Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako tukufu ili niweze kuhitimisha hoja yangu ambayo niliwasilisha tarehe 30 Aprili, 2018. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuendelea kuniunga mkono katika kazi yangu na kwa uongozi wake ambao umetukuka. Kwa dhati kabisa napenda kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye yeye ndiye msimamizi mkuu wa shughuli za Serikali na hakika yeye ni kiranja kweli kweli, anatusimamia kweli kweli. Mheshimiwa Waziri Mkuu tunakushukuru sana kwa uongozi wako mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dhati kabisa napenda kukushukuru wewe wa kuniongozea mjadala wa hoja yangu tangu nilipoiweka mezani na mpaka sasa tunapohitimisha. Nakushukuru sana umeongoza hoja hii vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa shukrani za dhati kabisa kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii chini ya Uenyekiti wa Mheshimiwa Peter Serukamba na Makamu Mwenyekiti Mheshimiwa Juma Nkamia kwa ushirikiano mkubwa sana ambao ninaupata kutoka kwa Kamati hii. Nawashukuru sana kwa mchango mzuri ambao wameutoa katika hoja yangu na ninaahidi kwamba nitaendelea kuwapa ushirikiano na kuendelea kufanyia kazi maoni na ushauri mzuri ambao wananipatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe shukrani za dhati kwa Naibu Waziri wangu kwa ushirikiano mzuri anaonipatia, Katibu Mkuu, Naibu Makatibu Wakuu na watendaji wote ambao tumeshirikiana katika kuhakikisha kwamba tunafaikisha hoja hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwashukuru washirika wa maendeleo lakini kipekee naomba nimshukuru Bi. Alice Birnbaum ambaye ni Mwenyekiti wa Washirika wa Maendeleo kutoka Canada lakini yeye ndiye Mwenyekiti wa Wadau wa Maendeleo ya Elimu; Ndugu Pantaleo Kapich kutoka UNICEF; Ndugu John Lusingu kutoka DFID, Ndugu Helen Reutersward kutoka SIDA; Ndugu Faith Shayo kutoka UNESCO na Ndugu Mwanahamisi Singano kutoka Sekretarieti ya Development Partners. Hao wamekuwa na mimi tangu nilipowasilisha hoja hii na mpaka sasa hivi wapo wanaangalia ninavyohitimisha, nasema ahsanteni sana, thank you very much. Naamini kukaa kwenu hapa mmesikia hoja za Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo, nikija kwenu kuomba ili…

KUHUSU UTARATIBU . . .

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hata maandiko matakatifu yanatufundisha kwamba tushukuru Mungu kwa kila jambo. Hawa watu wametusaidia tumejenga madarasa, kwa hiyo, mimi nawashukuru, naomba niendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba niwashukuru sasa Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia hoja hii. Naomba nimalizie kwa kumshukuru mama yangu mzazi pamoja na mdogo wangu ambao wapo hapa kwa kuendelea kuniunga mkono, ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo, naomba niseme kwamba hoja yangu imepata michango mingi ya Waheshimiwa Wabunge ambapo jumla ya Wabunge 117 wamechangia hotuba. Waheshimiwa Wabunge 77 wamechangia kwa maandishi na Waheshimiwa Wabunge 46 ambao wamechangia kwa kuongea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kanuni haziniruhusu kuwataja Waheshimiwa Wabunge waliozungumza, majina yao ninayo hapa na nitaomba orodha yao iingie kwenye Hansard. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa unyenyekevu kabisa naomba nitoe shukrani za dhati kabisa kwa Waheshimiwa Wabunge wote ambao mmechangia. Kwa kweli michango yenu imekuwa ni mizuri sana na inaonesha ni jinsi gani ambavyo mnaithamini elimu. Kuonesha jinsi ambavyo michango imekuwa mizuri, leo tumepata mpaka na pambio kutoka kwa Mheshimiwa Mbatia, ametuimbia na wimbo wa chekechea. Waheshimiwa Wabunge nawashukuru sana na ninawaahidi kwamba michango yenu yote nimeipokea na nitaizingatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda sitaweza kujibu hoja zote, lakini naomba nizungumzie mambo machache ambayo yamezungumziwa na Waheshimiwa wengi, lakini pia nitajikita kujibu hoja ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wajumbe wa Kamati yangu. Kwa bahati nzuri hoja ambazo zimetolewa na Kamati pia zimekuwa ni hoja ambazo zimezungumziwa na Waheshimiwa Wabunge wengi. Kwa hiyo, napotoa maelezo nitakuwa sitaji hoja imetoka kwa nani lakini nitakuwa najikita kwenye hoja moja kwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ulikuwa unawahisha shughuli kaka yangu hapa wewe tulia tu hakuna shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nizungumzie hali ya elimu, ni suala ambalo limezungumzwa sana, limezungumza na Kamati yangu, lakini pia limezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge wengi sana ambao wamechangia. Katika