Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hoja iliyo mbele yetu. Kama ilivyo ada watu wamezoea kuwasifia na kuwapongeza Mawaziri mimi leo naomba nisiwapongeze na sababu ya kutowapongeza wanaijua. Siyo kwamba nawachukia ila sababu za kuacha kuwapongeza Mawaziri na watendaji wote wanazijua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na sera ya kumtua mama ndoo kichwani, hivi takwimu tunazopewa huwa zinalenga nini? Kwa sababu takwimu hizi haziendani na uhalisia na ninyi Wabunge humu ndani ni mashahidi siku yoyote pakitokea swali la maji Bunge zima linalipuka kuonesha kwamba hali ya maji nchini ni mbaya. Hata hivyo, ukisoma vitabu, mimi hapa nimesoma nimeambiwa kwenye upande wa vijiji watu milioni 36 wanaopata maji ni milioni 30.9 asilimia 85; lakini bado Waziri akaendelea kusema lakini upatikaji wa maji katika vijiji ni asilimia 58, sababu aliyoitoa ni usimamizi mbovu wa miradi ya maji. Kama kweli tuna sera ya kumtua ndoo kichwani ifikapo mwaka 2020 na huku kutokupeleka fedha kwenye miradi ya maji mbona hizi takwimu zinakwenda tofauti tofauti? Unawezaje kutekeleza hii sera wakati huo huo Serikali haipeleki fedha kwenye miradi ya maendeleo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nashindwa kuelewa hizi takwimu na hizi sera mnataka kumfurahisha nani kwa sababu hazina uhalisia. Kama kwenye miradi ya maji hampeleki fedha halafu mnasema ifikapo mwaka 2020 mnamtua mama ndoo kichwani. Mimi sielewi labda Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha anifafanulie zaidi sera hii maana yake ni nini lakini kama kwa namna hii ya upelekaji wa fedha kwenye Halmashauri zetu au kwenye miradi mbalimbali wa asilimia 22 halafu mnasema ifikapo 2020 mnamtua mama ndoo kichwani mimi siwezi kuelewa na wala sikubaliani na hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba nijielekeze kwenye miradi ya umwagiliaji. Nataka niseme Mheshimiwa Waziri kwenye hii miradi ya umwagiliaji tumefeli. Hakuna Mbunge hapa atasimama atasifia kwamba kweli halmashauri zake kuna miradi ya umwagiliaji imefanya vizuri sana, hakuna. Kwanza mimi naomba niwashauri hebu ondoeni kwanza utata nani msimamizi wa hii miradi ya umwagiliaji. Haiwezekani mradi wa umwagilaji uko Liwale kilometa 400 kutoka Mtwara halafu wasimamizi wa mradi eti wa Kanda watoke Mtwara waisimamie miradi Liwale halafu iende sawasawa, haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu mradi tangu unaanza inatakiwa yule mtaalam awe pale, at least kila baada ya siku mbili au tatu hata kama wiki atoke Mtwara aende Liwale akakague mradi, atakwenda kule mwezi mmoja umepita, wakandarasi wamefanya wanavyotaka halafu miradi inafeli na pesa zinapotea, mnasema kwamba mvua ilikuwa nyingi miradi imeharibika, si sawasawa. Hebu hii miradi mhakikishe inasimamiwa na Halmashauri, kama yule Mhandisi wa Maji yupo Wilayani tumpe huu mradi asimamie, tuone hii miradi ya umwagiliaji itafeli kama ilivyofeli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila nikisimama hapa naongelea Mradi wa Ngongowele. Mradi huu umeshaondoka na shilingi milioni 770 lakini umekufa. Nimeshaomba mara nyingi hapa ule mradi kama itawezekana, nasikia mwaka huu JICA wamekubali kuufadhili basi mtupe sisi halmashauri tuusimamie kwa sababu hawa watu wa Kanda wako mbali sana hata wawe na weledi wa namna gani, kwa shida ya usafiri tuliyonayo na barabara mabovu hizi, atoke Mtwara kila wiki aende Liwale kusimamia mradi wa umwagiliaji si sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze kwenye kitabu cha Mheshimiwa Waziri amesema kuna mipango ya ushirikishwaji wa ulinzi wa rasilimali maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti,nimeona maelezo tu ni namna gani