni mkaishi mahali popote wataenda kuishi wapi, kuna wazee, wajawazito, walemavu na watoto wadogo; wapi wanaenda shule yao na zahanati ipo pale, hawajui mahali pa kwenda. Wakitaka kwenda Zinga, Zinga ipo kwenye mpango wa EPZ ambao nao wanatakiwa waondoke kuna kaya 2,269, wakisema waende Kondo nayo inaondoka, kuna kaya 418, wakisema waende Mlingotini, nayo inaondoka kuna kaya 694 yaani hawana sehemu ya kwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa taratibu nzuri za nchi yetu ni kuhakikisha kwamba faida hii ya maendeleo ya Tanzania, basi wananchi hawa wanahama wanaenda mahali ambapo wataanza kuishi vizuri, vinginevyo tutatengeneza ombaomba, watu ambao hawana mahali pa kuishi. Kati yao wengi wamepata fidia ambayo haitawawezesha kununua ardhi wala kujenga nyumba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila mpango wa resettlement, haitawezekana wananchi hawa wakaweza kuishi katika maisha ambayo yatakuwa ya heshima bila kutengeneza ombaomba katika mradi huu mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili nalisisitiza sana, hili wananchi wangu wanalia sana, lisipoweza kutokea maana yake tutakwenda kuwahamisha wananchi pale kwa mitutu ya bunduki na sidhani kama Mheshimiwa Rais wetu jambo hili anapenda kulifanya. Naomba sana Mheshimiwa Waziri alisimamie ili ahakikishe linafanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa 129 kuna habari njema ya ujenzi wa barabara ya Bagamoyo – Saadan – Pangani mpaka Tanga, hii ni habari njema ni ahadi ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi ya miaka mingi. Namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kuweka hili, lakini… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)