Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia fursa hii ya awali ili na mimi niweze kuchangia katika hoja hii muhimu ya Wizara ya Ujenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni wazi kwamba Wizara hii ukiangalia kwenye fedha za maendeleo ndiyo Wizara ambayo inapata fedha nyingi kuliko Wizara zote. Kwa sababu katika shilingi trilioni 12 za maendeleo Wizara hii ambayo najua ni Wizara kama tatu zina takribani shilingi trilioni 4.1 sawa na asilimia 33. Pamoja na kupata fedha nyingi kiasi hiki tunaona ni jinsi gani barabara zetu zinavyojengwa chini ya viwango na fedha zinaibiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nitajikita zaidi kwenye suala ambalo lililetwa na Mheshimiwa Kiwanga akisema kwamba Mkoa wa Morogoro hawakuwa na Road Board wala RCC na Mheshimiwa Zitto alitaka kusimama kuomba Mwongozo, lakini haikuwezekana. Huu ni mwendelezo wa jinsi gani Serikali inayosema ni Serikali ya wanyonge lakini kama kilometa nne zinaweza kujengwa kwa shilingi bilioni 13 wakati katika hali ya kawaida kilometa moja ni kuanzia shilingi milioni 700 mpaka shilingi bilioni moja leo tunazungumzia shilingi bilioni 13 na zaidi kwa kilometa nne, hii inamaanisha kwamba kilometa moja imejengwa kwa zaidi ya shilingi bilioni tatu. Jambo hili tunaliona ni wizi mkubwa na najua Mheshimiwa Magufuli amekuwa akisema anapambana na rushwa.

Sasa tunaitaka Serikali na Waziri atakapokuja kutoa majumuisho jioni atuambie fedha hizi zimekwenda wapi na wahusika wamechukuliwa hatua gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ni upanuzi wa barabara ya Morogoro. Haya masuala ya ubaguzi yakiendelea katika nchi hii tunaenda pabaya. Haiwezekani katika eneo moja la barabara, mimi ninavyojua barabara inapaswa iwe imenyooka na iwe na upana wa kufanana. Barabara ya Morogoro inapoanzia kule bandarini upana wake ni kama mita 35 mpaka 40; lakini inapofika Ubungo hasa maeneo ya Kimara barabara ile upana kwa pande zote mbili ni mita 121. Kwa hiyo, naomba kufahamu hivi barabara siku hizi inakuwa sawa na chatu aliyemeza mtu au barabara inapaswa iwe imenyooka? Tunaomba maelezo najua Mheshimiwa Naibu Spika na wewe unakaa kule na umeona ni jinsi gani watu wamebomolewa halafu zinapokuja kauli kwamba hawa wabomelewe au hawa wasibomelewe kwa sababu wamenipa kura, haya mambo hatuwezi kuyakubali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nije kwenye suala zima la hapa Dodoma. Inajulikana kwamba Wabunge wengi, Mawaziri pamoja na wewe mwenyewe tunakaa maeneo ya Area D. Ilikuwa kuja Bungeni tunatumia takribani dakika tatu au nne, ilikuwa ni kama kilometa moja na nusu lakini sasa hivi tunakwenda mwendo wa kilometa sita na tunazunguka kwenye maeneo hatarishi sana. Wengine ukifika kwenye ile shule na tunashukuru Mungu kwamba kuna ile shule pale ambayo tunaweza kupita kwenye miti mvua zikinyesha tunahamia pengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi najua kuna teknolojia ya kila aina, hivi ni kwa nini Mheshimiwa Waziri na niliongea naye wasichimbe barabara ya chini hapa airport ili magari yaweze kupita chini? Najua Mheshimiwa Waziri umetembea nchi nyingi haya tunayajua. Jana kuna mmoja alisema kwamba magari ya Wabunge yawe yanapita, lakini tujue kuna emergency landing ya ndege jambo ambalo ni hatarishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani hapo ni nusu kilometa tu kujenga barabara ya chini ili magari yaweze kupita na hasa ukizingatia kwamba hata yale maeneo pale biashara zimekufa kabisa. Kwa hiyo, naomba sana jambo hilo lifanyike kwa sababu tunaona barabara nyingine ya kwenda kwa Waziri Mkuu kule inajengwa tulidhani hii ya hapa ambayo inapitisha watu wengi ingekuwa rahisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la nyumba za TBA, nimesoma kwenye kitabu hiki, mimi nimekaa kwenye nyumba ya TBA huu ni mwaka wangu wa 11, haijawahi kukarabatiwa wala kufanywa chochote hasa ukizingatia miundombinu ya maji ni ile ya zamani sana na kwa maana hiyo tunahitaji wabadilishe miundombinu hiyo ili iwe ya plastiki. Mimi nashangaa kama wameshindwa kuzi-maintain hizi nyumba ni bora wawauzie Wabunge au watu wanaozihitaji waweze kuzi-maintain. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashangaa kwamba TBA wanapewa vibali vya kujenga nyumba mbalimbali including zile hosteli za Magufuli ambazo zimekuwa na expansion joint ni kwamba hawana uwezo, lakini huku wanaendelea kupewa matumizi makubwa ya kwenda kujenga nyumba mbalimbali. Kwa hiyo, mimi niseme kwa kweli haya mambo haya tukiendelea kunyamaza kama wenyewe wanashindwa ku-maintain za kwao wanawezaje kwenda kujenga na huko kwenye kujenga tayari wameharibu. Kwa hiyo, nadhani TBA kuna tatizo kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie barabara ya kutoka Bahama Mama kwenda Chuo Kikuu. Barabara ile kwa kweli imesaidia sana lakini bado haijakamilika. Kwa hiyo, tunaomba kujua hii barabara ya Goba - Makongo mpaka Chuo cha Ardhi inaisha lini? Vilevile ile ya Msewe ambayo kwa kiasi kikubwa imeharibu sana mazingira ya Chuo Kikuu. Barabara za chuo kikuu zimekufa kabisa kwani zimekuwa na mashimo makubwa, tunaomba sana mmalize ili watu waweze kupita kwa urahisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.