Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia Wizara hii muhimu. Kwanza nimpongeze Waziri Mwigulu kwa kazi nzuri anayoifanya. Lakini pia nilipongeze na Jeshi la Polisi, wanafanya kazi nzuri. Naamini Taifa hili limetulia kwa sababu ya mchango mkubwa wa Jeshi la Polisi, kwa hiyo, tunawapongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii inaongozwa kwa mujibu wa sheria na mtu yeyote anayetaka kuishi kwenye Taifa letu kwa amani, kwa furaha, lazima afuate sheria za nchi hii, vinginevyo Jeshi letu la Polisi fanyeni kazi kwa mujibu wa sheria, washughulikieni wote ambao wanaenda kinyume na sheria ya nchi hii. Katika hili haijalishi ni kiongozi wa dini, haijalishi ni kiongozi wa kisiasa, hebu washughulikieni, Taifa hili lina amani kwa sababu wanafanya kazi nzuri na hizi kelele zinazopigwa zisije zikawatisha wakaacha kazi nzuri ambayo wamekuwa wakiifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunawaunga mkono na naamini mtu ambaye ametulia kwenye Taifa anafuata sheria, hawezi kusumbuliwa wala kubugudhiwa kwa namna yoyote. Wewe ukiona unasumbuliwa ujue una shida, ukiona wanavamia kwako, mara unalala magereza, mara unalala ndani, ujue una shida, fuata sheria uishi kwa furaha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wengi ambao wanajidai kumtaja Mungu lakini maandiko yanasema katika Tito, kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu. Kama unataka Mheshimiwa Rais afanye kazi vizuri pamoja na wewe mtii kwa sababu huyo ameletwa na Mungu na maandiko yanasema hivi, hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu hata hiyo iliyopo imeamuliwa na Mungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama unataka kuishi kwa imani itii hiyo mamlaka; ujumbe umefika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kulisemea Jeshi letu la Polisi kwa upande wa Kyerwa. Nimwombe sana Mheshimiwa Mwigulu na watendaji wote wa Mambo ya Ndani, kwa kweli Jeshi letu la Polisi Kyerwa wanafanya kazi kwenye mazingira magumu, hawana kituo cha polisi, wanafanya kazi kwenye ofisi ya kata ambayo ofisi yenyewe hali yake ni mbaya. Kwa hiyo, niombe polisi wetu hawa ambao wanafanya kazi kwenye maeneo ya mipakani wapewe vitendea kazi lakini wapewe ofisi ambayo inafanana na hadhi ya polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo ambazo nimewapa polisi, upo upungufu ambao naamini kila binadamu anao upungufu; hivyo tunashauriana, tunarekebishana, tunasonga mbele. Kwa upande wa bodaboda niwaombe sana Jeshi la Polisi; mazingira, namna ambavyo wanaendesha hawa vijana wetu wa bodaboda kwa kweli haipendezi. Kwa upande wetu kule Kyerwa bodaboda wakati mwingine wanakimbizwa mpaka kwenye migomba, wakati mwingine wanapata ajali, kwa hiyo, niwaombe sana polisi hili mliangalie tusije tukaanza kusema mambo mengine makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa Magereza kuna eneo ambalo Magereza walichukua pale Kyerwa na wakawaahidi wananchi kuwapa fidia. Wananchi hawa bado hawajafidiwa na wanasubiri kwa muda mrefu na maeneo yao wamezuiwa wasiyaendeleze. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Mwigulu hili aliangalie na walisimamie ili wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa waweze kupewa fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo niongelee upande wa uandikishaji unaoendelea. Kule kwenye Jimbo langu la Kyerwa wananchi wangu wengi unakuta unapomhoji saa mbili, tatu kwa Kiswahili inakuwa ni shida. Sasa kwenye mahojiano yale unakuta wanapowahoji wananchi mwingine anaposhindwa kujibu maswali mawili matatu kwa Kiswahili wanaanza kusema huyu ni mhamiaji haramu. Kwa hiyo, niombe sana hili waliangalie ili uandikishaji huu uweze kufanyika vizuri na kwa ufanisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nilisemee, Waheshimiwa Wabunge tumekuwa tukipita sana eneo la Mikese na eneo lile kituo cha polisi mara nyingi tunapata ajali, tunakuwa na matatizo mbalimbali. Hebu nimwombe Mheshimiwa Mwigulu, kile kituo cha polisi kipewe vitendea kazi, wana gari moja ambalo haliwasaidii. Kwa hiyo, niombe sana kile kituo Waheshimiwa Wabunge wengi tumekuwa tukipata msaada pale, kwa hiyo na chenyewe wakikumbuke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nikushukuru na niendelee kusema Mheshimiwa Mwigulu asonge mbele, Rais wetu anafanya kazi nzuri, hebu wamuunge mkono na Jeshi letu la Polisi kazi kubwa waliyoifanya Kibiti imedhihirisha Jeshi la Polisi wanafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.