Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi nichangie Wizara hii ya Elimu.

Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara hii pamoja na walimu wote wa shule za msingi pamoja na shule za sekondari, wanafanya kazi katika mazingira magumu sana, lakini hawana nyumba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipata mradi wa MMEM tumejenga madarasa, tukasahau nyumba za walimu, tumepata mradi wa MMES tumejenga madarasa, tumesahau nyumba za walimu. Kwa hiyo, walimu wanaishi katika mazingira magumu sana na ndiyo maana elimu inashuka. Tusilaumu walimu kwamba kwa nini elimu inashuka ni kwa sababu ya mazingira wanayoishi.

Mheshimiwa Mwenyeki, jambo la pili ni ukarabati wa vyuo na shule za sekondari kongwe. Mheshimiwa Waziri nikushukuru sana, Chuo cha Ualimu Mpwapwa kimekarabatiwa vizuri sana pamoja na Shule ya Sekondari ya Mpwapwa ambayo ilianzishwa mwaka 1926. Hata hivyo, kwa nini mnakarabati vyuo na shule za sekondari, nyumba za walimu hamkarabati? Bahati nzuri Mheshimiwa Waziri umefika Mpwapwa mara nyingi sana wakati wa ukarabati wa chuo cha ualimu. Ukifika Kijiji cha Mwanakianga angalia kushoto nyumba za walimu zina hali mbaya sana, nyingine zimejengwa mwaka 1926. Kwa nini hatuna huruma na hawa walimu wetu jamani? Nyumba imechakaa mtu anaishi katika mazingira magumu sana. Pangeni fungu mkarabati nyumba za walimu wa sekondari pamoja na walimu wa Chuo cha Ualimu Mpwapwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu elimu bure. Kwa kweli wananchi wanashukuru sana likiwemo Jimbo langu la Mpwapwa na Wilaya ya Mpwapwa kwa ujumla. Hata hiyo, elimu bure ni kutoka darasa la kwanza mpaka kidato cha nne lakini kidato cha tano na cha sita wameachwa. Mheshimiwa Waziri hawa wote ni wako, hiyo shule ina form one mpaka form six, wengine wamesamehewa wengine hawakusamehewa, wanajisikiaje wale wanafunzi? Nakuomba sana Mheshimiwa Waziri hawa nao muwasamehe, ni watoto wa Serikali moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende upande wa shule huko huko kuhusu chakula wanachopata wanafunzi wa bweni cha shilingi 1,500 kwa siku. Hivi kweli Mheshimiwa Waziri upewe shilingi 1,500 unywe chai asubuhi, chakula cha mchana na chakula cha jioni itatosha? Kwa nini tunawaweka katika mazingira magumu sana wanafunzi wetu? Mimi nashauri tuongeze hii posho ya chakula angalau wapate shilingi 2000 inaweza kusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni maslahi ya walimu. Walimu wanafanya kazi katika mazingira magumu, lakini kila Wilaya walimu wanadai maslahi yao ya likizo, mishahara na wengine wamepandishwa vyeo. Kwa hiyo, nakuomba sana Mheshimiwa Waziri shughulikia maslahi ya walimu wetu. Walimu wakidai posho zao muwalipe mapema. Mtu anatoka kijijini anakuja mjini kwa DEO, anakaa pale wiki nzima anafuatilia maslahi yake. Naomba sana Mheshimiwa Waziri, hawa walimu lazima tuwaheshimu, hakuna mtu ambaye hakupitia darasani hapa, lazima tuwape heshima yao walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ya kwangu yalikuwa ni hayo, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi, lakini nimuombe sana Mheshimiwa Waziri pangeni bajeti maalum kwa ajili ya kujenga nyumba za walimu. Wananchi wamejenga shule za msingi, shule za sekondari na sasa Serikali imeanzisha kidato cha tano na cha sita katika baadhi ya shule, mfano, katika Wilaya ya Mpwapwa Shule ya Sekondari ya Wasichana Mazae na Shule ya Sekondari ya Wavulana ya Berege, lakini hakuna nyumba za walimu wala hostel, wanafunzi hawa wa form five na six wanalala madarasani. Naomba sana Mheshimiwa Waziri tuwaonee huruma wananchi wamefanya kazi kubwa sana. Shule zote za msingi na sekondari madarasa yote wamejenga wenyewe, tuwaonee huruma na Serikali nayo iweke mkono wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, nikushukuru na naunga mkono kwa asilimia mia moja hoja ya Mheshimiwa Waziri. Ahsante sana.