Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, natanguliza shukrani na pongezi kwa Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi nzuri inayofanyika. Nampongeza Rais, Mheshimiwa John Pombe Magufuli; Makamu wa Rais, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu; Waziri Mkuu na Baraza lote la Mawaziri, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano pamoja na Naibu Mawaziri kwa kazi nzuri na kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, miongoni mwa mambo ninayojivunia anayoyafanya Rais wangu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ni pamoja na kujenga uchumi wa viwanda; kujenga nidhamu ya watumishi; kukemea uzembe; kuendesha vita dhidi ya ufisadi na dawa za kulevya; kufufua Shirika la Ndege Tanzania; kujenga reli ya kisasa (SGR) na barabara; kuongeza vyanzo vya umeme ikiwemo miradi ya gesi ya Stiegler’s Gorge Hydro Elecricity Power na kusambaza umeme hadi vijijini; kujenga bomba la mafuta kutoka Hoima (Uganda) – Tanga (Tanzania); kuimarisha huduma za afya; kutoa elimu ya msingi hadi kidato cha nne bila malipo; kujenga miradi ya maji; kuandaa mifuko ya maendeleo ya vijana, akina mama na walemavu; na kuhamishia makao makuu ya nchi Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee naishukuru Serikali kwa kuipatia Wilaya ya Longido miradi ya maendeleo kama ifuatavyo:-

(i) Mradi wa maji safi na salama kutoka Mto Simba Mlimani Kilimanjaro hadi Longido Mjini wenye jumla ya shilingi bilioni 16;

(ii) Ujenzi wa vituo vitatu vya afya katika Kata za Longido, Engarenaibor na Kimokoukwa/Namanga zinazogharimu zaidi ya shilingi bilioni 1.5;

(iii) Ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ambayo imetengewa fedha za kujengwa katika mwaka huu wa fedha wa 2018/ 2019;

(iv) Umeme wa REA Awamu ya Kwanza na Pili ambayo ulifikia vijiji 19 kati ya vijiji 49 vya Wilaya ya Longido; na

(v) Barabara inayosimamiwa na TANROADS kutoka Sanya Juu hadi juction ya barabara ya Mto wa Mbu Ngaresero yenye zaidi ya kilometa 200.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nijielekeze katika kuiomba Wizara iangalie orodha ya miradi ya maendeleo itakayotekelezwa katika kipindi cha mwaka wa fedha 2018/2019 kama ifuatavyo:-

(i) Ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kutoka Sanya Juu, Wilayani Siha, Mkoa wa Kilimanjaro hadi Mjini Longido, Mkoa wa Arusha (kilometa 64). Barabara hii ilibainishwa kwenye Ilani ya CCM ya 2015-2020;

(ii) Kuendeleza mradi wa REA ili umeme ufike katika vijiji 30 vilivyosalia ndani ya Wilaya ya Longido. Kati ya kata 18 za Wilaya ya Longido ni kata 10 tu ndizo ambazo zimeshafikiwa na umeme wa REA. Kati ya vitongoji 176 za Wilaya ya Longido ni 36 tu ndizo vimefikiwa na umeme.

(iii) Katika Wilaya ya Longido bado tuna vijiji vingi ambavyo bado havina mitandao ya mawasiliano ya simu. Mbaya zaidi baadhi ya vijiji hasa kama Kata nzima ya Matale, Gelai - Wosiwosi na Kamwanga zinalazimika kutafuta mawasiliano ya simu kwa kutumia mitandao ya nchi jirani ya Kenya. Maeneo mahsusi ambayo bado hayana mawasiliano ya simu ni pamoja na Kata ya Matale, Gelai, Meirugoi, eneo la Wosiwosi, Kata ya Lumbwa, Elang’ata Dapash, Noondoto, Engikaret eneo la Kiserian na Kata ya Kamwanga.

(iv) Kutokana na kupanuka kwa eneo la jiografia na la kiutawala hasa kwa kuongezwa vijiji, kata na tarafa mpya Wilayani Longido, kuna vijiji kadhaa ambavyo bado vina changamoto kubwa ya miundombinu ya barabara. Naziomba TARURA na TANROADS zitusaidie kufikisha huduma ya barabara katika vijiji vya Meirugoi – Magadini (kilometa 34); Gelai Lumbwa – Wosiwosi (kilometa 54); Ketumbeine – Elang’ata Dapash (kilometa 18); barabara ya Ketumbeine hadi Iloirienito (kilometa 24); Meirugoi – Nadaare (kilometa 14); Engarenaibor – Matale C (kilometa 15); Namanga – Sinonik na Kimwati (kilometa 40); Sinya – Namanga (kilometa 30) na Engikaret – Kiserian (kilometa 14).

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kuna barabara nyingi za kuunga vijiji na vitongoji vyake zinazoendelea kujengwa kwa nguvu za wananchi Wilayani Longido, naiomba TARURA itenge fedha za kuwaunga mkono wananchi kwa kupitisha greda katika barabara hizo ili zipitike kirahisi. Miongoni mwa barabara zinazojengwa kwa sasa kwa nguvu za wanachi ni pamoja na barabara ya Mundarara – Orpukel – Gelai (kilometa 20); barabara ya Mundarara – Ingokiin – Engarenaibor (kilometa 15); barabara ya Mundarara – Injalai (kilometa 8); barabara ya Mairowa – Ing’ong’wen (kilometa 12); na barabara ya Matale A – Emurutoto – Mesera (kilometa 16).

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho naomba niishauri Serikali kuhusu kuboresha huduma za usafiri wa anga na barabara kuja mji mkuu wa makao makuu ya nchi, Dodoma. Nashauri ATCL waanzishe safari za kutwa asubuhi na jioni kutoka Dar es Salaam – Dodoma; Dodoma – Arusha/ Kilimanjaro; Mwanza – Dodoma na Dodoma – Mbeya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri vilevile barabara za Mji wa Dodoma ziboreshwe, vibao viwekwe na kuwe na parking ya uhakika nje ya eneo la Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.