Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja asilimia mia moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri na Makatibu Wakuu kwa kazi nzuri wanazofanya. Natoa shukrani zangu za dhati ya moyo kutokana na miradi mingi ya Serikali iliyotekelezeka katika Mkoa wa Dar es Salaam. Nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kutuzindulia miradi mbalimbali katika Mkoa wetu wa Dar es Salaam, Mungu ambariki sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri ujenzi wa barabara ya mwendokasi Mbagala sasa mradi ule uanze angalau tupate tumaini.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa barabara ya Nzasa – Kilungule - Buza uangaliwe kwa moyo wa huruma kwani ni barabara muhimu ambayo itasaidia kuunganisha Wilaya ya Ilala na Temeke na Jet ambayo kama mtu anatoka Mbagala anaweza kufika mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Temeke Mwisho kwa jina Mbagala Road nayo sasa ijengwe kwa uimara zaidi kwa kuwa imekuwa inabomoka mara kwa mara. TARURA waongezewe nguvu kwa kupewa nyenzo za kufanyia kazi kama greda na vifaa vingine. TANROADS nawapongeza sana kwa kazi nzuri wanazofanya wanajenga barabara nzuri sana kiasi kwamba tunataka barabara zote zichukuliwe na TANROADS, kwa hiyo tusiwapunguzie nguvu bali tuwaongezee nguvu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu uwanja wa ndege, naipongeza sana Serikali kwa kuwezesha ujenzi wa uwanja wa ndege mpya wa Dar es Salaam na kutuletea ndege tatu. Tunashukuru sana ukiangalia tulikotoka na tunakokwenda tumepiga hatua kubwa sana. Ombi langu tuboreshe huduma zetu ziende na wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu TBA kwa kweli kuna haja ya kuboresha au kukarabati nyumba zetu na kama hakuna uwezekano tufanye utaratibu ambao mpangaji akifanya ukarabati kisha akatwe katika rent. Miundombinu ya nyumba, mifumo ya maji safi na maji taka imekufa kabisa na hata mafundi wa TBA hawana vifaa vya kufanyia kazi. Nyumba za TBA ni nzuri na zimejengwa kwa uimara wa aina yake tatizo ni kukosa service. Tunaishi miaka kumi hakuna ukarabati wowote siyo vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu TPA naipongeza Serikali kwa ujenzi wa mageti ndani ya Bandari yetu ya Dar es Salaam, nataka kujua Serikali ina mpango gani na Bandari ya Bweni? Fungu la SSR la kutoka bandari pamoja na kutuletea mashuka katika Hospitali yetu ya Temeke namshukuru na kuwapongeza sana kwa moyo wa huruma.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu naomba TPA waangalie na shule zenye watoto walemavu na wenye mtindio wa ubongo ambazo ni Shule ya Mtoni – Maalum, Shule ya Sinza – Maalum na Uhuru Maalum. Shule hizi zina watoto ambao wana mahitaji; kuna wasioona, walemavu wa viungo na akili. Mamlaka yetu iangalie kundi hilo. Nawatakia kila la kheri TPA naona mizigo ni mingi na meli ni nyingi baharini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja asilimia mia moja.