Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili nichangie kwenye hoja iliyo mbele yetu. Naomba nianze mchango wangu kwa maneno mawili: Nangurukuru na Liwale, nitatoa ufafanuzi baadaye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba mchango wangu kwa leo kabla ya kusema chochote, kwanza nawashukuru Mawaziri wote wanaohudumu kwenye Wizara hii kwa utendaji wao. Nasikitika tu kwamba wataangushwa na Mheshimiwa Mpango kwa sababu ili waonekane kwamba kweli wanaweza Mheshimiwa Mpango lazima awape pesa. Naomba vilevile kuwashukuru siyo tu Mawaziri na watendaji wote wanaohudumu kwenye Wizara hii na taasisi mbalimbali kwa kazi zao nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze mchango wangu kwa kujielekeza kwanza kwenye mawasiliano. Sekta hii ya mawasiliano kama sitakuwa nimesahau tunao mfuko unaoitwa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote, ambao una pesa zake ambazo zimeandaliwa kisheria. Napata mashaka ninaposikia kwamba mfuko huu unashindwa kutekeleza baadhi ya miradi kwa kukosa fedha wakati hawa fedha zao zipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Mpango awape fedha hawa USCAF ili waweze kufanya kazi. Watu wa USCAF wanafanya kazi nzuri sana kwa sababu kwanza kazi zao wanajikita zaidi vijijini ambako kunasemekana huko hakufikiki kibiashara. Sasa kama Serikali ya Awamu ya Tano inasema kwamba ni Serikali ya wananchi wa hali ya chini, basi ni vizuri sana kwenye sekta ya mawasiliano ikawapa fedha mfuko wa USCAF ili waweze kutimiza majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano katika Halmashauri yangu ya Wilaya ya Liwale haifikiki kwa barabara, redio au mitandao ya simu. Hivi navyoongea kwenye halmashauri ile kuna Kata za Mpigamiti, Ngongowele, Milui, Lilombe, Mkutano, Mtungunyu, Ndapata na Kimambi ili uweze kupata mawasiliano na ndugu zako ni lazima upande juu ya miti au juu ya vichuguu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili linatupa shida sana hata wafanyakazi kama Walimu na watumishi mbalimbali wanashindwa kukaa kwenye maeneo haya kwa sababu ya kukosa mawasiliano. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali iwapatie fedha hawa jamaa wa USCAF waweze kutuhudumia ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie kwenye mtandao wa barabara ya Nangurukuru – Liwale. Nashukuru Mheshimiwa Waziri kwa mwaka huu nimeona kwenye vitabu barabara ya Nachingwea - Liwale iko kwenye upembuzi yakinifu na detailed design, nashukuru kwa hilo. Nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri barabara ya Nangurukuru - Liwale kwa maana ya Liwale na Mkoa wa Lindi kwa ujumla wake ni barabara ya kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyoongea pamoja na kwamba zao la korosho limefanya vizuri sana kwenye soko la kimataifa lakini sisi Liwale tunakwama sana, korosho zetu zinakaa ghalani muda mrefu, tunashindwa kufanya minada kwa wakati kwa sababu korosho zetu zinashindwa kutoka Liwale kufika Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri hii barabara siyo tu kwamba ina umuhimu vilevile imeongelewa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na ni barabara ambayo inarudiwa mara kwa mara. Naomba Mheshimiwa Waziri aitazame barabara hii ya Nangurukuru - Liwale kwa jicho la huruma sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nataka niongelee barabara inayotoka Masasi - Nachingwea – Nanganga. Barabara hii tayari upembuzi yakinifu umekamilika miaka miwili, mitatu ya nyuma iliyopita. Barabara za Masasi - Nachingwea; Nachingwea – Rungwa; Ruangwa – Nanganga; Nanganga - Nachingwea msipoziwekea lami itakuwa ni miujiza kupata lami katika barabara ya Nachingwea - Liwale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nasisitiza Mheshimiwa Waziri waijenge hii barabara ya Masasi - Nachingwea – Nanganga; Ruangwa - Nachingwea ili nami niweze kupata hii barabara ya Liwale - Nanchingwea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze kwa upande wa madaraja. Mheshimiwa Waziri atakapokuja mara ya pili ku-wind up ajaribu kuniambia. Kuna miradi mingine utakuta daraja linapangwa moja moja lakini madaraja mengine yamewekwa kwenye makundi. Kwa mfano, sisi kwenye halmashauri yetu kuna daraja linalotuunganisha Nachingewa na Liwale la Mbwemkulu, ni daraja refu na kubwa sana na ndiyo kikwazo kikubwa cha kupeleka korosho Nachingwea mpaka Mtwara na sijaliona kwenye vitabu hapa likikumbukwa. Sijui Mheshimiwa Waziri wana mpango gani na hili daraja la Mbwemkulu linalounganisha Nachingwea na Liwale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nataka nijielekeze kwenye hizi taasisi zilizoko chini ya Wizara hii, kwa mfano TTCL. Tumeamua tuwekeze kwamba TTCL ifanye biashara lakini ina madai makubwa sana kutoka kwenye taasisi zingine za Serikali. Naomba TTCL walipwe pesa zao ili tuweze kuwapima utendaji wao baada ya kupata mtaji. Leo hii hatuwezi kuwapima TTCL utendaji wao wakati hatujawapa pesa, wanadai pesa zao nyingi taasisi nyingine za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nataka niungane na Mtemi Chenge, anasema ni utaratibu mzuri kuamua kujenga reli ya standard gauge lakini ni lazima tutafute fedha au wahisani ili watusaidie speed iongezeke na vilevile Serikali iweze kupumua ili sehemu nyingine napo wapate pesa. Maana leo hii kila tukiamka reli, ndege, as if hatuna shughuli zingine za kufanya kama Serikali. Naomba Serikali mkope pesa kwa mkopo nafuu au kutafuta wahisani ili reli hii tuijenge kwa speed inayotakiwa na Serikali iweze kupumua na kutekeleza miradi mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee Kampuni ya Meli ya Maziwa Makuu. Kama kweli tumeamua kuifufua kampuni hii ni lazima tukubali tuchukue madeni yake Serikali wawalipe wafanyakazi ili tuwape mitaji hawa watu ndiyo tuweze kuwapima. Nashukuru taasisi nyingi kwenye Wizara hii zimepata viongozi wazuri sana ,tena wazalendo na wenye moyo lakini kama hatutawapa pesa za kutosha, hatutaweza kuwahukumu baada ya miaka miwili, mitatu ijayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze kwenye upande wa bandari. Kuna miradi mingi sana ya bandari imetajwa hapa, lakini nataka niwaambie kwamba sisi zamani Mkoa wa Lindi tulikuwa na Bandari ya Lindi, tulikuwa na meli ya MV Lindi. MV Lindi na Bandari ya Lindi imekufa na kwenye vitabu vya Mheshimiwa Waziri haipo. Naomba sana Bandari ya Lindi nayo waikumbuke kama ni kuifanyia ukarabati au kuijenga upya lakini sisi kama Lindi tunahitaji bandari…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.