Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri na timu yake kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya ya kusimamia masuala mbalimbali ya maendeleo yenye kuleta tija na kuboresha suala zima la elimu. Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa kuwasilisha taarifa yake ya mapato na matumizi katika kipindi hiki cha 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze sana Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa kuwasilisha taarifa yao nzuri, taarifa ambayo imetoa maelezo mbalimbali ya kuishauri Serikali lakini wameona changamoto mbalimbali zilizojitokeza katika kipindi hiki ambacho tunamaliza cha 2017/2018. Kwa hiyo, imeturahisishia sana kwa sababu kila Mbunge aliyesimama amezungumzia mambo ambayo tayari Kamati wameshayaona, imekuwa ni rahisi kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpetia taarifa hii ya Waziri, nimeona namna ambavyo Serikali imepiga hatua kwa namna mbalimbali kwa lengo la kutaka kuleta tija katika suala zima la kuleta mabadiliko makubwa sana upande huu wa elimu, lakini kuwafanya vijana wetu waingie katika mfumo huu wa sekta ya viwanda. Katika kipindi hiki cha bajeti tunayoimaliza, Wizara ilijitahidi sana katika kuboresha vyuo vikongwe na mimi kama Mbunge wa Mkoa wa Lindi nilizungumzia sana Chuo cha Ualimu Nachingwea (TTC Nachingwea) kwa sababu chuo kile ni kikongwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru Mheshimiwa Waziri wa Elimu alisikia kilio chetu na napenda kutumia nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Elimu, dada yangu Mheshimiwa Profesa Joyce Ndalichako, kwa kweli amesikiliza kilio chetu na kwa bahati njema aliweza kututengea fedha, ametupatia shilingi bilioni mbili kwa ajili ya ukarabati wa Chuo cha Ualimu Nachingwea.

Kwa hiyo, hizo ni jitihada kubwa sana ambazo Serikali yetu inazifanya za kutaka kukiimarisha Chuo cha Ualimu cha Nachingwea ili kiendelee kuleta tija na kuzalisha walimu kwa sababu bado changamoto kubwa ya walimu tunayo katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyeki, lakini nimeona ambavyo Serikali inaweza kuboresha elimu kwa upande sekondari. Labda nizungumzie katika Mkoa wangu wa Lindi ambapo tuna Shule ya Lindi Sekondari, shule hii ni kongwe, ilijengwa na wakoloni toka mwaka 1959 lakini ilikabidhiwa Serikalini mwaka 1963.

T A A R I F A. . .

