Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kutoa mchango wangu katika hoja hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli kwa uongozi wake thabiti, makini na uzalendo mkubwa. Pia nichukue nafasi hii kumpongeza Waziri, Naibu Mawaziri, Katibu Mkuu na wataalam na watendaji wa Wizara kwa utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo nianze kwa kutoa mchango wangu na nianze na kuwasemea watu wangu wa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki na hasa kuhusu TRC kupitia RAHCO. Naipongeza Serikali kwa kuanza ujenzi wa reli ya kisasa ya mwendokasi kutoka Dar es Salaam mpaka Morogoro na Morogoro mpaka Makutupora, Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na maendeleo ya ujenzi huu wa reli kuna watu walioathirika kwa kupisha maeneo yao ili kujengwa kwa reli, lakini mpaka sasa watu hawa hawajalipwa fidia zao. Fidia hulipwa ndani ya miezi sita baada ya tathmini na hulipwa kabla ya eneo kuchukuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuchelewa kulipwa fidia hii kumeleta athari kubwa kwa watu wetu kwa sababu wananchi walikuwa wanategemea maeneo hayo kwa shughuli za kiuchumi kama vile kilimo, mifugo na pia ni makazi yao kwa baadhi ya watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wamebomolewa nyumba zao, mashamba yao, huduma za jamii kama zahanati, shule na kadhalika. Kwa mfano, watu wa Ngerengere na Mikese wamebomolewa nyumba zao bila kulipwa fidia na wengine kulipwa fidia ndogo isiyolingana na bei ya soko na hali halisi katika Kijiji cha Mikese Station, zahanati mpya inabomolewa na kutakiwa kulipwa shilingi milioni 70 ambayo ni ndogo kuliko gharama zilizotumika au kuhitajika kujenga upya.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuishauri Serikali kulipa fidia kwa wakati na kiwango kinachostahili ili kuwainua wananchi kiuchumi au kuwalipa kwa kiwango kwa kuzingatia thamani halisi badala ya kuwarudisha nyuma zaidi kiuchumi na kijamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali kuwalipa fidia watu hawa walioathirika.