Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili basi na mimi nichangie katika Wizara hii ya Maji na Umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia 22 ya bajeti ya maendeleo ambayo imekwishatolewa mpaka sasa ni kielelezo tosha kwamba Serikali ya CCM maji siyo kipaumbele chao cha kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya CCM ina kipaumbele cha mipango tu lakini siyo utekelezaji wa mipango hiyo na ndiyo maana mpaka sasa hivi sehemu kubwa ya Watanzania wameshindwa kupata huduma ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niseme kwamba bado Serikali haijafanikiwa kuondoa tatizo la maji kwa wananchi wake kwani wananchi wana shida kubwa ya maji. Sina shida na utendaji wa Waziri na Naibu wake wanajitahidi na kama wangekuwa wamewezeshwa basi mambo yangeweza kwenda sawasawa, lakini tatizo hilo lote kubwa linatokana na Wizara ya Fedha ambayo inashindwa kutoa pesa kwa wakati ili Waziri na Naibu Waziri waweze kutekeleza miradi ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya CCM imekuwa ikijigamba kwamba inakusanya pesa zaidi ya mipango yake, lakini cha kushangaza utekelezaji wa miradi ya maendeleo na maendeleo muhimu kama ya maji inashindwa kutekelezwa, tunashindwa kuelewa. Kama mnakusanya pesa za kutosha kwa nini miradi ya maji ikwame? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali bado haijaliona tatizo hili, sera inaelekeza kumtua mama ndoo kichwani, lakini bado akimama wa vijijini wanapata maji kwa kuyabeba kichwani. Serikali iliangalie hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni suala zima la Azimio la Bunge lako tukufu. Kamati yangu ya Kudumu ya Usimamizi wa Serikali za Mitaa tulipokuwa tunawasilisha taarifa tulitoa angalizo na Bunge likaazimia kuundwe Kamati Teule ya Bunge kwa ajili ya kuangalia utekelezaji wa miradi ya maji. Lile lilikuwa ni Azimio la Bunge na Bunge lilitaka Kiti kihakikishe kinaunda Kamati Teule ya Maji kuangalia utekelezaji wa miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati yangu imefanya ukaguzi wa miradi ya maendeleo tumegundua kuna tatizo kubwa la utekelezaji wa miradi ya maji na ndiyo maana tukaja na pendekezo lile ambalo sasa limeshakuwa Azimio la Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi kukikumbusha Kiti, tunaomba Kamati Teule iundwe ili utekelezakji wa miradi ya maendeleo uweze kuangaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wachangiaji wengi wamejaribu kueleza tatizo la utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya maji ni shamba la bibi. Naomba hiyo Kamati iundwe haraka ili Bunge liweze kuangalia tatizo hili na kutafuta suluhu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye matumizi ya maji ya Mto Rufiji. Mito yote mikubwa tayari ina miradi mikubwa ya maji, lakini mpaka hivi leo Mto Rufiji maji yake yanamwagika bure tu baharini. Maji ya Mto Rufiji mamba na boko wanaogelea tu, hayajakuwa na faida za moja kwa moja kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa za kijiolojia zinaelekeza kwamba ukanda wote wa Pwani ukichimba maji utapata maji ya chumvi. Kwa hiyo, ili basi kuwezesha kutoa huduma ya maji kwa wananchi wa Ukanda wa Pwani, maji ya Mto Rufiji yatumike. Tunaomba Serikali ianzishe mradi mkubwa wa maji ili basi wananchi wa Ikwiriri, Muhoro, Somanga, Njianne, Miteja, Kilwa Kipatimu, Kibata wapate maji, tunaomba sana katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna suala zima la miradi ya maji katika Jimbo langu la Kilwa Kaskazini. Mpaka hivi ninavyozungumza zipo kata ambazo bado hazijapata miradi ya maji. Kuna Kata za Namayuni, Chumo, Kibata, Kinjumbi, Somanga na vijiji vya Mkarango, Mtondo wa Kimwaga na Ndembo katika Kata ya Kipatimu havina mradi wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni wenzetu wa DDCA walikuja na wakafanya utafiti kwa baadhi ya vijiji lakini wakashindwa kufika katika Kijiji vya Nandembo na Kibata. Niwaombe wafike katika vijiji vile kwa sababu wananchi katika maeneo hayo bado wana matatizo makubwa ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala zima la huduma ya maji katika Hospitali ya Wilaya pale Kilwa Kivinje, bado kuna matatizo makubwa. Tuiombe Serikali ihakikishe hospitali ile inapatiwa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna suala zima la Wakala wa Maji Vijijini na Mijini, limezungumzwa na wachangiaji wengi na Serikali pia ilishaelekeza kwamba ina mpango huo, tunaomba hili jambo lianze kwa haraka. Angalizo ni kwamba, wakati jambo hili litakapoanza Madiwani katika halmashauri zetu wapewe elimu ya kutosha namna gani wakala hii itakavyokwenda kufanya kazi ili kuepusha mgongano ambao unaweza ukatokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni suala zima la umwagiliaji. Katika Jimbo langu la Kilwa Kaskazini ambalo lina utajiri wa mabonde hakuna mradi hata mmoja wa umwagiliaji ambao unatekelezwa. Kwa mfano, tuna Mabonde ya Ngamwana, Marendego, Nambacho, Nalulo, Liomanga, hayo ni mabonde ambayo yanatiririsha maji wakati wote lakini hakuna project ya umwagiliaji hata moja. Niiombe Serikali iangalie eneo hilo na sisi tupate miradi ya umwagiliaji ili basi wananchi wetu waweze kujiendeleza kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo mnafahamu eneo la Kilwa na Lindi kwa ujumla wake sisi tumekuwa wapokeaji wa wafugaji. Kuna maelfu ya mifugo yapo katika maeneo yetu lakini mpaka sasa Serikali haijafanikiwa kujenga mabwawa kwa ajili ya kunywesha mifugo hiyo. Kwa hiyo, kunakuwa na mgongano mkubwa kati ya wenyeji pamoja na wafugaji kugombea maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuiombe Serikali ihakikishe maeneo yale yanajengwa mabwawa ya maji ili kuwezesha kunywesha ile mifugo ili tuondokane na migongano isiyokuwa na sababu kati yetu na wafugaji. Tunawapenda wafugaji lakini miundombinu haijaandaliwa. Kinachotokea sasa hivi ni migongano ya kugombea maji. Naomba sana Serikali iliangalie hilo kwa sababu ni jambo muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mradi wa Mingumbi - Miteja ambao uligharimu karibu shilingi 4,750,000,000 umekamilika lakini mara tu baada ya kukamilika haufanyi kazi na haufanyi kazi kwa sababu vifaa vilivyotumika pale ni kama vifaa fake, mabomba yanapasuka hovyo hovyo, ule mradi ni kama mfu ndani ya muda mfupi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo lingine ni kwamba kuna hizi Mamlaka za Watumiaji wa Maji bado hazijapewa elimu ya kutosha kuona ni namna gani zinaweza kuhakikisha kwamba wananchi wanapata huduma hii ya maji. Naomba suala hilo liangaliwe…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)