Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nianze kwa kuwapongeza viongozi wa Wizara hii, ndugu yangu Profesa na wasaidizi wake Mheshimiwa Kwandikwa na Mheshimiwa Nditiye kwa namna ambavyo mnatekeleza majukumu yenu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na suala zima la TARURA. Tumeanza na TARURA inafanya kazi lakini bado ina changamoto na kule kwetu Kilwa TARURA hawana vifaa vya usafiri, hawana gari kwa hiyo utendaji wao wa kazi unakuwa ni shida. Kwa hiyo, niombe Wizara iwaone hawa ili waweze kufanya kazi yao vizuri zao sawasawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna hoja ya upembuzi yakinifu katika barabara ya Nangurukuru - Liwale. Imeelezwa katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwamba barabara hii itafanyiwa upembuzi yakinifu lakini mpaka sasa hakuna chochote kimefanyika. Niiombe Wizara ituangalie watu wa Kilwa, Liwale kufanya upembuzi yakinifu tayari kwa kuijenga barabara ile kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala zima la barabara zinazounganisha mikoa hasa barabara inayounganisha Mkoa wa Lindi na Mkoa wa Morogoro. Mheshimiwa Waziri naomba aliangalie hilo, sisi watu wa Lindi tuna haja ya kuunganishwa na wenzetu wa Morogoro ili tuweze kuwasiliana kijamii na kiuchumi ili mambo yetu yaweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna barabara ya Kipatimu - Njia Nne ambayo iko chini ya TANROADS inahudumiwa na hata sasa hivi wakandarasi wako site lakini tuna changamoto kubwa ya miinuko na milima. Kwa hiyo, tuombe Wizara katika milima mikali watuwekee hata vipande vya lami ili ile barabara iweze kupitika wakati wote. Kwa mfano, kuna Mlima wa Ndundu ni mkali sana, Mlima wa Ngoge na Mlima Kinywanyu Wizara ituangalie hivyo vipande viweze kuwekewa lami ili barabara hiyo ipitike wakati wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee sasa suala la mawasiliano ya simu. Katika Jimbo langu kuna Kata ya Chumo, mawasiliano ya simu yapo lakini mnara wa Vodacom uliofungwa pale una matatizo. Unafanya kazi kwa muda wa saa saba hadi nane tu kwa siku, wananchi wangu wanapata hasara kubwa. Ukianza saa tatu mwisho saa mbili usiku baada ya hapo mnara ule haufanyi kazi tena na ni kwa sababu ya chanzo cha umeme pale, wanatumia solar power ambayo nafikiri ina matatizo. Nimeshafikisha tatizo hilo Wizarani naomba mlishughulikie kwa sababu mawasiliano pale ni kama yapo nusu nusu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo kuna Kata ya Kandawale hawana mawasiliano kabisa, kuna Vijiji vya Mkarango, Dandete, Kinjumbi hivi vyote havina mawasiliano ya simu. Naomba basi ndugu yangu Mheshimiwa Nditiye utuangalie na sisi tuweze kupata mawasiliano hayo ya simu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda niongelee suala la mgawanyo wa bajeti ya barabara kwa mikoa. Nimejaribu kufuatilia bajeti za kila mwaka za mikoa inaonekana mgawanyo ni kama haulingani, kuna mikoa ambayo bajeti inakuwa kubwa sana na mingine kila mwaka bajeti inakuwa hafifu sana. Angalau mngejitahidi tuwe tunalinganalingana kwa sababu mikoa mingine kila mwaka bajeti iko juu sana lakini mikoa mingine kama Lindi kila mwaka bajeti iko chini sana. Mheshimiwa Profesa angaliaangalia, hatuwezi kufanana kwa asilimia lakini angalau tulinganelingane kwa sababu hatuelewi mnatumia vigezo gani ya kwamba mikoa mingine bajeti juu na mikoa mingine bajeti inakuwa chini sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna suala la mawasiliano ya redio. Katika bajeti ya mwaka 2016/2017 walisema wangejenga mnara pale Nangurukuru ili na sisi watu wa Kilwa tupate mawasiliano ya Redio Tanzania, lakini mpaka sasa hakuna chochote ambacho kimefanyika. Tunakosa mawasiliano ya redio hasa redio yetu ya Taifa, Redio Tanzania. Tunaomba sasa mnara ule ujengwe, wananchi wanashindwa kuelewa nini kinachoendelea hasa kupitia mawasiliano ya redio. Ni muhimu sana mnara ule ukajengwa ili wananchi wapate mawasiliano ya redio. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la upanuzi wa Bandari ya Kilwa Masoko. Kama ambavyo mnafahamu tunayo bandari yetu pale, lakini mpaka sasa hivi bado haijaonwa. Wizara iione Bandari ya Kilwa Masoko iifanyie upanuzi. Bandari ile ni kama imesahaulika, mtukumbuke na sisi watu wa Kilwa, Bandari ya Kilwa Masoko ipanuliwe kwani itatusaidia sana katika sekta ya utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la upanuzi wa Uwanja wa Ndege Kilwa Masoko. Katika miaka miwili, mitatu iliyopita kulikuwa kuna mpango wa upanuzi wa Uwanja wa Ndege Kilwa Masoko na kuna tathmini ilikuja kufanyika pale ili wale wananchi wanaozunguka uwanja ule waweze kupata fidia lakini mpaka sasa hivi hakuna kinachoendelea, wananchi wale wamebaki pale hakuna uendelezaji wowote unaofanyika na hakuna dalili kwamba ni lini wananchi wale watafidiwa. Kwa hiyo, niiombe Serikali na Wizara iwaangalie wananchi wa Kilwa Masoko ili basi na wao waweze kupata stahiki zao, wafanye mambo mengine kwa ajili ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho na mimi niungane na Wabunge wengine ambao wamejaribu kuelezea shida Waheshimiwa Wabunge wanayoipata ya kusafiri kutoka hapa tulipo kuelekea Area D. Mimi nafikiri Serikali itafute suluhu ya haraka sana kwa sababu haieleweki sehemu ambako Waheshimiwa Wabunge wanakaa namna ya kusafiri inakuwa shida yaani ni kana kwamba Wizara imelala au haioni. Waheshimiwa Wabunge wanapitapita vichochoroni wanaweza wakaibiwa, lakini mazingira yale siyo rafiki. Kwa hiyo, hilo liangaliwe ili Waheshimiwa Wabunge waweze kusafiri comfortable kwenda katika zile nyumba ambazo wanaishi na kufika hapa Bungeni. Ahsante sana.