ushirikishwaji huu upo haieleweki. Mpaka sasa hivi hatujaambiwa wameunda vikosi kazi kwenye vijiji gani, kwenye mabwawa au mito. Huu ushirikishwaji mnaosema hapa kwamba mna mpango wa ushirikishwaji wa ulinzi wa rasilimali maji, kwenye vitabu nimeuona, lakini kwenye uhalisia hatujauona kwamba ni mikakati gani imechukuliwa na Serikali katika kulinda hii miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona tu kweye karatasi imeandikwa lakini sijasikia kumeundwa task force ya namna gani, kijiji gani au halmashauri gani katika kutimiza hili lengo la ushirikishwaji. Kwa sababu haiwezekani Wizara ninyi mnaweza kulinda rasilimali maji bila kuwashirikisha wananchi, ni lazima muwashirikishe wananchi ili miradi hii iweze kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukipitia hii miradi ya maji hata ukiangalia ile miradi ya maji vijijini, fedha nyingi ni za wafadhili, fedha ya Serikali hapa hatuioni hata kama ipo ni kidogo sana na ndiyo hiyo ambayo haiji. Mheshimiwa Waziri nimeshamfuata mara nyingi ananiambia kinachotakiwa pale ni Mhandisi kuleta certificate ya miradi wao watalipa. Nataka niseme kwamba kwenye Halmashauri yangu certificate zipo nyingi kwenye Wizara yako lakini sijapata fedha. Hata bajeti ya mwaka jana nilivitaja vijiji ambavyo havina maji mpaka leo, vya Nangano, Kipelele, Kikuyungu, Naujombo, Kiangara, Mikunya, Kipule, Makata, Mkutano, Mlembwe na miradi ya maji ipo. Sasa sijaelewa hizo certificate ambazo Wizara inadai ni za namna gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nataka niongelee vile vijiji ambavyo tayari vina maji. Vile vijiji ambavyo tayari vina mashine za maji tuna tatizo kubwa sana na mashine hizi zinazoendeshwa na dizeli. Mashine zinazoendeshwa na dizeli kwenye vijiji vyetu tunashindwa kumudu gharama ya maji kwa sababu unakuta ndoo inauzwa kuanzia shilingi 100 mpaka shilingi 200. Kwa mtu wa kijijini yuko tayari aende kilomita tano afuate maji kuliko kutoa shilingi 200 kununua ndoo ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano halisi ni katika Kijiji cha Mpigamiti ambacho kina mradi wa maji sasa hivi una takribani zaidi ya miaka tano lakini pale kijijini wanakosa fedha za kuendesha mradi ule. Kwa sababu mwisho wa siku wanakosa fedha za kununua dizeli kwa hiyo watu hawapati maji. Ushauri wangu ingewezekana kabisa miradi hii wakaanza kuipeleka kwenye solar, miradi ambayo inaendeshwa kwa mitambo ya solar inafanya vizuri sana.

Namshauri Mheshimiwa Waziri hii miradi ya vijiji iliyobaki badala ya kuielekeza kwenye mafuta tuielekeze itumie solar, hapo ndiyo itaweza kufanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii sera ya kumtua mama ndoo kichwani naomba niirudie, hebu mtuletee time frame, mtuletee takwimu, mpaka leo hii mmeshafikia asilimia ngapi ya utekelezaji ili tuweze kuona kwamba je, itakapofika mwaka 2020 kweli mtafikia lengo? Hapa mnaleta tu takwimu za ujanja ujanja, hatuletewi ni asilimia ngapi kwamba mpaka sasa hivi mmefika asilimia ngapi, hatujui.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitaka kujua nchi hii tuna tatizo kubwa la maji, leo hii nchi hii kuzindua kisima cha maji anaenda Rais. Hiki kitabu unakiona yaani Makamu wa Rais anamtwisha mama ndoo, anazindua kisima cha maji, hizi kazi wanafanya hata Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikichimba kisima pale kijijini kwetu Diwani anaenda kukizindua, lakini leo tunamtuma Rais akazindue kisima cha maji, muone jinsi gani tulivyo mbali. Tuko mbali na uhalisia ndiyo maana inakuwa hivyo yaani inaonekana ni jambo la ajabu mama kutua maji mpaka Rais, Waziri Mkuu, Waziri wanaenda, hizi ni kazi za Madiwani. Tatizo la maji ni kubwa kuliko hivyo mnavyofikiria.