Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kunipa uwezo nami niweze kuchangia katika hotuba hii ya Waziri wa Ujenzi na Mawasiliano. Kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia uhai na kunipa nguvu niweze kuchangia katika hotuba yako hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Rais wangu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya ambayo imetukuka ambayo haina mfano. Hata hivyo, nataka nimwambie kaza buti, watasema sana na watochonga sana, lakini kaza buti mwendo uwe uleule. Kuna hadithi ya Mtume inasema: basi wapendelee wenzako vile vitu ambavyo unavyovipendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija Mathayo 22:34–39 inataja upendo, wapende au mpende jirani yako kama vile unavyoipenda nafsi yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiofichika kwamba, Rais anawapendelea Watanzania kuliko hata familia yake. Huu ni ukweli ambao haujafichika na watu ambao wanabeza basi, ujue hawa wana lao jambo, lakini kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu atamjalia Rais wetu, atamjalia miaka mingi na atatimiza kazi hii na wao watasema baada ya Mheshimiwa Rais kustaafu ndio watajua kwamba, Rais wetu anafanya nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimshukuru Waziri Mheshimiwa Profesa Mbarawa na timu yake, Naibu Waziri Mheshimiwa Nditiye na Naibu Waziri Mheshimiwa Kwandikwa kwa kazi kubwa wanayoifanya, Mungu atawalipa, sisi hatuna cha kuwalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika kuchangia sasa. Nimshukuru Rais wangu na niishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inaongozwa na Rais wangu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kunipatia barabara ya lami kilometa moja kila mwaka. Kwa hiyo, nimwombe sasa Waziri Mheshimiwa Profesa Mbarawa, kilometa hii ni chache sana, kwani naamini kabisa inaenda kwa kusuasua, niombe iongezwe hata iwe kilometa mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila ninapopata nafasi naongelea barabara kupandishwa hadhi, barabara ya kutoka Mlalo – Ngwelo – Mlola – Bakanya – Bilingano hadi Mashewa na ikitoka Mashewa inaenda kwa Mheshimiwa Kitandula mpaka Chongoleani Tanga, kule Mabokweni. Barabara hii Waziri Mheshimiwa Profesa Mbarawa aliniahidi kwamba, itapandishwa hadhi mwaka huu na niliongea nae na akajiridhisha kwa Meneja wa TANROADS Mkoa wa Tanga akaambiwa kila kitu kiko vizuri. Nashangaa kwenye bajeti hii siioni barabara ile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Profesa Mbarawa hebu aniambie, nitumie style gani, ili barabara yangu aweze kuipandisha? Watoto wa mjini wanasema nitoke vipi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha sana, unaposema barabara ya Lushoto ina maana umesema uchumi wa Lushoto. Barabara hiyo ambayo nimeitaja sasa hivi hata ng’ombe anapita kwa tabu. Nimwombe Mheshimiwa Profesa Mbarawa, niko chini ya miguu yake, naomba barabara hii wakati wa ku-wind up basi aipandishe hadhi kwani naamini kabisa hata wananchi wangu wanashindwa kwenda hospitali, akinamama wanajifungulia njiani maana hata gari halipiti wanawabeba kwenye machela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mbogamboga, viazi, matunda, ina maana hayafiki kwa wakati, wakati barabara ile ni barabara ya mkakati, barabara ya kiuchumi. Nilishaongea siku nyingi sana, namwomba Mheshimiwa Profesa Mbarawa asije aukawa masuula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, kuna barabara ambayo inaanza Dochi kwenda Nguli mpaka Mombo, kilometa 16... (Makofi)

T A A R I F A . . .

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa yake siipokei, kwani hajui analolifanya na tabia zake zinajulikana kabisa hapa Bungeni na Tanzania nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kutoka Dochi kupitia Ngulwi hadi Mombo, kilometa 16.1 barabara hii Mheshimiwa Naibu Waziri alikuja, Mheshimiwa Kwandikwa, akashuhudia barabara ile na akaongea na wananchi. Barabara ile ni barabara ya kihistoria, barabara ile ilitumika tangu mkoloni mpaka sasa hivi kuna sehemu inaitwa Kalimasumni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kalimasumni ina maana mababu zetu walikuwa wanabebeshwa mizigo na wazungu kutoka Bondeni Mombo mpaka hapo Kalimasumni sehemu wanaita Ngulwi kwa hiyo, analipwa senti 50 ndio maana panaitwa Kalimasumni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sasa Serikali yangu Tukufu, Mheshimiwa Profesa Mbarawa na timu yake, naomba barabara ile itengenezwe kwa sababu barabara ile ni barabara mbadala. Nimeshaiongelea sana barabara ile kila wakati nachangia. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Profesa Mbarawa sasa, barabara hii naomba kabisa aiweke kwenye mkakati wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitengenezewa barabara mwaka 1984 na JBG. JBG baada ya kutengeneza barabara kutoka Mombo mpaka Lushoto kilometa 32, walikabidhi majengo yale kwa halmashauri ya Lushoto, lakini RRM wakayachukua majengo yale mpaka sasa hivi majengo yale ni ya TBA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimwombe Waziri Mheshimiwa Profesa Mbarawa, nimwombe Waziri wangu, chonde-chonde, naomba majengo yale sasa yarudishwe halmashauri, ili tuweze kufungua Chuo cha VETA pale kwa sababu, majengo yale tayari yana karakana, yana garage na chuo cha seremala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwombe Waziri wangu Mheshimiwa Profesa Mbarawa atakapohitimisha hoja yake basi, nimwombe karakana ile iweze kurudi halmashauri yetu tuweze kufungua Chuo cha VETA, Lushoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara za TARURA. Inasikitisha sana, inasikitisha mno unapozungumzia barabara za vijijini ni nyingi mno kiasi kwamba, TARURA hata haiwezi. Hebu angalia barabara ambayo nimemwambia, hiyo barabara ya kutoka Dochi – Ngulwi mpaka Mombo, barabara ile tangu mafuriko ya mwezi wa Nne mwaka 1917 haijawahi kupitika, matokeo yake TARURA naona wamepanga eti ukarabati sehemu korofi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mheshimiwa Profesa Mbarawa, barabara haipitiki halafu inapangiwa pesa eti sehemu korofi, hivi inakuwaje? Basi nimwombe barabara hizi nazo ziweze kupatiwa fedha ziweze kutengenezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kitandula alisimama akasema kwamba, kuna Kampuni ya Kichina inawekeza kiwanda kikubwa sana ambacho kinatumia trilioni saba, lakini kuna baadhi ya watu au mtu ambaye amekwamisha Wachina wale wasijenge gati maeneo yale ya Mkinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini Mheshimiwa Profesa Mbarawa mtu huyu anamfahamu, kama sio mmoja basi ni wengi anawafahamu. Nimwombe atakapo-wind up basi mtu huyo ampigie simu awaachie, atoe kibali, ili wananchi wa Mkinga au Mchina yule aweze kujenga gati pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.