Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa sababu nina dakika tano, nami ni mwanamuziki bora kabisa wa hip hop nitakwenda kwa style ya rap kidogo, yaani mbio. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikazie alipoishia mwenzangu Mheshimiwa Devotha Minja. Ni masikitiko makubwa sana kwa Waheshimiwa Wabunge wa Mkoa wa Morogoro na wadau wote wa maendeleo Mkoa wa Morogoro kwa kitendo cha Mkoa wa Morogoro kushindwa kukaa katika Bodi ya Barabara na kushindwa kukaa katika Kamati ya Mashauriano ya Mkoa, ni aibu kubwa sana kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikwambie, tumekuja hapa Dodoma ndiyo tunaletewa makabrasha makubwa yaani kama hivi ili tuanze kuyasoma wakati hatujapitisha na hatujui bajeti ya Mkoa wa Morogoro imepitishwa na nani? Mnaweza mkapata picha, Waheshimiwa Wabunge mnajua umuhimu wa Road Board na mnajua umuhimu wa RCC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisogeza hilo kwa Mheshimiwa Waziri ili aweze kuangalia jinsi atakavyotusaidia kama inawezekana kweli wanasema wanaweza kutumbuana, wajaribu kuangalia hili jambo watali-handle vipi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema nitakwenda haraka kidogo. Jambo la kwanza ninalotaka nianze nalo, kilio cha wana Kilosa na Mikumi ni barabara ya kutoka Dumila kwenda Kilosa kuishia Mikumi. Hii barabara ni muhimu sana na mpaka sasa imejengwa kwa kilometa 45 tu. Nimeona kwenye kabrasha la Wizara hapa, wanasema wametenga shilingi bilioni sita na zenyewe ni kwa sababu ya kulipa madeni ya mwanzo huko ya watu wengine. Hatujui kimetengwa kiasi gani cha kukamilisha kilometa 24 za kutoka pale Ludewa mpaka Kilosa, lakini pia kilomita 78 za kutoka Kilosa mpaka Mikumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni barabara ni ya msingi, inakwenda kuunganisha watu wa kaskazini wanaopita Korogwe wanaokuja kutokea Turiani wanakuja Dumila, wanatokea Kilosa – Mikumi wanakwenda kwa Mheshimiwa Lijualikali kule Kilombero, wanakuja kutokea Mlimba lakini wanaenda kuingia Njombe pamoja na Songea. Unaweza ukaona jinsi ambavyo barabara hii ni ya muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tumeomba pia kupandishwa hadhi kwa barabara yetu inayotoka pale Ruaha Mbuyuni, inaenda Malolo – Uleling’ombe inakuja kutokea Kibakwe kwa kaka yangu Simbachawene, lakini mpaka leo hatujapata majibu hii barabara itakuwaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu Daraja la Ruhembe. Nilishaongea mara nyingi hapa, hili daraja ni la muhimu, ndugu zetu wanakufa mara kadhaa. Mheshimiwa Waziri alisimama na kuniambia kwamba wametenga shilingi milioni 700, sizioni sehemu yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walituambia watatupa daraja la muda pale kutoka Kiberege, limeshakuja, machuma yamewekwa chini, ndugu zangu wa kule Ruhembe bado wanaendelea kufa, watu na mama zetu wanataabika sana. Naomba sana Mheshimiwa Waziri, akija atuambie mpango gani wanao kuhusu Daraja ya Ruhembe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu uchukuzi. Jimbo la Mikumi mnajua ni la utalii lakini sasa hivi ukimaliza tu pale kwenye vibao vya kuingia Mikumi, upande wa kulia wote Railway wamepiga X, maana yake nyumba zote na vitega uchumi vyote na mahekalu yote yaliyojengwa kule inabidi yabomolewe. Wananchi wa Mikumi wanaishi kwenye taharuki kubwa sana. Hii siyo Mikumi peke yake, bali Kata ya Kidodi na Kata ya Ruaha ambayo ni Kata mama katika Jimbo la Mikumi, nao wanaishi katika sintofahamu hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilijaribu kuwasiliana na viongozi wa Railway wakatuambia kwamba wanajua kwamba pale Mikumi kulikuwa na reli inatoka Kilosa kuja pale kwenye kiwanda cha sukari, lakini hiyo reli yenyewe mpaka leo mataruma yameshang’olewa. Hakuna dalili ya reli yoyote, wanawafanya wananchi wa Mikumi wanaishi kwa wasiwasi, wanashindwa kuendeleza biashara zao, watalii wanashindwa kuwekeza kwa sababu ya kuwa na alama za X na tunaambiwa tutabomolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Mheshimiwa Waziri wawaambie watu wa TRL waje kukaa na watu wa Mikumi kwa sababu watu wamepewa hati na wamejenga pale wamewekeza kwa ajili ya utalii, lakini wanakuwa katika hali ya sintofahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu suala la TARURA. Tunajua umuhimu wa TARURA. Mama yangu Mheshimiwa Kiwanga hapa amegusia kuhusu barabara ya pale Kilosa Mjini, shilingi milioni 600 imepigwa, lami imewekwa pale miezi sita haijafika inatimka vumbi, lakini bado hakuna kinachoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA Kilosa bado wana hali ngumu sana, fedha zinazokwenda ni ndogo lakini pia hawana usafiri. Wilaya ya Kilosa ni Wilaya kubwa sana, lakini pia jiografia yake ni mbaya sana. Tujaribu kuangalia jinsi ya kuwawezesha hawa TARURA ili waweze kufanya kazi nyingine za kutosha kusaidia wananchi wa Mikumi, maana kuna barabara zime… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.