hoja hii wamesema kwamba hali ya elimu katika nchi yetu inashuka na kuna changamoto nyingi katika utoaji wa elimu katika nchi yetu, miundombinu, upatikanaji wa walimu na vifaa toshelezi vya kufundishia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kuelezea kwamba elimu katika nchi yetu imekuwa ikipita katika vipindi mbalimbali. Tumekuwa na kipindi ambacho tulikuwa na changamoto sana ya uandikishaji katika shule za msingi na sekondari, tukaja na Progamu ya Maendeleo ya Elimu ya Msingi almaarufu kama PEDP ambayo iliongeza udahili wa wanafunzi katika shule za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tulikuwa na changamoto ya udahili mdogo katika shule za sekondari na tukawa na Programu ya Mpango wa Maendeleo ya Sekondari. Vilevile kulikuwa na mkakati wa dhati kabisa wa kujenga shule ya sekondari katika kila kata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango hii imekuwa na mafanikio makubwa sana. Ukiangalia idadi ya shule za sekondari zilizokuwepo, mwaka 2005 zilikuwa 1,202 na kutokana na mikakati hii hadi kufikia mwaka 2010 jumla ya sekondari zilizokuwepo nchini zilikuwa 3,508. Mafanikio haya yalienda sambamba na ongezeko kubwa la wanafunzi ambao waliongezeka kutoka wanafunzi 524,324 hadi kufikia 1,401,330 kutoka mwaka 2005 hadi 2010.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mafanikio haya ya ongezeko kubwa la wanafunzi ni dhahiri kwamba yaliambatana na changamoto kama vile miundombinu ambayo sasa haitoshelezi kama vile madarasa, ofisi za walimu, mabweni na maabara lakini pia ilileta uhaba mkubwa wa walimu. Sote tunafahamu tulipokuwa tunatekeleza mpango wa PEDP na SEDP kulikuwa na upungufu mkubwa wa walimu. Serikali ilifanya jitihada za kukabiliana na changamoto ya walimu kwa kuwa na mikakati mbalimbali ambapo bado utoshelezi haujafikiwa hasa katika masomo ya sayansi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua haya, Rais wetu wa Awamu ya Tano, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli alipokuwa ameingia madarakani alikuwa anatambua fika kwamba amekabidhiwa nchi ikiwa na changamoto ambazo zilitokana na mafanikio ya kuongeza upatikanaji wa nafasi za elimu kwa watoto wa Kitanzania kwenye elimu ya msingi na elimu ya sekondari. Kwa kutambua hayo, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipokuwa analizindua Bunge hili tarehe 22 Novemba 2015, alizungumza na naomba kunukuu; “Natambua juhudi kubwa zimefanyika katika upanuzi wa elimu ya awali, msingi, sekondari na vyuo vikuu. Serikali ya Awamu ya Tano itajielekeza katika kuongeza ubora wa elimu inayotolewa ikiwa ni pamoja na kuongeza mkazo katika masomo ya sayansi.” Mwisho wa kunukuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema hayo ili kukumbusha kwamba elimu imekuwa ikipitia katika vipindi mbalimbali na Mheshimiwa Rais alitambua changamoto zilizokuwepo na alizungumza ndani ya Bunge lako Tukufu. Nimpongeze sana Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa sababu ametekeleza ahadi yake kwa vitendo. Ndani ya kipindi chake cha uongozi tumeona akitekeleza kwa vitendo uboreshaji wa elimu na nitaeleza kwa uchache mambo ambayo yamefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na uboreshaji wa elimu, Mheshimiwa Rais akaanzisha utoaji wa elimu bila malipo. Kwa kweli hiyo ni commitment kubwa huku unaboresha elimu na wakati huo unatoa elimu bila malipo. Utoaji wa elimu bila malipo nao umekuja na mafanikio makubwa sana, idadi ya wanafunzi waliojiandikisha darasa la kwanza iliongezeka kutoka 1,386,592 hadi kufikia 1,896,584. Kwa hiyo, kwa maneno mengine changamoto ya madarasa ikazidi kuongezeka kutokana na ongezeko la wanafunzi ambao wanakwenda shuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano katika sekta ya elimu ni kazi ambayo inaonekana wazi kabisa, haijajificha. Nenda katika Halmashauri yoyote utaona kazi nzuri ambayo imefanywa na Serikali ya Awamu ya Tano katika sekta ya elimu. Kuna miundombinu ambayo inajengwa, lakini vilevile kumekuwa na kuhakikisha kwamba tunapeleka vifaa vya maabara. Kwa kweli, niseme tu kwamba Waheshimiwa Wabunge suala la kuboresha elimu ni commitment ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano na analitekeleza kwa vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme tu kwa uchache mambo ambayo yamekwishafanyika kutoka Serikali Kuu, tukumbuke kwamba ujenzi wa miundombinu ni jukumu la TAMISEMI, hizo kazi zinafanywa na Halmashauri zetu, lakini kwa kutambua uzito na mzigo ambao halmashauri zilikuwa zinaelemewa Serikali ya Awamu ya Tano imeona pia nayo ishiriki katika kuangalia yale maeneo ambayo yana changamoto kubwa