Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii nami nichangie kwenye hoja iliyopo mbele yetu. Nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa wingi wa baraka zake ambazo amezidi kutukirimia siku hadi siku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kumpongeza na kumshukuru sana Naibu Waziri, ndugu yangu Mheshimiwa Kwandikwa kwa ziara aliyoifanya kule Mkinga. Nashukuru sana kwa sababu ziara ile ilijenga matumaini kwa watu wa Maramba, Gombero, Mtonibombo, Daluni, wakijua kilio chao cha muda mrefu sasa kimepata jibu, lakini nimepitia vitabu hivi, bahati mbaya sana kilio chao hakijasikika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kutoka Mabokweni – Maramba – Bombomtoni – Umba – Kisiwani – Same - Mkomazi ni barabara ya kuunganisha Mkoa wa Tanga na Kilimanjaro, ni barabara ya kimkakati, kiuchumi na ni barabara ya ulinzi. Ni barabara ambayo wagombea wetu wote wa urais kila wakati wa kuomba kura wamekuwa wakiipitia barabara hiyo, ni barabara ambayo imepewa ahadi mara nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi hawa wamekuwa na subira sana kwa barabara hii lakini barabara hii ni kero na imekuwa mateso kwao. Nilikuwa nasoma kitabu hiki nikadhani angalau safari hii tutaona neno feasibility study inafanyika kwa barabara ile lakini hakuna. Ni barabara ambayo nimeisemea sasa kwa miaka saba mfululizo, lakini Serikali haisikii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii mzee wangu Mheshimiwa Kikwete alipopita aliposikia kelele hizi akasema tuiweke kwenye utaratibu wa Performance-Based Management and Maintenance ili angalau iwe inapitika, tukafanya hivyo. Baadaye tukasema iingizwe kwenye mpango maalum kupitia MCC, namshukuru sana dada yangu aliyekuwa Mkuu wa Mkoa, dada Chiku Galawa akapambana tukaleta maombi barabara hii itengenezwe kupitia MCC, lakini haikuwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano alipokuja kwenye kuomba kura ndugu zetu wa Maramba wakaomba, akasema amesikia. Alipofika Daluni Kibaoni pale wananchi wakamlilia, akatoa ahadi. Tumeisemea barabara hii lakini kwa masikitiko makubwa kilio chetu hakijasikika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi kweli barabara inayounganisha Mbuga ya Saadani na Mbuga ya Mkomazi hatuioni umuhimu wake? Hivi kweli barabara inayounganisha Mbuga ya Tsavo na Mbuga ya Mkomazi na Kilimanjaro hatuioni umuhimu wake? Hivi kweli tunashindwa kukamata kundi la watalii kutoka Mombasa ili waje kutembelea eneo la Mto Umba na Mbuga ya Saadani mpaka Kilimanjaro hatuoni umuhimu wake? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi barabara inayotupa uhakika wa usalama wa nchi yetu kiulinzi hatuoni umuhimu wake? Hivi barabara inayopita kwenye maeneo ya uzalishaji wa kahawa, chai, mpunga, mkonge hatuoni umuhimu wake? Barabara hii haituweki vizuri kisiasa. Mheshimiwa Waziri alikuwa Mjumbe wa Kamati Kuu ya chama chetu, ninaposema barabara hii haituweki vizuri kisiasa, najua anaelewa. Naomba kilio hiki kisikike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni bandari. Pale Mkinga tuna wawekezaji wa Hengya Cement na kampuni ya Sinoma wameamua kuja kuwekeza pale watajenga viwanda kumi. Miongoni mwa viwanda hivyo kutakuwa na kiwanda kimoja cha cement chenye uwezo wa kuzalisha tani milioni saba kwa mwaka. Maana yake unazungumzia kiwanda ambacho production inayofanyika sasa nchini inakuja kufanywa na kiwanda kimoja. Tunazungumzia uwekezaji wa trilioni 7.5.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameomba pamoja na uwekezaji huo, wapewe ruhusa wajenge gati itakayowawezesha kusafirisha mizigo yao wenyewe. Wanataka kujenga gati ile kwa utaratibu Build Operate and Transfer watumie fedha zao wenyewe. Sasa huko bandarini kuna mtu nasikia ameweka ngumu hataki kutoa kibali. Uwekezaji wa trilioni saba kuna mtu mmoja anakwamisha, hatuwezi kukubali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisipopata majibu ya kuridhisha nakusudia kushika shilingi. Waheshimiwa Wabunge, naomba kwenye hili mniunge mkono. Hatuwezi kuacha uwekezaji mkubwa wa trilioni saba uzuiwe na mtu mmoja. Hatuwezi kukubali ajira ya watu 4,000 izuiwe na mtu mmoja eti ana ndoto ya kutujengea bandari ya Tanga iwe na uwezo wa kuwa valid kwa miaka 200 ijayo, lakini wakati akisema hayo sisi tunazo taarifa watu wa Tanga kwamba tangu mwaka 77 kwenye business plan ya Mamlaka ya Bandari imekuwa ikisema itajenga Bandari ya Mwambani haijatokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kuna mtu ana hela zake anataka ajenge gati ili uwekezaji mkubwa wa namna hii utokee sisi tunaweka ngumu, haiwezekani. Wakati tunaweka ngumu hii ya kuruhusu kujenga gati pale Pangani Mamlaka hiihii ya Bandari imejenga gati, kwa nini Pangani tujenge gati lakini Mkinga iwe nongwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaunga mkono hoja nikipata majibu ya uhakika. Nashukuru.