Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Pamoja na juhudi kubwa sana za Serikali ya Awamu ya Tano za kuifanya Tanzania kuwa Taifa la uchumi wa kati kupitia sera ya Tanzania ya viwanda, sekta ya ujenzi, uchukuzi na mawasiliano inao mchango mkubwa katika mwelekeo huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imejipanga kujenga barabara za lami, madaraja makubwa, reli ya kisasa standard gauge, upanuzi wa bandari, ununuzi wa meli mpya katika maziwa yetu makuu pamoja na vivuko, ujenzi wa flyovers Jijini Dar es Salaam na mipango ya kuendeleza ujenzi kama huo Jijini Mwanza na Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza pia Serikali kwa mpango wake wa kuendelea na upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa ajili ya ujenzi wa Daraja la Kigongo – Busisi, hatua hii ni muhimu sana katika kukuza uchumi wa kanda ya ziwa na nchi jirani za Jumuiya ya Afrika Mashariki
na nchi za Afrika ya Kati kwani daraja hili litarahisisha usafirishaji wa watu na mizigo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe tunaipongeza Serikali kupigia TANROADS Mkoa wa Geita chini ya uongozi madhubuti wa Meneja wa TANROADS Mkoa Ndugu Haroun Senkunku na msaidizi wake na watumishi wote wa TANROADS Mkoa wa Geita kwa kazi nzuri ya kupigiwa mfano.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha napenda kuuliza, je, Serikali ina mpango gani wa kutenga fedha kwa ajili ya kuanza upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na hatimaye kuanza kujenga kwa kiwango cha lami kwa barabara za Butengolimasa – Iparamasa – Mbogwe hadi Masambwe, barabara ya Katoro – Lulembela hadi Ushirombo na barabara ya Ushirombo hadi Bwehwa – Mbogwe ili kusaidia kukuza uchumi wa wananchi wa Wilaya yetu ya Mbogwe?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hakika Tanzania mpya ni hakika na siyo nadharia. Naipongeza kwa hakika Serikali kwa wazo la kushirikiana na Serikali ya Rwanda kujenga reli ya standard gauge kutoka Isaka – Kigali – Msongali. Reli hii itakuwa ni kichocheo kikubwa cha ukuaji wa uchumi baina ya nchi zetu mbili za Tanzania na Rwanda, naiombea mafanikio mipango yote ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, ununuzi wa ndege na kulifufua shirika letu la ndege la ATCL kutaweza kuchangia katika kuitangaza nchi yetu kimataifa na kuleta tija katika sekta ya utalii kutokana na Taifa letu kuwa na vivutio vngi vya utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe pia Serikali itupie jicho ujenzi wa uwanja wa ndege wa mjini Geita uliopo eneo la Buhalahala, Geita ili kuiwezesha sekta ya usafiri wa anga kuchangia iwezekanavyo kwa wananchi wa Mkoa wa Geita na wale wa maeneo jirani.

Mheshimiwa Naibu Spika, upanuzi wa uwanja wa ndege wa Mwanza ni hatua chanya katika kurahisisha ushirikiano wa kimataifa na kikanda kwa sekta ya utalii na ukuzaji wa uchumi kwa ujumla wake. Kwa hiyo, naipongeza Serikali kwa kuendelea na hatua kama hizi kwa viwanja vyote vikubwa vya ndege vya KIA, JNIA Dar es Salaam, Songwe na viwanja vingine vya ndege nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe pia Serikali kuendelea na upanuzi wa bandari katika maziwa makuu ya Victoria, Tanganyika na Nyasa na kwa Mkoa wa Geita Bandari za Pores, Nungwe, Nkome, Chato, Nyamirembe na Bukondo. Naunga mkono hoja.