tumekuwa tukipeleka kuwaunga mkono. Kwa hiyo, tayari jumla ya madarasa 1,947 na mabweni 338 yamekwishajengwa. Tumekuwa tukizungumzia hapa adha ambayo mtoto wa kike anaipata kutembea umbali mrefu kwenda shuleni. Serikali ya Awamu ya Tano inaliona hilo na kwa kupitia Serikali Kuu tayari tumekwishajenga mabweni 338 sambamba na yale ambayo yanajengwa na Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile matundu ya vyoo tumekwishajenga 4,501; nyumba za walimu 95; maktaba nne, majengo ya utawala 21 na mabwalo 14. Haya ni yale ambayo yamefanywa na Serikali Kuu, lakini hayajajumuisha idadi ya vyoo ambavyo vimejengwa katika Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tumeshuhudia jinsi ambavyo shule zetu kongwe zilikuwa zipo katika hali mbaya, zilikuwa zipo choka mbaya kweli kweli, lakini Serikali ya Awamu ya Tano inakarabati shule kongwe na tayari tumeanza na shule 46 na mpaka sasa hivi tumekwishakamilisha shule 20 na ukarabati wa hizi shule nyingine unaendelea na shule zote kongwe 88 zitakarabatiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, hata vyuo vyetu vya ualimu vilikuwa katika hali ya uchakavu. Tumekwishafanya ukarabati katika vyuo vya walimu 22 na dada yangu Mheshimiwa Esther Matiko hata kwake Tarime tumefika tunafanya ukarabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali inaendelea na uboreshaji wa miundombinu katika sekta ya elimu ikiwa ni pamoja na vyuo vikuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuonyesha dhamira ya Mheshimiwa Rais wetu muungwana, akiahidi anatekeleza, hata bajeti ya mwaka huu ambayo nimesimama Waheshimiwa Wabunge na naomba wote kwa pamoja muiunge mkono kwa sababu elimu ndiyo uti wa mgongo wa maendeleo ya nchi yetu na kwa hiyo elimu haina itikadi, naomba mtuunge mkono bajeti yetu ya maendeleo imeongezeka kutoka shilingi 916,841,822 hadi shilingi 929,969,402. Kwa hiyo, hiyo, inaonesha dhamira ya dhati ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano katika kuboresha elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwaambie tu Waheshimiwa Wabunge hata Roma haikujengwa kwa siku moja, lakini jitihada kubwa zinafanyika, muendelee kumuunga mkono Mheshimiwa Rais wetu na nina hakika kwa hapa tulipoanzia tutafika na elimu yetu itakaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya pia usambazaji wa vifaa, tumekuwa tukinunua vifaa vya maabara na tumepeleka katika shule 1,696. Kama mnakumbuka ahadi ya Mheshimiwa Rais ilikuwa pia kuboresha mambo ya ufundishaji wa sayansi. Tunatambua pia kwamba ili elimu iweze kwenda vizuri lazima kuwe na mwalimu bora. Kwa hiyo, Serikali imekuwa ikiwekeza pia katika mafunzo kwa walimu kazini. Katika hili tumefanya sana, tumeweza kutoa mafunzo kwa walimu wa awali 16,129; tumetoa mafunzo kwa walimu wanaofundisha stadi za kusoma, kuandika na kuhesabu ambazo Mheshimiwa Mbatia naona naye atakuja kuungana nao ili aweze kufundisha kwa nyimbo zake zile nzuri walimu 65,232; tumetoa mafunzo kwa walimu wenye mahitaji maalum 800 na vilevile tumetoa mafunzo kwa walimu wa sekondari 12,726 kati ya hao walimu wa sayansi 10,614 na walimu wa lugha 2,112. Hayo ni kwa uchache tu kwa sababu ya muda siwezi kuelezea mambo ambayo Serikali ya Awamu ya Tano inafanya kuboresha elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge tuungane na tuhakikishe kwamba ule upungufu ambao tunaweza tukaenda kwa kasi zaidi, ushauri wenu tunaupokea, tutaufanyia kazi lakini tunatambua kwamba tumetoka mbali katika historia ya elimu yetu. Tusiangalie tu Awamu ya Tano, lakini kama nchi historia ya elimu yetu imekuwa katika mapito mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala ambalo limezungumzwa sana hapa la wahitimu kumaliza bila kuwa na umahiri unaotakiwa. Wamezungumzia watu wanamaliza elimu ya msingi, hawajui kusoma na kuandika, watu wanamaliza vyuo vikuu, mtu anachukua sheria lakini hawezi kuandika hukumu na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili naomba niseme kwamba Serikali itaendelea kuimarisha usimamizi na ufuatiliaji katika sekta ya elimu. Niungane mkono na Kamati yangu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, wamenukuu Taarifa ya Benki ya Dunia kuhusu viashiria vya utoaji huduma (service delivery indicators) ambazo zinaonesha kwamba walimu wanakuwa shuleni, lakini hawaingii madarasani au wakati mwingine hawafiki shuleni kabisa. Hali hii inaonesha kutowajibika kwa viongozi ambao wamepewa dhamana ya kusimamia elimu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba hapa katika sekta ya elimu tuna bahati kwa sababu tuna usimamizi mpaka kwenye ngazi ya kata, tuna Afisa Elimu Kata.

Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kutoa maagizo kwa Maafisa Elimu wote nchini kuhakikisha wanafanya kazi yao ipasavyo, wasimamie kwa karibu elimu na kuhakikisha kwamba walimu wanafundisha kama inavyotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaase waache mtindo wa kumchukulia mwalimu sasa kama ndio mtu wa kulaumiwa yanapotokea matatizo, mwalimu ndiyo anaachishwa kazi. Kwa nini usubiri matokeo ya mtihani shule yake ikifanya vibaya ndiyo umuachishe kazi, ulikuwa wapi mwaka mzima kumfuatilia, kuangalia anafanya nini, unasubiri matokeo ya mtihani yeye ndiyo umfukuze kazi. Hiyo sio sawa, ni uonevu kwa wakuu wa shule kwa sababu na wenyewe wana viongozi juu yao, kwa nini wao ambao wanatakiwa kuwasimamia wasiwajibishwe? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaagiza Maafisa Elimu wafanye kazi yao vizuri. Maafisa Elimu wa ngazi ya Kata unakuta mtu ana shule tano tu, utashindwaje kuzisimamia au utashindwaje kuona matatizo. Kwa hiyo, katika hili Serikali itahakikisha tunaimarisha usimamizi ikiwa ni pamoja na kuwaondoa viongozi ambao ni mzigo, ambao ndiyo wanaotufikisha hapa. Serikali inafanya kazi kubwa ya kuwekeza, lakini kama hakuna usimamizi imara katika sekta ya elimu tutakuwa kama vile tunatwanga maji kwenye kinu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa taasisi za elimu ya juu na vyuo vya kati, wahitimu wanamaliza hawawezi hata kuandika hukumu, tunavyo vyombo ambavyo vimepewa mamlaka kisheria vya kuhakikisha vinadhibiti ubora katika elimu ya kati na elimu ya juu. Tunalo Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na tuna Tume ya Vyuo Vikuu nchini. Kwa hiyo, hii nayo inadhihirisha kwamba pengine zana wanazozitumia katika kufanya ukaguzi zinahitaji kufanyiwa mapitio. Kwa sababu tumekuwa tukiona hapa Tume ya Vyuo Vikuu imekuwa ikifungia vyuo kwa sababu havina sifa, tumeona hapa Baraza la Taifa la Ufundi limekuwa likifungia vyuo lakini nadhani ipo haja ya kukaa chini kwa taasisi hizi kupitia upya zana wanazozitumia kukagua vyuo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, natoa maagizo kwa Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi, wakae chini wapitie upya vigezo ambavyo wanatumia kuangalia ubora wa vyuo vyetu vikuu. Angalieni mitaala inayotumika, angalieni sifa za walimu ambao wako katika vyuo vikuu, angalieni mpaka na aina ya mitihani ambayo inatolewa, namna inavyosahihishwa ili muangalie vigezo vyote kwa ujumla wake. Kwa sababu haiwezekani tuwe tunafungia vyuo halafu bado hata vyuo ambavyo tunaviona vinafaa vinatoa wahitimu ambao hawahitajiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kutoa wahitimu ambao hawana sifa zinazotakiwa halikubaliki. Naviagiza hivi vyombo kufanya kazi yao bila kumuogopa mtu yeyote. Chuo chochote ambacho kitabainika hakina sifa, iwe ni cha Serikali, iwe ni cha binafsi, kama hakina sifa kifungiwe. Hatuwezi tukaendelea kuangamiza Taifa hili kwa kuzalisha watu ambao hawana sifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la hali ya ufaulu nchini. Suala hili pia limeongelewa sana na hata Kamati yetu imetoa takwimu kubwa na mimi nikiri kwamba hali ya ufaulu ilivyo hata na mimi natamani kwamba wanafunzi wangeweza kufaulu kwa wingi zaidi kuliko wanavyofaulu sasa. Kama nilivyotangulia kusema Waheshimiwa Wabunge ni kwamba maendeleo na hasa katika sekta ya elimu ni hatua kwa hatua. Kwa hiyo, tumekuwa kwa kweli na ufaulu ambao ukiangalia asilimia kubwa ya wanafunzi wanakuwa katika daraja la nne na daraja la sifuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu kwamba mtu anayefaulu kwa daraja la kwanza amefaulu zaidi kuliko wa daraja la nne lakini niombe tu tusije tukaweka dhana kwamba mtu aliyepata daraja la nne hafai kabisa, kwa sababu kwa vigezo tulivyonavyo sasa daraja la nne amefaulu. Suala ambalo tunaweza tukazungumza ni kama