Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi ya kuchangia hoja ya Wizara ya Elimu, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Profesa Ndalichako, Naibu Waziri Mheshimiwa Ole Nasha, Katibu Mkuu, Naibu Makatibu Wakuu na watendaji wote kwa hotuba nzuri, na vilevile kwa kazi kubwa wanayoifanya kuhakikisha elimu inaendeshwa vizuri nchini kwetu katika kukuza rasilimali watu ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kupongeza Kamati ya Kudumu ya Bunge la Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa taarifa nzuri iliyojaa uchambuzi na mapendekezo mazuri na ya kimkakati ambayo yakizingatiwa yote kwa ujumla wake yanaweza kuboresha kwa kiasi kikubwa sana sekta hii ya elimu nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, napenda nijikite kwenye suala la VETA. VETA ni taasisi ya Serikali iliyoanzishwa kwa ajili ya kutoa elimu na mafunzo ya ufundi stadi, hizi zikiwa ni stadi za kazi kwa ajili ya kuandaa vijana na jamii kwa ujumla waweze kujiingiza katika shughuli zenye kuwapatia kipato cha kujikimu kimaisha na pia kuchangia katika pato la Taifa. Taasisi hii ya VETA inafanya kazi kubwa ya kuwapa vijana wetu stadi za kazi, lakini pia inatoa nguvu kazi kwa ajili ya viwanda. VETA pia ndio mojawapo ya mihimili ya kufanikisha mkakati wa Serikali kuanzisha viwanda. Bila nguvu kazi yenye stadi zinazohitajika na viwanda hatutaweza kufanikisha mkakati huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbili, kulingana na sheria iliyoanzisha VETA ya mwaka 1994, VETA ni taasisi ambayo inaendeshwa kwa michango inayotolewa na waajiri kwa njia ya Skills Development Levy(SDL) ambapo waajiri wanakatwa asilimia 4.5 ya fungu la mishahara (wage bill) kila mwezi. Hata hivyo VETA inapata theluthi moja tu ya makato hayo, theluthi mbili zinabaki Serikalini. Sehemu kubwa ya waajiri wanatamani VETA ipate 100% ya makato yote yaani 4.5% inayokatwa ili soko la ajira lipate mafundi mahiri walioiva vizuri na mafunzo toka VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi inatakiwa iwajibike kwa waajiri ambao ndio wana gharamia uendeshaji wa taasisi hiyo. Hawa waajiri wako chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Ajira na Watu Wenye Mahitaji Maalum. VETA ipo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Kimsingi VETA inatakiwa iwajibike kwa waajiri kwa njia mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kuhakikisha waajiri kuwa mafunzo yanayotolewa na VETA yanaendana na mahitaji ya waajiri na kuwa mitaala ya VETA inayotumika kufundishia inabadilishwa mara kwa mara kulingana na mahitaji ya waajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbili kuhakikisha matumizi ya fedha za SDL (1/3 SDL) ambayo ni michango ya waajiri kuendeshea VETA inatumika kama ilivyokusudiwa. Pia waajiri wakipendezwa na matumizi ya michango yao wanaweza kutafuta njia nyingine za ziada za kuisaidia VETA ili ikidhi matarajio yao waajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo huu uliopo sasa ambao waajiri na VETA wapo kwenye Wizara mbili tofauti, VETA haitaweza kuwajibika kwa waajiri moja kwa moja. Hivyo uhusiano wa VETA na waajiri wanaoigharamia ni dhaifu. Hii inaweza kufanya waajiri kukosa imani na utendaji wa VETA maana hawana mamlaka juu ya utendaji wao. Waziri wa Elimu hana nguvu ya kisheria ya kuitisha kikao cha waajiri kuzungumzia masuala ya elimu na mafunzo ya ufundi stadi zinazohitajika katika soko la ajira, kwa sababu hawa waajiri wako chini ya Wizara nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Waziri anayehusika na kazi hana nguvu ya kisheria ya kuiagiza mamlaka inayosimamia mafunzo ya ufundi stadi yaani VETA kurekebisha mitaala yao kutegemea mabadiliko katika soko la ajira maana VETA iko chini Wizara nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo wa utoaji wa mafunzo ya ufundi stadi kwa sasa inahusisha waajiri (wenye viwanda) kutoa mafunzo wakishirikiana na kupokezana na vyuo vya ufundi stadi (Dual Apprenticeship Training). Utaratibu huu unahitaji ushirikiano wa karibu sana kati ya waajiri (viwanda) na vyuo vya ufundi stadi. Hali ya namna hii inahitaji miongozo ya Wizara mama. Tunapokuwa na Wizara mbili tofauti ni vigumu sana kutengeneza miongozo hiyo kwa sababu tofauti za majukumu ya Wizara husika na hata usimamizi wake unakuwa mgumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri VETA iwekwe chini ya Wizara moja na waajiri yaani Waziri Mkuu, Kazi, Ajira, Watu Wenye Mahitaji Maalum. Hii italeta mahusiano mazuri kiutendaji na italeta ufanisi kiutendaji kwenye kipindi hiki muhimu cha kuandalia mafundi stadi kwa ajili ya ustawi wa viwanda vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande mwingine Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ina vitengo vingi sana. Wizara inashughulikia Elimu ya Juu, Elimu ya Vyuo vya Kati, Elimu ya Sekondari, Elimu ya Msingi, Elimu ya Awali, Elimu ya Watu Wazima, Elimu ya Ufundi, Elimu ya Mafunzo ya Ufundi Stadi, Taasisi ya Mitaala TIE, Baraza la Mitihani, TCU, NACTE, VETA, TEA, Maktaba ya Taifa, Bodi ya Mikopo na taasisi nyingine. Pia changamoto zilizopo katika Wizara hii ni nyingi sana na ni vigumu kuweza kupata muda wa kusimamia kikamilifu elimu na mafunzo ya ufundi stadi ambayo ina mtizamo tofauti na idara nyingine za elimu. Pia kuna hatari ya kuifananisha elimu ya ufundi stadi na elimu ya msingi au sekondari ambapo sehemu kubwa ya elimu ya ufundi stadi ni vitendo kuliko nadharia tofauti na elimu ya sekondari na msingi. Upana na utawala wa Waziri wa Elimu (span of control) ni pana sana jambo ambalo linaweza kuathiri ufanisi katika utendaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko nchi nyingi duniani ambazo sekta ya ufundi stadi ipo chini ya Wizara ya Kazi mfano, Korea Kusini, Indonesia, Singapore, Malaysia na kadhalika. Nashauri Serikali irejeshe VETA iwe chini ya Wizara ya Kazi kama ilivyokuwa zamani na hasa kipindi hiki tunapojenga uchumi wa viwanda ili VETA iweze kuwa na ushirikiano wa karibu na waajiri kwa nia ya kutoa stadi zinazohitajika kwenye soko la ajira yaani demand driven trainingAINING” katika kujenga uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya Wizara imeonesha kwenye ukurasa 26 na 27 umezungumzia Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA). Wilaya ya Ileje kupitia Mbunge tulipata ufadhili wa Balozi wa Japan na kujenga majengo ya VETA na kutokana na uwezo mdogo
wa Wilaya tuliwasiliana na Wizara yako na kuomba Serikali iichukue hii VETA na kuiendesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulishauriwa tuongeze eneo, na kupima eneo la VETA ndipo Wizara kupitia VETA Makao Makuu wataichukua na kuiendesha. Yote haya yamefanyika na kwa barua ya Halmashauri ya Ileje ya tarehe 05 -11-2017 kuainisha kuwa tayari masharti yote yamekamilishwa na sasa tunaomba Serikali ichukue VETA Wilaya kuiendesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika kuona kuwa katika hotuba ya Waziri hakuna popote VETA ya Wilaya ya Ileje kuainishwa ili hali ni ahadi na maagizo ya Wizara yenyewe, VETA hii imesimama kwa miaka mitatu sasa hata mfadhili yaani Balozi wa Japan amesikitika sana na ameshindwa kuendelea kusaidia hadi VETA izinduliwe na ianze kazi. Kwa hiyo, ninaomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha atueleze wana Ileje hii VETA yetu wataichukua lini? Kwa hiyo, nguvu za Mbunge na mfadhili ziende bure?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kutoa pendekezo kuwa Wizara ioneshe jinsi mitaala ya elimu ya ufundi stadi inaendana na mkakati wa Serikali ya uchumi na viwanda. Vilevile mitaala ya ufundi stadi iboreshwe na kuwekewa madaraja ya standard seven, form four, form six na wa diploma kwa maana ya kuzi-upgrade VETA nyingine into polytechnics ambazo zinatumia ujuzi juu na teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Wizara sana kwa kutupatia fedha za kukarabati shule za msingi kongwe tatu. Kati ya shule kongwe za msingi 14 za Wilaya ya Ileje, shule zilizosalia nazo ni kongwe, na miundombinu yake ya mwanzo na ni za ujenzi wa kutumia udongo. Kwa hiyo, ni hatarishi kwa wanafunzi maana zimeharibika sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ileje haina maktaba ya Wilaya tofauti na Wilaya nyingine, hili ni tatizo. Kuweka maktaba kungesaidia hata watu wengine kupenda kujisomea zaidi ya wanafunzi na watu wazima, lakini vilevile kwa wanafunzi na raia wanaohitaji kujiendeleza kimasomo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumejitokeza mtindo wa kugeuza vyuo vya kati kuwa vyuo vikuu, hii ni hatari. Vyuo vya kati viendelezwe kuwa vyuo bora kwa kutumia teknolojia sahihi na uhitaji wa viwanda na viweze kuzalisha watoa huduma katika viwanda vidogo na kwa viwanda vikubwa. Kwa mfano Singapore wameboresha vyuo vya kati, vinachangia ajira kwa asilimia 95 kwa kuimarisha mitaala ya kiteknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamwangukia Mheshimiwa Waziri anisaidie nipate shule ya sekondari ya wasichana Ileje tena yenye mrengo wa sayansi, hisabati na teknolojia na lugha za kigeni. Tunajitahidi kujiandaa kama Wilaya kuanza shule hiyo, lakini Wilaya yetu ni maskini mno, ila wananchi wamejitolea maeneo mawili hata ya Ibada na Mlaly ya ekari 22 kila moja kwa ajili ya ujenzi wa shule za sekondari za wasichana kidato cha kwanza hadi cha nne. Naomba sana Mheshimiwa Waziri anipe jibu la kututia moyo Ileje hususan kwa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ileje ina changamoto nyingi. Kubwa ni upungufu wa walimu 201 wa elimu ya msingi na wa shule ya sekondari hasa wa sayansi takibrani 50; na zaidi Idara ya Elimu Msingi haina gari tangu mwaka 2010. Shule za A-Level ni mbili tu Wilaya nzima. Tunahitaji kuongezewa shule nyingine mbili. Miundombinu ya shule zetu zote ni mibovu, haina vyoo, ofisi za walimu, nyumba za walimu, mabweni na madarasa. Tunaomba sana sisi wa Wilaya za pembezoni tuangaliwe kwa jicho la huruma, tumesahauliwa kwa muda mrefu. Tunaomba utusaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja.