Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama hapa na kipekee kabisa niipongeze Serikali, nimpongeze Waziri wa Maji kwa jitihada kubwa anazofanya na tumeshuhudia ni kwa jinsi gani ambavyo amekuwa mstari wa mbele kutembelea maeneo mbalimbali kushughulikia tatizo la maji. Pamoja na yote haya maji ni shida sana na tunafahamu kwamba maji ni uhai na maji ni kwa wote, uwe mwenye ulemavu, usiye na ulemavu kila mmoja anahitaji maji.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu mwaka jana alikuja kuzindua mradi wa maji katika Kata ya Nduruma, Vijiji vya Maroroi, Mlangarini pamoja na vijiji vingine vya jirani, tunashukuru sana kwa hili kwa sababu ndani ya miaka 50 hatukuwa na maji ya bomba zaidi ya maji ya mito ambayo tulikuwa tumeyazoea, kwa hili naishukuru sana Serikali.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yote tunafahamu Mkoa wa Arusha tumejaaliwa Mlima Meru na katika huu Mlima Meru baadhi ya maeneo wanapata maji lakini maeneo mengine tunafahamu kama katika Jimbo la Longido, Jimbo la Ngorongoro kote huko maji ni shida na wanaopata shida kubwa ya maji ni akina mama kwa sababu wao ndiyo wachotaji wakubwa wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekti, ninaomba nizungumzie shida kubwa iliyopo katika Hamashauri ya Arusha DC ambapo tuna tatizo kubwa la madini ya fluoride yanayowaathiri wananchi kwa kiasi kikubwa. Inasikitisha sana kwa sababu watoto wanapinda miguu, akina mama wanapinda migongo na hata hao watoto ukiangalia mahudhurio yao shuleni siyo mazuri kwa sababu maji yenye madini ya fluoride yamewaathiri kwa kiasi kukubwa sana. Eneo kubwa ambalo limeathirika na maji ni katika Kata ya Oldonyosambu pamoja na Oldonyowasi ambako huku kuna athari kubwa sana ya madini haya ya fluoride, maji yanapatikana kwa kiwango kidogo lakini hata hayo yanayopatikana kwa kiwango kidogo bado ni shida sana.

Mheshimiwa mwenyekiti, ulemavu unaepukika na ulemavu huu tunafahamu upo ulemavu wa kuzaliwa, upo ulemavu wa ajali na changamoto nyingine lakini ulemavu huu unaosababishwa na maji yenye madini ya fluoride haukubaliki kwa sababu tuna uwezo wa kupeleka maji na kuwaondolea shida akina mama na watoto ambao wanapata athari kubwa, wanapinda miguu na wanapata athari pia hata kwenye kusoma inakuwa ni shida. Kwa bahati nzuri, Mheshimiwa Waziri nilikuonesha video ambayo inaonesha ni kwa jinsi gani watoto wameathirika na maji haya yenye madini yenye fluoride na kwako wewe pia ilikuwa ni jambo la kushangaza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwamba umeahidi lakini kwa kweli tunahitaji jitihada za haraka katika kuhakikisha kwamba tunawasaidia wakazi hawa katika hizi Kata za Oldonyosambu pamoja na Kata ya Oldonyowasi ili basi tuondoe tatizo hili la ulemavu unaotokana na maji yenye madini ya fluoride.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tatizo hili ni kubwa na kwa kuwa sasa katika Wilaya ya Longido chanzo kingine cha maji cha Mto Simba kutoka Wilaya ya Siha, basi tunaomba hivi sasa kwamba chanzo cha maji ambacho ni cha Engutoto na tunafahamu kabisa kwamba kulikuwa kuna mradi unaofadhiliwa na DFID kwa kushirikiana na Water Aid Tanzania, tunaomba katika Halmashauri hii ya Arusha kile chanzo cha maji ambacho awali kilikuwa kipeleke maji katika Jimbo la Longido na hatimaye chanzo hiki tumekiacha, tunaomba sasa chanzo hiki kiweze kupeleka maji katika Kata hii ya Oldonyosambu pamoja na Kata ya Oldonyowasi ili tuondoe tatizo hili la madini ya fluoride. Tukipeleka chanzo hiki cha maji tutasaidia vijiji vya Losinoni ambavyo hali yake ni mbaya sana, tutasaidia vijiji vingine ambavyo ni vya Lengijave lakini siyo hiki tu kuna kijiji cha Lemanda ambacho kimeathirika kwa kiasi kikubwa sana.

Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri ninakuomba sana ili basi uweze kuhakikisha kwamba tunapeleka fedha, tunakishughulikia chanzo hiki cha maji ili tuweze kutatua madini haya ya fluoride. Kuna baadhi ya wenzetu wakati mwingine hata kucheka inakuwa ni shida kwasababu ya meno yameathirika na maji. Mheshimiwa Waziri, hatupendi kwahiyo tunaomba sana mtusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunafahamu katika Mkoa wa Arusha, tumesomeshwa wengine na bustani kwa sababu tulikuwa na kilimo cha umwagiliaji kwa miaka yote kutokana na maji yanayotoka katika Mlima Meru. Hivi sasa hatuwezi tena kulima kwa sababu wamiliki wa mashamba makubwa ya maua sasa hivi wanayahodhi yale maji yote, matokeo yake wananchi ambao walitegemea kilimo kutokana na kilimo hiki cha umwagiliaji sasa hivi hawawezi tena kulima. Tunawapenda wawekezaji, tunawahitaji wawekezaji, lakini wawekezaji hawa wasitufikishe hapo wananchi wetu wanapata shida. Kwa hiyo, ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri ili uweze kushughulikia na kupitia basi kwa sababu wengine wamehodhi maji na wanasema kwamba wana hati miliki ya kuhodhi maji hayo kwa miaka 100 yaani kwa maana 99.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania wetu wanaangamia, ndugu zangu nimesoma mimi kwa kulima bustani, hivi sasa imekuwa ni shida kwa hiyo tunaomba sana mashamba ya maua yaliyopo katika eneo la vijiji vya Chekereni, lakini pia njiapanda ukienda Mlangarini, mashamba ya maua yale wamiliki wote wamehodhi maji, tunaomba tunayahitaji haya maji ili wananchi wetu waweze kurudi na kulima kilimo cha umwagiliaji tofauti na sasa ambako tunasubiri mvua mpaka mvua na siku hizi kumekuwa na mabadiliko ya tabianchi maji haya yanakuwa ni shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana, hiki ni kilio cha wananchi cha muda mrefu, tunawahitaji wawekezaji kama nilivyosema, lakini wawekezaji hawa wasihodhi maji yote, kwa hiyo ninaomba sana Serikali ipitie haya... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)