labda pengine tunaona viwango viko chini tunaweza tukafikiria hata kuviongeza lakini kwa sababu kwa viwango tulivyojiwekea daraja la nne mtu amefaulu, tusiongee katika lugha ambayo ni kukatisha tamaa. Kwa hiyo, nimesema kwamba kupata division one amefaulu vizuri zaidi, lakini kwa utaratibu uliopo sasa hivi hata aliyepata division four amefaulu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme pia kwamba suala la idadi ya ambao wamepata division one mpaka three kama nilivyosema si ya kuridhisha kwa kiwango ambacho hata Serikali ingetamani. Sisi hatuwezi kuchakachua matokeo, tunatoa matokeo kadri ambavyo yapo, lakini Serikali inachokifanya ni kutekeleza wajibu wake, kuweka miundombinu na kuhakikisha walimu wanapatikana. Kwa hiyo, pia nitumie nafasi hii kuwaomba wanafunzi nao watekeleze wajibu wao kwa sababu hata mwanafunzi naye pia ana wajibu katika kuweza kufanya vizuri katika mitihani yake, lakini hata mzazi naye ana wajibu kwa mwanafunzi kufanya vizuri. Serikali itaendelea kutekeleza wajibu wake lakini suala la ufaulu mzuri ni collective responsibility kati ya mzazi, walimu, wanafunzi na jamii kwa ujumla. Kwa hiyo, naomba kwa kweli tushirikiane na Serikali kwa sababu Serikali ina dhamira ya dhati ya kuhakikisha kwamba wanaopata daraja la kwanza mpaka la tatu wanakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ufaulu umekuwa ukiongezeka kama ninavyosema, japo siyo kwa kasi kubwa, lakini ukiangalia mwaka 2015 waliopata daraja la kwanza mpaka la tatu walikuwa asilimia 25.34; mwaka 2016 walikuwa asilimia 27.60 na mwaka 2017 walikuwa asilimia 30.15. Kwa hiyo, kuna ongezeko dogo lakini tukishirikiana na usimamizi ukawa mzuri naamini hata hii kasi ya ongezeko inaweza ikaenda vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii pia kuwaomba Waheshimiwa Wabunge tuiangalie elimu katika mapana yake kwa ujumla. Hata sisi Waheshimiwa Wabunge ulipoingia humu Bungeni siku ya kwanza na ulivyo leo, sasa hivi tuna miaka miwili na nusu uko tofauti kabisa, hakuna chaki, hakuna ubao lakini hata interaction ambayo unaipata pia ni elimu tosha. Kwa hiyo, tunapopima mafanikio ya elimu tuangalie pia katika ujumla wake hata mwamko wa wananchi kupeleka wanafunzi shule pia ni mafanikio katika sekta ya elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani Serikali ilikuwa inatumia nguvu kubwa sana kupita katika kijiji na katika kaya kuwatoa watoto ili waende shuleni lakini sasa hivi tunashuhudia mafuriko ya wanafunzi shuleni. Mimi nasema kwamba haya ni mafanikio katika elimu na mafanikio haya ndiyo yameendelea kuleta changamoto ambazo Serikali inazifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie mwamko wa wananchi katika shughuli za kijamii, unakuta hata mzee anakwenda kushiriki katika kujenga shule na zahanati. Mimi nasema haya ni mafanikio kwa sababu wangekuwa hawaoni umuhimu wa elimu wasingejitokeza kujitolea nguvu zao. Pia hata ukiona mwitikio katika masuala ya kijamii kwa ujumla, masuala ya afya, idadi ya wanawake ambao wanakwenda kliniki, yote ni mafanikio ya elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nielekee kwenye suala lingine ambalo limeongelewa kweli kweli, suala la usimamizi wa shule binafsi, lakini pia nitaliunganisha na suala la wanafunzi kukariri. Waheshimiwa Wabunge wameongea sana na wengine wameongea kwa hisia na wengine wameenda mbali kabisa wanasema kwamba Serikali inaonea wivu sekta binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na suala la kukariri na naomba nilizungumze tu vizuri, nami najua Waheshimiwa Wabunge ni waelewa, wakati mwingine pengine inawezekana hamkuwa na taarifa kamili ya jambo hili. Kimsingi niseme kwamba suala la wanafunzi kukariri ni suala ambalo lipo kwa mujibu wa taratibu na kukariri hata wanafunzi wa shule za Serikali wanaruhusiwa kukariri kwa mujibu wa utaratibu ambao umewekwa.

