Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Zainab Mndolwa Amir

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ZAINAB M. AMIR: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kunipa afya njema ili na mimi niweze kuchangia machache katika Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Pili napenda kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia na tatu, napenda kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake pamoja na Naibu wake na pongezi nyingi ziende kwa Kamati ambayo imetoa maoni, naomba Serikali izingatie maoni hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuja na mpango wa elimu bure, lakini haikuwa na maandalizi ya kutosha. Wazazi na Taifa likahamasika kupeleka wanafunzi mashuleni, lakini katika shule zile madarasa na madawati ni machache. Serikali ikajitahidi kufanya harambee kwa taasisi mbalimbali pamoja na wadau kuleta madawati, lakini ilikuwa haifikirii kwamba yale madawati yanaenda kuwekwa wapi. Matokeo yake wanafunzi wakawa wengi kuliko madarasa yaliyopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utakuta darasa moja kuna wanafunzi 100 mpaka 120 na natolea mfano hivi karibuni nilienda katika shule ya msingi Ungindoni iliyopo Kata ya Mjimwema, Wilaya ya Kigamboni, wanafunzi wanakaa zaidi ya 120 kiasi kwamba mwalimu anashindwa kumsaidia yule ambaye ni slow learner ili aweze kufaulu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatakiwa ijipange, isilaumu walimu kwamba hawafundishi ndiyo maana watoto wanafeli. Kuwaadhibu walimu kwa kufeli kwa watoto wetu kwa kweli wanawaonea. Kama Serikali ingekuwa ina-provide incentives zote kwa walimu, mishahara mizuri, mazingira mazuri ya kufundishia, nyumba bora na mishahara ya walimu inatakiwa iongezwe kwa kiwango cha juu ili walimu waweze kuvutiwa na fani hii. Tunaona tuna ukosefu mkubwa wa walimu kutokana na wengi hawapendi kujifunza fani hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke sote sisi tumepita kwa walimu, madaktari wamepita kwa walimu, wanasheria wamepita kwa walimu lakini walimu wamefanywa kuwa madaraja kwa taaluma nyingine, hatuwajali. Mheshimiwa Ndalichako mama yangu nakuomba sana, wewe umepitia kwa walimu mpaka umekuwa Profesa, wasaidie walimu hawa katika kuboresha maslahi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, madai yao sasa hivi imekuwa kama ni wimbo wa Taifa maana yanaandikwa kwenye vitabu hayatekelezwi. Mimi naona sasa imekuwa mgomo baridi kwa wao kutojituma ili kuleta ufaulu wa hali ya juu. Shule za private zinafaulisha kwa sababu utakuta mwalimu anatoka Serikalini anakwenda kufundisha private kwa sababu ya incentive anazopata, mshahara na mazingira mazuri, kwa nini Serikali haioni haja basi na sisi kuboresha mazingira ya walimu wetu katika shule hizi za Serikali? Kwa nini sisi ambao tumepitia kwa walimu tunadharau walimu wetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nakuomba sana, nakuomba mama yangu umepitia kwa mwalimu mpaka umefikia hatua hii na angalia yule mwalimu uliyemuacha kule kijijini ulikosoma hali yake ilivyo. Nakuomba tuwaboreshee maslahi yao ili walimu hawa waweze kufanya kazi zao sawasawa ili kusaidia wanafunzi wetu kuweza kufaulu kwa kiwango cha juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitembelea shule ya msingi Yombo Dovya iliyopo Kata ya Makangarawe, Wilaya ya Temeke, shule ile kwa kweli ni mtihani. Ina wanafunzi walemavu na wa kawaida, madarasa hayatoshi. Nimejitolea pale tani moja ya mifuko ya saruji na mabati 20 lakini pia hayakidhi mahitaji. Vyoo ni vichache, walimu wanangojea wanafunzi wakajiasaidie na wao waingie katika vyoo vilevile, ofisi za walimu hawana meza za kutosha, wanatumia madawati kama meza zao, huwezi kujua kama hili ni darasa au ni ofisi ya walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tuwajali walimu wetu, hii ndio source ya kushuka kwa elimu yetu. Tusiwaadhibu walimu wala shule zile kuzifungia, sisi Serikali ndio wenye matatizo. Serikali inatakiwa ku-provide kila kitu ili walimu waweze kufanya kazi kwa bidii na kujituma.
Nadhani tukifanya kila kitu wanafunzi wetu watafaulu kwa kiwango cha juu na hatuwezi kumtafuta mchawi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwafukuza walimu kwamba hawajafaulisha tunawaonea. Kuwasimamisha au kufungia shule kama alivyosema Mheshimiwa Profesa Jumanne Maghembe mimi siafiki, kwa sababu mwalimu hawezi kujenga darasa wala maabara, kwa nini unamuadhibu kwamba kasababisha wanafunzi wafeli. Inayotakiwa iadhibiwe ni Serikali ambayo haijaweka mazingira rafiki ya kufundishia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana pindi tutakapopitisha bajeti yako Mheshimiwa Waziri uwajali sana walimu ndio kila kitu, bila walimu sisi tusingefika hapa, bila walimu wewe Mheshimiwa Waziri usingekuwa Profesa.

Kwa hiyo, haya ya kujenga maabara, ukanunue vitabu bila kumwezesha mwalimu huwezi kumlazimisha ng’ombe kunywa maji kama hataki kunywa maji. Utamwekea mazingira, lakini kama mshahara yake hujamboreshea, hujamwekea nyumba bora zenye umeme, anafanya andalio la somo na azimio la kazi kwenye giza hawezi kufanya kazi vizuri. Ndiyo maana wengi hawataki kukaa vijijini wanakimbilia mjini angalau kufanya biashara huku wanafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nakuomba sana Mheshimiwa Waziri utakapokuja hapa tueleze una msimamo gani kwa walimu wetu wa Tanzania kuwaboreshea maslahi yao ambayo yataleta ufaulu wa juu kwa shule zetu. Kwa sababu ukisema uwafukuze walimu unawaonea, ufungie shule zile pia unazionea kwa sababu hawana uwezo. Hata wewe mshahara wako huwezi ukasema ukajenge maabara. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ishauri Serikali na Rais walimu ndiyo kila kitu katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, ahsanteni sana.