Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Musa Rashid Ntimizi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. MUSA R. NTIMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya Maji ambayo ni Wizara muhimu sana katika maisha yetu na ya wananchi wetu, hasa sisi watu wa vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza na mimi nichukue nafasi hii nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, kaka yangu Injinia Kamwele, mdogo wangu Naibu Waziri na Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri wanayoifanya. Pamoja na changamoto nyingi za maji tulizonazo katika maeneo yetu na nchi yetu lakini kwa kweli wanajitahidi kutimiza wajibu wao. Pamoja na bejeti ndogo wanayopata lakini maeneo mengi wanajitahidi kufika na kutatua kero zilizopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo naomba nitoe shukrani kwa Mheshimiwa Waziri na watendaji wake, bajeti zilizopita nilikuwa nazungumzia sana shida ya maji katika Jimbo langu la Igalula, ukizingatia mradi mkubwa wa maji wa Ziwa Viktoria unaokuja katika Mkoa wetu wa Tabora, Jimbo langu la Igalula lilikuwa halimo katika maeneo yanayopata maji kutoka Ziwa Victoria. Nilijaribu kuomba mara mbili, tatu kwamba, kama kuna uwezekano tuone uwezekano wa kupata maji mbadala wakati maji ya Ziwa Viktoria tunategemea yatakuja hapo baadae. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sasa miradi imeanza kuja jimboni kwangu, mradi wa Igalula tumepata zaidi ya shilingi milioni 380, tumekarabati bwawa kubwa la maji lilipo pale Igalula na sasa tunaelekea kupata maji ya uhakika katika Jimbo letu la Igalula hasa katika Kata ya Igalula. Pia upembuzi yakinifu unaendelea kufanyika katika mradi wa Kata ya Nsololo na Goweko, wataalam wameshakwenda, nina hakika maji yatapatikana muda si mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za Loya na Tura tuna bwawa kubwa sana kuliko Bwawa la Kazima lililo katika Manispaa ya Tabora Serikali kupitia Wizara ya Maji imekubali sasa kuuwekea miundombinu mradi ule mkubwa wa maji wa Tura, nina hakika sasa wananchi wangu wa Jimbo la Igalula tutapunguza kero kubwa ya maji tuliyokuwanayo, nashukuru kwa kazi kubwa inayofanyika.

Naomba pia nimpongeze Mkurugenzi Mkuu wa TRL kwa kukubali lile bwawa walilochimba TRL liweze kutumiwa na wananchi wangu wa Tura kwa kuwekewa miundombinu na Wizara baada ya Mheshimiwa Waziri wa Maji kukubali kuweka miundombinu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na haya yote niliyoyaeleza, nilitaka nitoe ushauri kidogo ili tuendelee kutatua changamoto ya maji, najua hatuwezi kumaliza matatizo ya maji kwa mara moja, lakini kuna namna ambayo tunaweza tukafanya tukaendelea kupunguza matatizo ya maji katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kusema maeneo yangu ya Jimbo la Igalula tumejaribu kuchimba visima vingi virefu na vifupi, upatikanaji wa maji umekuwa ni mdogo sana na siyo katika Jimbo la Igalula tu maeneo mengi ya Mkoa wetu wa Tabora visima vinachimbwa lakini baada ya mwezi mmoja visima hivyo vinakuwa havitoi maji. Ushauri wangu ni kwamba Serikali sasa iwekeze kwenye uchimbaji na utegaji wa mabwawa ambayo mara nyingi yanasaidia sana upatikanaji wa maji ya uhakika. Zile fedha nyingi tunazozipoteza katika kuchimba visima nadhani sasa Serikali ijipange na mradi mkubwa wa kuangalia maeneo yanayoweza kuchimbwa mabwawa yakachimbwa mabwawa na yakawekewa miundombinu inasaidia sana kupunguza kero ya maji kuliko hizi fedha zinazoendelea kupotea katika visima tunavyovijenga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mimi kwangu Igalula tuna bwawa lilichimbwa mwaka 1970, mwaka huu zimetolewa shilingi