Kuna mitihani ambayo inatolewa, kuna mtihani wa darasa la nne mwanafunzi ambaye hafikishi alama anatakiwa kukariri na kuna mtihani wa kidato cha pili mwanafunzi anaruhusiwa kukariri. Mbali na mitihani hiyo bado kuna utaratibu ambao mwanafunzi anaweza kukariri ikiwa mzazi wake anaona kwamba uwezo wa mtoto wake ni mdogo kama ataendelea na hatua aliyofikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, utaratibu huo upo na nizishukuru sana shule binafsi kwa sababu asilimia kubwa wanatekeleza kikamilifu miongozo na taratibu za elimu. Hata hivyo, wapo wachache, tena wachache sana ambao wanakwenda kinyume na utaratibu na nitatoa mifano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Waheshimiwa Wabunge walikuwa wanazungumzia suala la wanafunzi kukariri, lakini tatizo ni zaidi ya hapo, sio tu kukariri, shule zimekuwa zikiwafukuza wanafunzi na kufukuza huko kwa kweli mimi nasema kwingine kumepitiliza. Kwa mfano, tulipokuwa tunaanza mwaka huu 2018, shule ambazo zimetoa taarifa, tulikuwa na wanafunzi 1,029 ambao wengine wako katika mwaka wa mtihani amefukuzwa tu kwa sababu hajafikia alama, siyo kwamba anakariri, hapana, anaambiwa ondoka, aende nyumbani, mzazi amelipa mamilioni ya fedha na kwa sababu mwanafunzi hakufikisha alama anaambiwa aondoke. Kwani kazi ya shule ni nini, si ndiyo kutoa elimu? Kama mwanafunzi hawezi si umwambie akae hapo umfundishe? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli suala la kuwafukuza wanafunzi si halali. Suala hili linakwenda kinyume na sheria ya elimu kwa sababu hizi shule binafsi nazo zinatakiwa zizingatie sharia hii kwa sababu sheria tunapozitunga hapa Bungeni wote tunawajibika kuzizingatia ikiwemo Serikali na kila mmoja ambaye sheria hiyo inamhusu. Sheria ya Elimu ya mwaka 1978 inasema wazi kwamba; primary school shall be compulsory for every child who has reached the age of seven years to be enrolled for primary school. Sheria hiyo inaonesha kabisa kwamba mtoto lazima asome, ahudhurie mpaka amalize, ndivyo sheria inavyosema, haisemi akifika darasa la sita kwa sababu unamuona hajafikisha alama umfukuze aende mitaani, tutazalisha watoto wa mitaani bila sababu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni kutokana na changamoto hiyo ambayo nikitoa mfano shule ya Panda Hill iliyoko Mbeya peke yake ilikuwa imefukuza wanafunzi 114, shule moja wanafunzi 114, eti hawajafikisha alama ambayo imewekwa na shule. Hivi shule moja wanafunzi 114 wakishindwa kufanya vizuri ni tatizo la wanafunzi au inawezekana ni tatizo la walimu wao hawakuwafundisha vizuri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule hizi zinachukua wanafunzi ambao ni cream, leo wanafunzi 114 unawafukuza? Ni kutokana na sababu hizo za watu kufukuza ndiyo Serikali ikawa hata imetoa na maelekezo kwamba wale waliofukuzwa warudi shuleni, suala la kukaririsha halina matatizo yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kutokana na changamoto hizo mimi mwenyewe binafsi nilikutana na wamiliki wa shule binafsi. Mwanzoni walikuwa wanaona kama vile Serikali imewaonea, lakini baada ya kuwapa takwimu kwa kweli na wenyewe walikiri kwamba suala hili shule moja kama hiyo Panda Hill imefukuza wanafunzi 114, Shule ya Sekondari ya St. Pius ya Dar es Salaam wanafunzi 89 kwa mwaka mmoja wanafukuzwa. Kwa hiyo, wao wenyewe shule binafsi mimi nawashukuru sana, hata na wao ni wazalendo sana, walisema Mheshimiwa Waziri, hili jambo ungetuambia sisi wenyewe, tuna chama chetu tungewashughulikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa kweli suala hili wala siyo tatizo kubwa sana ni suala tu sasa la baada ya hayo kutokea tulichokubaliana na wamiliki wa shule binafsi ni kwamba tukae kwa pamoja kwamba pamoja na nia njema ya kuhakikisha kwamba kabla mtoto hajaendelea anakuwa na viwango vizuri, lakini tuweke na utaratibu wa kulinda watoto wa wanyonge wa Kitanzania ambao wanakuwa milioni za fedha halafu mtu mmoja tu kwa mtihani ambao hakuna anayejua ameutunga kwa vigezo gani, kwa mtihani ambao hakuna anayejua ameusahihisha kwa vigezo gani, analala anaamka anawaambiwa watoto 114 kwenye shule moja waondoke. Jambo hili halikubaliki na Waheshimiwa Wabunge naomba katika hili la kufukuza kwa utaratibu huo mniunge mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna Kamati ya Majadiliano ambayo kuna wajumbe kutoka Wizara ya Elimu na wajumbe kutoka sekta binafsi ambao kwenye sekta binafsi kuna Bwana Laurent Gama wa TAPIE ambaye ni Katibu, kuna Bi. Stella Rweikiza wa TAPIE na Bwana Moses Kyando kutoka TAMONGSCO ambapo majadiliano yanakwenda vizuri. Wenyewe wamesema pia wataisaidia Serikali katika kuhakikisha hakuna shule za binafsi ambazo zinawachafua kwa sababu wanatambua kwamba samaki mmoja akioza wote wameoza. