Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE.JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kupata fursa hii. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri na Watendaji wa Taasisi zote zinazoshughulika na michezo na bila shaka wanajua mimi ni mwanamichezo niliyekubuhu na nashughulika na michezo zaidi ya miaka 40 sasa. Kwa hiyo, najua kila kitu kilichoko ndani ya Wizara hii na ndani ya michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Huduma za Jamii na sehemu kubwa, maoni yetu ni yale ambayo tuliyajadili kule, nami nikiwa mdau pia, maoni yetu tuliyatoa kwenye Kamati na Serikali tuliieleza kila kitu, kwa hiyo, hapa nitakuwa na mchango mdogo tu wa kusisitiza. La kwanza ni juu ya michezo mashuleni. Kwa hulka Watanzania hatuna Academy za michezo nyingi kwa sababu ya gharama za uendeshaji. Sasa vituo vyetu hivi kwa maana ya Shule za Msingi, Sekondari na Vyuo ndiyo Academy zetu zinazoweza kutoa wanamichezo wazuri na hasa kwa kuzingatia historia huko nyuma, UMISETA tulikuwa na wachezaji wazuri waliotutetea vizuri kwenye timu za Taifa na pia UMITASHUTA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa maoni yangu ni kwamba Serikali hebu ijaribu kurejea huko nyuma tulifanyaje kwenye michezo shuleni pamoja na kwamba hapa katikati kuna watu walilewa madaraka wakafuta, nadhani tuwaache tu na mambo yao, lakini turudi nyuma kabla ya kufutwa, nini kilifanyika na nini tulifanikiwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni juu ya ruzuku kwa Vyama vya Michezo. Huko nyuma Serikali ilikuwa na mkono wake kwenye Vyama vya Michezo na tuliona faida zake, lakini sasahivi imebaki tunasifia tu, timu ikifanya vizuri tunasifia lakini kwa sasa naona msaada wa Serikali au mkono wa Serikali uko mbali sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali iweke mkono kwenye Vyama vya Michezo ili iwe na power ya kuwaambia no, hiki wanachokifanya siyo. Kama tunasubiri tu mafanikio, mtu tukafanikiwa huko anakuja hapa Bungeni tunapiga makofi na nini, mkono wa Serikali kama haupo, maana yake ni kwamba hata kuwagusa watu hawa hatutaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Chumi amezungumzia ushiriki wa timu zetu za Taifa, siyo kwa maana ya mpira wa miguu tu peke yake. Juzi tumeona kwenye madola, tunaondoka kwa mbwembwe lakini tunarudi hata haijulikani timu imerudi au haijarudi. Maana yake hatuna
maandizi. Ikifika mahali tunashindwa, turudi kwenye ushauri ule, tuache kwenda kucheza ili tujitengeneze vizuri tukaporejea, turudi na nguvu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni juu ya mapato ya Uwanja wa Taifa na Uwanja wa Uhuru. Kamati imetoa maoni yake, lakini mimi nakuja na kitu kingine kabisa. Mapato ya Uwanja wa Taifa na Uwanja wa Uhuru, Baraza la Michezo linachukua asilimia 15, TFF inaambulia asilimia tano. Nadhani jambo hili siyo sawa. Tutoe asilimia tano ya wenye uwanja, tuwape TFF kwa maana ya kuimarisha Mfuko wa Timu ya Taifa, angalau watakuwa na pesa nyingi za kuweza kuhudumia. Vinginevyo, Timu ya Taifa ni mzigo mkubwa Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe unajua Timu ya Taifa ni mzigo. Tunaweza kufikiri kwamba mapato yapo ni mengi ya kuweza kuhudumia, lakini wakati mwingine hata kucheza mechi za Kimataifa timu inashindwa kwa sababu ya gharama. Kwa hiyo, wazo langu, tuangalie, ukiacha viwanja vingine hatuwezi kuvisemea viwanja vile vinavyomilikiwa na Chama cha Mapinduzi mimi siwezi kuwasemea, lakini nazungumzia viwanja vinavyomilikiwa na Serikali; asilimia tano tuitoe kule ili iende kwenye asilimia za TFF. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, sitaki kutumia dakika nyingi. Nimekuwa nasema hapa toka 2010 tunayo Timu ya Vijana Wanaoishi katika Mazingira Magumu kule Mwanza. Timu hii 2010 ilikwenda kushiriki Kombe la Dunia la Watoto Wanaoishi katika Mazingira Magumu kule South Afrika. Tumetoka kule tukawa washindi wa pili. Mwaka 2014 tumekwenda Brazil, tukawa mabingwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kupata ubingwa, watu wakafurahi, wakaja hapa wakatupokea Bungeni, tukaona raha na ahadi nyingi, mpaka leo hakuna jambo lililotekelezwa. Serikali ijaribu kurudi wapi imejikwaa, kwa nini itoe ahadi ya zawadi hewa? Mpaka leo vijana hawajapewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wiki ijayo tunakwenda Urusi kama mabingwa watetezi wa Kombe la Dunia la Watoto Wanaoishi katika Mazingira Magumu. Nini msaada wa Serikali juu ya timu hii? Wakati mwingine hapa Tanzania hakuna bingwa wa dunia isipokuwa wale watoto, hatuoni fahari?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaambia, tukipata ubingwa kama hamtusaidii ni afadhali msituite Bungeni. Bungeni hapa tutakuja kwa utartaibu mwingine. Habari ya kuahidi hapa kila siku, watoto tunawaahidi wanatoka hapa wanasema tumeahidiwa moja, mbili, tatu, sijui viwanja, sijui maisha bora kule kwenye kambi yetu; kama hamtusaidii, wala msianze kufurahia tutakacholeta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kawaida, maneno yangu huwa hayapasi papasi. Nakushukuru sana.