milioni 380 tumelirekebisha lile bwawa, tumeliwekea miundombinu, watu takribani 20,000 wanapata maji kupitia mradi ule wa bwawa lakini tungechimba kisima cha shilingi milioni 40 kisingeweza kutoa maji ya kutosha watu takribani 40,000 wa Kata ya Igalula. Kwa hiyo, Wizara ije na mpango mahsusi katika maeneo yetu nchi nzima, hata kama tutapata kidogo kidogo, lakini tuanze kufikiria sasa kuchimba na kutega mabwawa ili wananchi wetu waweze kupata maji ya uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la miradi ya umwagiliaji. Baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wamesema hapa, na mimi nataka miradi hii haijapewa umuhimu wa kutosha. Naomba Wizara iangalie umuhimu wa miradi hii ya umwagiliaji. Miradi hii ya umwagiliaji ina faida zake, kwanza wananchi wetu wanapata maji ya uhakika, lakini wananchi wetu watasaidiwa upatikanaji wa chakula; wananchi wetu watapata kipato kutokana na mazao yatakayopatikana katika ule mradi wa umwagiliaji, lakini pia halmashauri zetu zitakusanya kodi kwa sababu uzalishaji utakuwa mkubwa, watapata kodi ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine wananchi wetu wataondokana na umaskini. Wanapokuwa na uhakika wa chakula maana yake wananchi wetu hawatakuwa ombaomba na wananchi wetu wataweza kusomesha watoto wao vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii ya umwagiliaji iwekewe fedha na sio itengewe tu fedha, fedha ziende kwenye miradi hii. Tusipofanya hivi wananchi wetu watakosa faida kwa sababu miradi mingi ya umwagiliaji inatengewa fedha, inafanyiwa feasibility study, inafanyiwa kila kitu, lakini mwisho wa siku haitengewi fedha na kwenda kutekelezwa, hili ni jambo la msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na umuhimu wa maji, kuna miradi wamezungumza Waheshimiwa Wabunge haitekelezeki kutokana na kutopelekwa fedha. Niiombe Wizara ijipange miradi yote ambayo ilitengewa fedha na haijakamilika ipelekewe fedha ikakamilike nchi nzima. Tunapoteza fedha za walipa kodi na mwisho wa siku wananchi wanakuwa hawatuelewi, shida ya maji inaendelea kuwepo na fedha zimepelekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna maeneo mkandarasi amekimbia site, aidha, kwa kutolipwa fedha au mwingine ameshindwa kuiendeleza ile miradi. Wale ambao wameshalipwa fedha, kama walivyosema wenzangu, Wizara lazima iwachukulie hatua hawa wakandarasi, aidha kuwashitaki au kuhakikisha wanarudi site kuikamilisha miradi iliyoanzishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho Wizara hii imepumulia zile shilingi 50 tulizowawekea kwenye tozo ya petroli, Mawaziri wanajua bila fedha hii miradi yote ambayo imetekelezwa isingeweza kutekelezeka. Kwa hiyo, kwa sababu tumeweza kupumulia shilingi 50 na miradi mingi imeonekana katika katika maeneo yetu, wazo langu nataka Bunge hili liungane tuhakikishe safari hii kieleweke, shilingi 50 lazima iongezwe kwenye bei ya petroli na fedha hiyo iende kwenye miradi ya maji. Kwa sababu sisi ni waathirika hasa sisi tunaotoka vijijini, safari hii hakitaeleweka hapa kama shilingi 50 itakataliwa kuongezwa, tunataka ifike shilingi 100. Kama kwa shilingi 50 tumeweza kufanya miradi mikubwa mingi kiasi hiki na sisi tuliahidi kumtua mama ndoo kichwani kijijini, miaka inazidi kwisha, tunataka shilingi 50 iongezwe ili twende tukatekeleze miradi iliyopo katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa kuishukuru sana Wizara hii. Changamoto wanazokutana nazo ni kwa sababu ya shida kubwa ya maji tuliyonayo katika maeneo yetu. Tunaomba wasikate tama, waendelee kufanya kazi, sisi tuko pamoja nao na Mungu atawabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Ahsante sana.