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge hili suala halina tatizo lolote na baada ya muda mfupi tutafikia mwafaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nihitimishe hoja hii kwa kulieleza Bunge lako tukufu kwamba Serikali inaheshimu na kuthamini sana mchango wa sekta binafsi katika utoaji elimu. Kwa taarifa tu ya Bunge hili, sekta binafsi kwenye elimu ni wadau wakubwa sana ambao Serikali kwa namna yoyote ile haiwezi ikawachezea au kutothamini mchango wao kwa sababu shule za msingi za binafsi zilizoko nchini ni 1,247; shule za sekondari za binafsi ni 1,192 na wanaosoma hapo ni watoto wa Kitanzania. Sasa ina maana Serikali ikinyanyasa shule binafsi inanyanyasa watoto wa Kitanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahakikishie kwamba hakuna mgogoro wowote, hakuna wivu wala chuki kwa shule binafsi. Labda tu kinachoweza kujitokeza ni mawasiliano, pengine inawezekana kuna watendaji ndani ya Wizara yangu wakiona wamiliki wa shule binafsi wanakuwa wanawapa majibu ambayo siyo mazuri. Sasa hilo ni suala la kiutendaji na naomba kama wapo watendaji wa namna hiyo niambiwe, nitawashughulikia kikweli kweli, wasituharibie ushirikiano wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo imezungumzwa ni suala la udhibiti ubora wa shule na Waheshimiwa Wabunge wengi kwa ujumla wao wameizungumza sana lakini hata na Kamati yangu wamezungumza na kumetolewa ushauri wa kuundwa chombo cha kudhibiti ubora yaani uanzishwaji wa Mamlaka ya Udhibiti wa Ubora wa Elimu katika nchi yetu. Kwanza nianze kusema kwamba napokea ushauri huu kwa heshima kubwa na niseme kwamba kama nilivyotangulia kusema katika maelezo yangu ya utangulizi, nimefaidika sana na michango ambayo Waheshimiwa Wabunge mmeitoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala hili nalipokea lakini nizungumzie jitihada ambazo kwa sasa Serikali ilikuwa imeanza kuzifanya katika kuboresha hii sekta ya udhibiti ubora wa shule. Kwanza, nimeelezea ile changamoto ya wanafunzi kuwa wengi katika shule zetu, lakini nimeeleza pia na jitihada ambazo Serikali ya Awamu ya Tano imekuwa ikifanya katika kukabiliana na changamoto hizo. Ni ukweli kwamba katika baadhi ya shule ile idadi ya ongezeko la wanafunzi halijaenda sawia na idadi ya walimu ambao wanatakiwa kuwepo shuleni. Kwa kutambua hilo, Wizara imekuwa ikiendelea kuimarisha mafunzo kazini na uhaba wa walimu wa sayansi pamoja na mkakati wa wanafunzi wale ambao walikuwa wako UDOM ambao mwaka huu kuna bunch ambayo imemaliza lakini pia hata katika bajeti yangu mwaka huu tutatenga fedha kwa ajili ya waafunzi ambao wamesoma Bachelor of Science, ile general, ili wakafanye Postgraduate Diploma in Education kuweza kuendelea kutatua changamoto za elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika udhibiti ubora wa shule, kwa kutambua umuhimu mkubwa wa ufuatiliaji na ujifunzaji kwa sababu Wadhibiti Ubora wa Shule ndiyo jicho letu, ni sawa ambavyo CAG ndio jicho la Serikali katika matumizi ya fedha za umma.

Kwa hiyo, Wizara kwanza tumebadilisha mfumo wa ukaguzi, nimeeleza katika hotuba yangu kwamba tumeandaa kiunzi cha udhibiti ubora wa shule ambacho kitaboresha usimamizi wa masuala ya elimu.

Pia tumetoa mafunzo kuanzia ngazi ya shule na Kamati za shule. Kwa mara ya kwanza tumeshirikisha pia Kamati za Shule, kwa sababu ni kweli tunaona kwamba tuwe na chombo cha kuangalia hii elimu yetu lakini niseme kwamba tuna shule za msingi 17,000, tuna shule za sekondari kama 5,500, kwa hiyo, kwa namna yoyote ile chombo ambacho kitakuwa kipo kitaifa bado kitakuwa na changamoto. Mkakati wa Wizara pia ni pamoja na kuimarisha Bodi za Shule abazo ndizo zinazowajibika katika usimamizi wa moja kwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu udhibiti ubora wa shule tunauboresha na nashukuru katika michango kuna Waheshimiwa Wabunge waliona kwamba tunajenga ofisi 50 za udhibiti ubora wa shule. Pia nimesema tumenunua magari 54, pikipiki 2,894 kwa ajili ya kuimarisha ufuatiliaji ngazi ya kata. Waheshimiwa Wabunge pikipiki hizi tutazigawa kabla hatujamaliza Bunge. Kwa hiyo, mkirudi majimboni mtapata pikipiki ili kuimarisha usimamizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tushirikiane katika kuwabana watu wasimamie elimu ipasavyo, hii ndiyo jitihada ya Serikali. Kama nilivyosema, elimu ni juhudi za Serikali, wazazi, wanafunzi, wote kwa ujumla wetu tukishikana mkono, nina uhakika kwamba elimu ya Tanzania itasimama. Niwatoe hofu kabisa wale ambao mnasema kwamba elimu ya nchi yetu iko vibaya; niwaambie elimu ya nchi yetu iko vizuri kabisa, ina afya njema na Rais wetu ana utashi, amekwishafanya mambo makubwa, kitu kikubwa ni ushirikiano ambao unatakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata suala la kuwa na mjadala wa elimu limezungumzwa sana. Niseme tu kwamba mjadala katika sekta ya elimu ni mjadala ambao utatuwezesha sisi kubaini matatizo. Niseme kwamba kuna matatizo ambayo tayari tunayafahamu, tunafahamu kwamba kuna shule ambazo zina mrundikano na ndiyo maana tumejikita katika miundombinu; tunafahamu kuna shule zina uhaba wa walimu, namshukuru Mheshimiwa Waziri wa Utumishi ameahidi kwamba ataendelea kulitatua; tunafahamu kwamba kuna shule ambazo watoto wanatembea umbali mrefu, ndiyo maana tumekuwa tunajenga mabweni.

Kwa hiyo, kipaumbele cha Serikali kwa sasa ilikuwa ni kujikita katika kutatua changamoto ambazo tayari tunazifahamu lakini hii haizuii wadau ambao wana mapenzi mema na nchi yetu kuendelea kuibua changamoto nyingine na kuipa changamoto Serikali yao ili sambamba na changamoto ambazo Serikali imeamua inafanyia kazi, kama zipo nyingine zitafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mjadala ji suala ambalo lina afya kwa sababu linalenga katika kuibua changamoto zilizopo ili Serikali, Serikali hii sikivu iweze kuzifanyia kazi na tumekuwa tukishuhudia mijadala kwa mfano tulikuwa na Kigoda cha Mwalimu kilikuwa kinazungumzia masuala ya uporaji wa rushwa na rasilimali za nchi yetu; tumeshuhudia Kibweta cha Mwalimu ambacho kilikuwa kinazungumzia kuelekea uchumi wa kati. Kwa hiyo, tumekuwa na mijadala mbalimbali ambayo ikitokea katika nchi na hivyo basi mjadala kwenye elimu ni suala ambalo niseme kama Waziri mwenye dhamana linapokelewa kwa mikono miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshapigiwa kengele na nisingependa kupigiwa kengele ya pili kama nilivyosema michango ya Waheshimiwa Wabunge ilikuwa ni mingi ni mizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie na moja tu ambalo nalo lilizungumzwa sana kuhusiana na Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 na kwamba hakuna mpango mkakati wa sera na kwamba tunatumia sheria ya mwaka 1978, nikiri kwamba kweli ile sera yetu ya elimu bado haijawekewa zile sheria na niseme kwamba tayari ile sera ya elimu kwa namna ambavyo iliandikwa kwa bahati mbaya iliandikwa katika namna ambayo inakuwa ni nyaraka au document ambayo haiishi, wanasema a living document kwamba mle ndani kwa mfano imesema Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa sasa hivi haipo mle ndani inazungumzia Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ile pale Wizara sasa hivi haipo na mambo mengine nimetoa kwa uchache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaona kwamba ni vema hata hiyo uandishi wa sera yetu uandikwe katika namna ambayo itakuwa ni document ambayo inaweza ikakaa miaka mingi bila kuhitaji kubadilisha badilisha na Mheshimiwa Mbatia naona ameishilikia, lakini tu kwa uchache ni kwamba hii suala la sera ya elimu pia kuna suala kwa mfano na umri wa kwenda shuleni kutoka miaka saba kwenda miaka mitano ilibadilishwa kabla ya hata kubadilisha sheria kwa sababu miaka saba umri wa kwenda shuleni umewekwa ndani ya sheria. Kwa hiyo, tayari hata kuna mkingano katika sheria zilizopo. Niombe katika hii sera ya elimu tunakusudia kufanya mapitio vile vitu ambavyo vinaukinzani tuvibadilishe kwanza kabla hatujaenda kwenye kutengeneza sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maelezo hayo na kwa sababu kwamba muda wa kwenda shuleni miaka saba umetajwa kwenye sheria ya elimu na katika Bunge lako tukufu hamjafanya mapitio ya marekebisho ya Sheria ya Elimu miaka ya elimu ya msingi itaendele kuwa miaka saba hadi pale marekebisho ya sheria yatakapofanyika. Kwa hiyo, suala la kusema kwamba kutakuwa na wanafunzi ambao wanamaliza wengine darasa la sita, wengine ni darasa la saba kwa sasa halipo mpaka hii sheria ambayo tunaitumia itakapofanyiwa marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo na ufafanuzi huu wa hoja naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge ambao sikuweza kupata muda wa kujibu hoja zao kwamba hoja zote tutazijibu kwa maandishi na baada ya ufafanuzi wa hoja mbalimbali zilizotolewa ambazo nimeweza kuzielezea pamoja na zile ambazo ninazileta kwa maandishi, sasa kwa unyenyekevu mkubwa kabisa ninawaomba Waheshimiwa Wabunge wote tutakapokaa kama Kamati naomba wote kwa pamoja muunge mkono hoja yangu mnipitishie Makadirio ya Mapato na Matumizi ili sasa haya ambayo nimewahaidi niweze kwenda kutekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo naomba kutoa hoja.