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyeki, namwomba Mheshimiwa Mwambe asinipotezee muda wangu na hiyo taarifa yake ni ya kwake mwenyewe, sina time nayo kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwamba Shule ya Lindi Sekondari ni kongwe na naiomba Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi ili shule hii iingizwe katika mpango wa ukarabati wa shule kongwe kwa sababu ni shule ya muda mrefu, tumeirithi kutoka mikononi mwa wakoloni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mwaka 2016 shule hi imepata ajali ya moto kutokana na hitalafu ya umeme na imeathirika vibaya mno. Katika madarasa 28, 18 yameathirika vibaya sana lakini bado kuna matundu ya vyoo 24 nayo yameathika na shule hii ina wanafunzi zaidi ya 900. Kwa hiyo, kwanza nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo ameungana na wananchi wa Mkoa wa Lindi katika kufanya harambee na kuhakikisha shule hii inajengwa. Pamoja na jitihada hizo kubwa tulizozifanya bado tuko nyuma kabisa katika kufanikisha ujenzi wa shule hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba sana Serikali kwa sababu shule hii ina four one, form four, form five na form six na watoto wanaosoma form five na form six ni watoto wa Tanzania nzima na si watoto wa Lindi peke yake na hii shule ni ya Serikali. Kwa hiyo, naomba kabisa Serikali kutia mkono wake kuhakisha wanatuunga mkono ili shule hii iweze kujengwa na watoto warudi katika mazingira safi na salama ili waweze kupata elimu bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana Mawaziri ambao wametembelea mkoani kwetu Lindi na kila Waziri aliyepita alikuja kutoa pole katika eneo la shule ile. Lakini cha kusikitisha, wageni hao wote waliokuja wametoa pole ya mdomo tu na kutuahidi kwamba tutasimamia suala hili na shule itajengwa. Kwa kweli mimi nasikitika sana imekuwa kama ni sehemu ya utalii wageni kuja kutembelea pale, lakini bado katika ujenzi wameendelea kutuachia wananchi wa Lindi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Serikali iweze kusimamia na kuweza kutuunga mkono katika kuhakikisha shule hii inajengwa kwa sababu ilikuwa ni shule tu ya kawaida lakini sasa hivi baada ya kuungua moto viongozi walishauri kwamba tujenge shule ya jengo la ghorofa. Mahitaji ya ghorofa ni shilingi 2,200,000,000; lakini pamoja na kuwa tumefanya harambee tumepata shilingi 700,000,000 tu. Sasa shilingi 700,000,000 kujenga jengo la shilingi 2,200,000,000 kwa kutumia harambee tutafika miaka 15 jengo lile halijakwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba kwa dhati kabisa Serikali yangu itutazame kwa jicho la huruma, itusaidie kutuunga mkono kuhakikisha Shule ya Lindi Sekondari inajengwa ili watoto wapate mahali pazuri pa kukaa na kupata masomo. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali na natumaini kabisa Mheshimiwa Profesa Ndalichako atasikiliza kilio chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa elimu katika Mkoa wetu wa Lindi tunafanya vibaya sana. Katika shule ambayo inakuwa ya mwisho Mkoa wa Lindi tunaongoza, tunaweza kuwa wa pili mwishoni, wa kwanza mwishoni lakini kuna mambo mbalimbali yanachangia elimu kushuka katika Mkoa wa Lindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wa Lindi tuna shule za sekondari za Serikali 113 lakini asilimia 60 ya shule hizi hazina walimu wa hesabu wala masomo ya sayansi. Sasa ukitulinganisha sisi na shule zingine ambazo zimekamilika, zina maabara za kutosha na vifaa vya kutosha, zina walimu wa hesabu na sayansi, hivi kweli sisi tutakuwa wa kwanza au wa pili au hata kumi bora tutaingia, hata 20 hatuwezi, hata tukaishi kwa miaka 100 kwa style hii hatuwezi kufika.

Kwa hiyo, bado tunaendelea kuleta kilio chetu kwa Serikali kuhakikisha mnatupatia walimu wa hesabu na sayansi ili watoto wetu wa Mikoa hii ya Kusini ya Lindi na Mtwara waweze kupata masomo haya ya hesabu na sayansi ili tuweze kulingana na wanafunzi wa maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado Mkoa wa Lindi ni mkoa ambao umesahaulika, tunaitwa mikoa ambayo imesahaulika, ni mikoa maskini, mikoa ambayo iko pembezoni. Kwa hiyo, Mkoa wa Lindi ni mojawapo ya mikoa hiyo lakini Serikali ilituambia kwamba bajeti hizi zitazingatia mikoa ile ambayo iko pembezoni mwa mji. Tunaiomba Serikali iutazame Mkoa wa Lindi ukizingatia kwamba ni mkoa ambao umesahaulika. Kwa hiyo, tuna matumaini makubwa sana kuona kwamba Serikali inatubeba kwa nguvu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia ukurasa wa 26, umeelezea masuala mazima ya elimu na ufundi stadi. Mimi naipongeza sana Serikali kwa sababu sasa imeonesha kwamba inataka kuendeleza ujenzi wa Vyuo hivi vya Ufundi Stadi katika Mikoa ya Mwanza, Geita, Simiyu pamoja na maeneo mengine Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Mkoa wa Lindi tumebahatika kupata Chuo cha VETA na kipindi kilichopita nilizungumzia chuo hiki kwamba kina changamoto mbalimbali ikiwemo miundombinu ya majitaka, lakini bado mpaka leo tatizo hili lipo linaendelea. Pia Chuo kile cha VETA hakina mabweni na tunategemea wanafunzi kutoka Wilaya za Mkoa wa Lindi wapate mafunzo pale wale ambao hawakubahatika kuendelea na masomo, lakini wazazi wanashindwa kwa sababu mazingira ya kuishi mzazi anapanga nyumba. Leo mzazi ampangie nyumba mtoto wa kike, hivi kweli tunamtakia kheri mtoto huyu wa kike akae kwenye nyumba ya kupanga peke yake, hana mtu wa kumtazama na gharama za chakula mzazi agharamie? Kwa hiyo, inakuwa ni mzigo mzito na kusababisha baadhi ya Wilaya za Mkoa wa Lindi wanashindwa kumudu kuwaleta watoto wao pale...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana.