Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kunipa nafasi hii ya kuchangia. Kwanza niishukuru sana Serikali kwa kazi kubwa ya miradi mingi inayotekelezwa hapa nchini ikiwemo ya barabara, viwanja vya ndege, ununuzi wa meli, ununuzi wa ndege na ununuzi wa rada pamoja na miradi mingi ambayo ipo chini ya Wizara hii. Niwapongeze sana wafanyakazi wa Taasisi zote kwa kazi kubwa wanayoifanya pamoja na Waziri na wasaidizi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa muda ni mfupi nilikuwa naomba nizungumzie maeneo ya msingi ambayo tunahitaji tuishauri Serikali; la kwanza tunahitaji suala la kurudishwa maduhuli ya fedha za taasisi zinazokusanya fedha kwenye maeneo hasa ya Bandari, TAA, TCRA, waweze kuwezeshwa. Maeneo haya ni ya msingi ili tuweze kuyawezesha yaweze kufanya kazi vizuri, tunapokusanya fedha na tukachukua zote zikaenda kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali tunazinyima hizi Taasisi ziweze kushindwa kufanya kazi.

Naomba sana Serikali iangalie umuhimu wa kuwawezesha bandari tunapoiwezesha bandari kuwarudishia fedha ziweze kufanya kazi wanaweza wakatengeneza mazingira ya kukuza bandari zingine nchini kwa maana Bandaria ya Mtwara, bandari ya Tanga na bandari za maziwa makuu kwa maana ya Mwanza na Kigoma. Tunaomba hili mliangalie kwa ukubwa wa aina yake ili muweze kuzisaidia taasisi hizi. Sambamba na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege, sambamba na Mamlaka ya Anga ili waweze kuwezeshwa fedha hizi ziweze kufanya kazi za kuendeleza miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nilikuwa naiomba Serikali iangalie tena ni jitihada ambazo zimefanywa kwa ajili ya kuliwezesha Shirika la MSL. MSL mmetoa fedha nyingi Serikali. Lakini tunaomba sana Serikali muwalipe mishahara wale wafanyakazi bila kuwawezesha au kuwalipa mishahara hamna kitu tutakachokuwa tumekifanya. Serikali inakarabati meli 14 lakini mpaka leo tunavyozungumza wafanyakazi hawajapata fedha na watakao operate hizo meli ni hawa hawa wafanyakazi. Tunaomba muwawezeshe ili waweze kufanya kazi na kulinda miundombinu ambayo tutakuwa tumewekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa muda ni mfupi naomba nijikite kwenye eneo la jimbo langu. Serikali imefanya kazi kubwa eneo la jimbo langu tuna ujenzi wa barabara ya kutoka Mpanda kwenda Kigoma eneo hili halijatengewa fedha nilikuwa naomba Serikali iangalie umuhimu wa kuweka fedha kiasi kwa ajili ya kuendeleza ile barabara. Tunashukuru Serikali imetoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya kutoka Mpanda kwenda Tabora naamni Serikali itafanya kazi kubwa kwa ajili yakuziunganisha hizi barabara, tunaomba eneo hili muliwezeshe na liweze kusimamiwa vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la reli; tunaomba reli ambayo imewekwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ifanyiwe kazi kama ilivyotengewa. Kamati yetu imeshauri Serikali tunaunga mkono jitihada za Serikali na kazi kubwa ambazo wamezifanya. Reli ya kutoka Dar es Salaam - Morogoro, reli ya kutoka Morogoro kwenda Dodoma, reli ya kutoka Makutupora kwenda Tabora na Mwanza tunaunga mkono na tunaomba reli ya kutoka Tabora kwenda Kigoma muiwekee umuhimu wa aina yake sambamba na matawi ya kwake ya kutoka Uvinza kwenda Msongati sambamba na matawi ya kutoka Kaliua - Mpanda - Karema, tunaomba maeneo haya myafanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi la mwisho kwa shirika TRC tunaomba eneo la Mkoa wa Katavi mlipelekee mabehewa ya kutosha kwa sababu barabara ya Mpanda - Tabora imefungwa tunaomba muwasaidie wananchi mpeleke behewa ili ziweze kuwasaidia kupata usafiri huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa muda ni mfupi naunga mkono hoja, ahsante