Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. MUSSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya Mambo ya Ndani. Kwanza kabisa nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya, Naibu Waziri na Katibu Mkuu. Vile vile nawapongeza Wakuu wa vyombo vilivyo chini ya Wizara hii. Nampongeza IGP kwa kazi nzuri anayoifanya, Mkuu wa Magereza, Kamishna wa Zimamoto na Kamishna wa Uhamiaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama walivyosema baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hapa upo upungufu katika Majeshi yetu, lakini yako mambo mazuri yanayofanyika katika Majeshi yetu. Ni vizuri kueleza upungufu uliopo ili uweze kurekebishwa, lakini wakati tunaeleza upungufu huo tusisahau wajibu wetu kama viongozi pia kupongeza pale ambapo mazuri yanafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuko humu ndani kushauri na tusijiondoe katika utaratibu huo. Tuna nafasi ya kuendelea kushauri pale ambapo upungufu unatokea. Sasa namna gani tunashauri, ni jambo la msingi sana sisi kama viongozi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi pia ni zao la Polisi. Baba yangu alikuwa Polisi na mama yangu alikuwa Polisi. Najua changamoto za Polisi. Ninapozungumza hapa leo, nazungumza nikijua kabisa shida za Polisi ziko wapi, ndiyo maana nataka leo niwapongeze kwa kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sisi tunaotoka vijijini, Jimbo langu ni la kijijini, Makao Makuu ya Polisi yalipo na maeneo yangu ni takriban kilometa 120, maeneo mengine kilometa 150. Wananchi tunapopata matatizo, kama Polisi hawapo katika maeneo yetu, shida tunazozipata, ndiyo maana tunajua umuhimu wa Polisi katika maeneo yetu. Usipopata Polisi katika maeneo yako huwezi kuona faida na hasara zake Polisi asipokuwepo katika maeneo yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano mmoja. Kata yangu moja ya Loya siku moja majambazi waliingia kwenye Kata yetu moja ya Loya, walivamia wakaiba pesa, wakafanya wanachotaka. Waliomba mpaka kupikiwa ugali, wakala. Tulipiga simu Polisi, walifika baada ya masaa mawili. Maeneo ambayo Polisi wapo, ujambazi au wizi hauwezi kufanyika katika maeneo hayo. Kwa hiyo, umuhimu wa Polisi katika maeneo yetu sisi tunaojua, tunapongeza kazi kubwa wanayofanya pamoja na changamoto zilizokuwepo katika maeneo yao ya utekelezaji wa kazi hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haraka haraka pia napongeza kazi nzuri wanayofanya Askari wetu wa kawaida.

Askari hao wanafanya kazi katika mazingira magumu sana, lakini hawajaacha wajibu wao wa kusimamia ulinzi na usalama katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie baadhi ya changamoto ambazo zipo, nami najielekeza katika Wilaya yangu ya Uyui na Jimbo langu la Igalula. Wilaya yetu ya Uyui Makao Makuu yetu yapo Isikizya, ni Makao Makuu mapya lakini mpaka sasa tuna takriban mwaka mmoja Askari wetu wamehamia pale, hakuna nyumba za kuishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba hakuna nyumba za kuishi Askari wetu, Askari wetu wamekubali kwenda kupanga nyumba mitaani, wanalipa gharama hizo wenyewe. Niombe sasa Wizara hii ya Mambo ya Ndani ione umuhimu wa kutenga fedha kwa ajili ya kujenga nyumba za Askari wetu pale Isikizya Makao Makuu ya Wilaya yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Serikali lazima iangalie sasa wale Askari wanaoishi katika nyumba za kupanga, wanaojilipia fedha kutoka katika mishahara yao, waone namna ya kuwapa posho ya kujikimu, kuweza kulipia makazi yao wanapokaa huko uraiani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema Mheshimiwa Makilagi, wanakaa katika mazingira magumu. Wale ambao sisi wahalifu tunakaa nao mitaani mle, lakini Mwenyezi Mungu anaendelea kuwalinda Askari wetu, tuone umuhimu kwa kweli kabisa wa kutenga fedha kwa ajili ya kujenga nyumba za Askari wetu katika maeneo mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo langu la Igalula kama nilivyosema ni kubwa sana, takriban kilometa 150 toka Makao Makuu ya Isikizya, lakini Wilaya yetu ya Uyui ina upungufu wa magari ya Askari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyoeleza, tukio likitokea Kata moja mpaka Askari waweze kufika, kwanza wana upungufu wa magari, lakini wakitaka kufika huko magari saa nyingine mabovu au hayana mafuta. Naomba Wizara iangalie utoaji wa magari kwa Wilaya ambazo zina changamoto ya umbali. Tukipata magari ya kutosha maana yake hata kama kuna matatizo Askari wetu wanaweza kufika katika maeneo mbalimbali kwa haraka na wananchi wetu wakaweza kupata huduma za kipolisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Wizara iangalie kwa ujumla wake nchi nzima uhitaji wa Vituo vya Polisi katika nchi yetu yote, ije na mpango mahususi wa kujenga Vituo vya Polisi katika maeneo yetu. Tumewahamasisha wananchi wetu na maeneo mengi wamekubali kujenga Vituo vya Polisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, katika Kata yangu ya Loya ambayo iko takriban kilometa 120 toka Makao Makuu ya Isikizya, Halmashauri yetu ilitenga shilingi milioni 200, tumejenga Kituo cha Polisi pale. Wananchi wamechangia takriban shilingi milioni 50, mimi Mbunge wao nimechangia takriban shilingi milioni 10. Mpaka sasa kituo kile kimefikia asilimia zaidi ya 95, kimekwisha, lakini mpaka leo kituo kile hakijafunguliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba waangalie mazingira, kilometa 150 toka Makao Makuu ya Wilaya ambako ndiyo Polisi ipo, mpaka kufika Loya, tuliamua kujenga kwa sababu ya umuhimu wake na sababu za kiusalama kutokana na maeneo yenyewe yaliyokuwa kule. Naomba Kituo hiki cha Polisi kiweze kukamilishwa, kifunguliwe na kiweze kupatiwa nyenzo za usafiri ili kuweza kusaidia usalama katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shida kubwa ya mafuta ya kusaidia magari ya Polisi wetu kufika maeneo mbalimbali. Kama nilivyoeleza ukubwa wa Jimbo langu, saa nyingine Polisi wana magari, wanapigiwa simu kwenda kwenye maeneo mbalimbali kunakuwa na shida kubwa ya mafuta. Mgao wa mafuta uangalie na jiografia ya Majimbo yetu. Jiografia ya maeneo mengine trip moja ya gari kwenda Kata moja mpaka nyingine ni takriban lita 150 mpaka lita 200, lakini mgao wa mafuta kwa mwezi unaweza ukakuta OCD anapewa lita 200 au lita 300. Naomba hili liangaliwe ili tuweze kusaidiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja.