Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake yote kwa kazi nzuri wanayoifanya pamoja na hotuba yake nzuri iliyojaa kutatua kero za elimu kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishukuru Serikali yangu tukufu inayoongozwa na Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutoa elimu bure kuanzia darasa la kwanza mpaka kidato cha nne. Ili kuendeleza juhudi hizi niishauri Serikali iwape vitendea kazi wakaguzi wa elimu katika Wilaya kwani idara hii ndiyo ambayo itakayoweza kusimamia hili suala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali ijenge vyuo vya VETA katika kila Wilaya kwani itakuwa mkombozi kwa watoto wetu wanaomaliza elimu ya msingi na sekondari walioshindwa kuendelea na masomo, kwani watoto hawa wakipitia kwenye vyuo vyetu vya VETA walio wengi watakuwa wanajiajiri wenyewe kupitia maarifa waliyoyapata kwenye vyuo vyetu vya VETA. Hii itakuwa mwarobaini kwa watoto wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali iangalie stahiki zote za walimu. Kuna malimbikizo makubwa ya walimu ambayo bado hawajapewa na walimu hawa wananung’unika, hili si jambo zuri kwa walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo walimu wanaoishi vijijini wanaishi katika maisha magumu sana. Kwa sababu hiyo, niiombe Serikali yangu tukufu ijenge nyumba za walimu hasa waishio vijijini pamoja na kumalizia madarasa yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi pamoja na maabara. Wananchi wameshajenga maabara hizo na kazi iliyobaki ni upande wa Serikali pamoja na kuongeza walimu wa kutosha katika shule zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na baadhi ya watendaji katika Halmashauri kuingilia kazi za wakaguzi. Niiombe Serikali itoe tamko kwa watendaji hawa kutoingilia kazi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali kuwa wanafunzi wote wakatiwe bima ya afya, hasa kwa wale wambao wanaishi boarding. Serikali ihakikishe watoto hawa wanapata bima hiyo ili waweze kupata matabibu bure kwani hii inaleta usumbufu mkubwa hasa kwa walimu, maana inatokea mtoto anaumwa na mwalimu mnamkuta hana hela na mwalimu hawezi kumuacha mwanafunzi kumpeleka hospitali atakopa au atatumia maarifa yake kuhakikisha mtoto anapata matibabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali yangu ipunguze masharti ya kusajili shule hasa hizi za msingi. Hata ikiwa shule hizi zina madarasa mawili isajiliwe tu ili kuondoa usumbufu kwa watoto wetu hasa kwa wale wanaokaa mbali na shule na hii itapuguza watoto kutotoroka shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Elimu ya Watu Wazima; elimu hii ni muhimu sana kwani ilifika mahali watu wazima wasiojua kusoma na kuandika ilipungua mpaka asilimia sita ya Watanzania, lakini sasa hivi imeongezeka mpaka kufikia asilimia 30. Hii ni ishara ya kuwa elimu hii haitiliwi mkazo katika Taifa letu. Hivyo basi niiombe Serikali itilie mkazo elimu hii ya watu wazima, ukizingatia sasa hivi kuna mfumo mzuri wa kuwafundisha watu wazima na wale watoto ambao wameshindwa kabisa kusoma na kuandika, inaitwa Graph Game.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wewe mwenyewe ni shahidi kwani wadau wa GG walikuja mpaka kwako na wadau hawa wamesaidia sana katika Jimbo la Lushoto kwa baadhi ya shule kwani kuna watu wazima zaidi ya 200 kwa sasa wanaojua kusoma na kuandika. Pia kuna watoto ambao walishindikana kabisa kujua kusoma na kuandika, lakini walivyotumia mfumo wa Graph Game sasa hivi wanajua kusoma na kuandika na ndio wanaoongoza madarasani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niishauri Serikali yangu tukufu iwasaidie wadau hawa ili waweze kukomboa watoto wetu pamoja na watu wazima hawa. Serikali iwajengee uwezo wadau hawa wa GG na hili Mheshimiwa Waziri ili ulione kuwa ni mkombozi wa Watanzania naomba upange ziara ya kutembelea Lushoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la michezo shuleni, hii elimu ya michezo haitiliwi umuhimu wakati tunajua kama michezo ni taaluma kama taaluma nyingine. Kwa hiyo, kujengwe vyuo vya michezo au hivyo hivyo vya VETA vifundishe na somo la michezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naunga mkono hoja asilimia mia moja.