Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa kazi nzuri. Vilevile pongezi ziwaendee Naibu Mawaziri pamoja na Makatibu Wakuu na watendaji wote wa Wizara kwa utendaji mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri nimefurahi sana kwa maelezo yaliyopo katika ukurasa wa 11, aya ya 23, kipengele cha (iii) kwamba barabara ya Geita – Bulyanhulu Junction - Kahama (Lot 1 anda Lot 2) kuwa usanifu wa kina wa sehemu ya Geita – Bulyanhulu Junction (kilometa 58.3) na Bulyanhulu Junction – Kahama maandalizi ya ujenzi yanaendelea. Kwa kuwa barabara hii ni kiunganishi kikubwa sana na muhimu kiuchumi kati ya Mkoa wa Geita na Mkoa wa Shinyanga, naomba Serikali ianze ujenzi wa barabara hii maana ni ahadi ya muda mrefu sana kwa ajili ya kuimarisha uchumi katika mikoa husika. Vilevile ndiyo barabara muhimu inayotumika kusafirisha bidhaa na malighafi muhimu zinazotumika katika shughuli za uchimbaji wa madini. Ikikamilika barabara hii itasaidia kuinua uchumi utokanao na uchimbaji wa madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande na barabara za mkoa, kwanza nimpongeze sana Meneja wa TANROADS, Mkoa wa Geita kwa kazi nzuri sana inayofanyika ndani ya Mkoa wetu wa Geita. Kwenye bajeti ipo barabara ya Geita – Bukombe ambapo Serikali imepanga kujenga kilometa moja ya lami, mimi nashukuru sana kwa mpango huu. Niombe kwamba baada ya kupitisha bajeti hii utekelezaji wa ujenzi wa barabara hii uanze mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo zipo ahadi za kilometa tano za lami katika Mamlaka ya Mji Mdogo Katoro ambazo ziliahidiwa na Mheshimiwa Rais kwenye mkutano wa kampeni mwaka 2015. Naomba pia ahadi hizi ziangaliwe na utekelezaji ufanyike. Tangu mwaka 2015 hadi leo ni miaka mitatu sasa sijaona utekelezaji wa ahadi hii. Naomba Wizara mlichukulie suala hili na mlifanyie kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru pia kwa mpango wa Serikali uliopo ukurasa wa 162 juu ya upanuzi wa vivuko mbalimbali ikiwemo ujenzi wa maegesho ya Bwina, Bukondo na Zumacheli katika kivuko cha Charo – Nkome. Kwa ujenzi wa maegesho ya Bukondo itarahisisha kwa kiasi kikubwa usafiri kwa wananchi wa Mkoa wa Geita kwani ilikuwa ni kilio kikubwa sana kwa wananchi wa maeneo ya Geita na Chato. Niombe sana ujenzi wa maegesho katika maeneo haya uanze mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa naomba barabara ya Katoro – Busanda – Nyakanga - Nyabulolo – Kamena – Nyamalimbe – Mwingiro ipandishwe hadhi kuwa barabara ya mkoa ili kurahishisha mawasiliano kati ya Wilaya ya Geita na Wilaya ya Nyang’hwale.

Mheshimiwa Naibu Spika, sina la ziada, naunga mkono hoja.