Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Engineer Isack Kamwelwe ambaye kwa upendo mkubwa aliweza kufanya ziara ya kikazi Mkoani Geita na hatimaye alifika Wilayani Mbogwe ambako alitembelea Mradi wa Maji wa Mji wa Masumbwe na kutembelea Makao Makuu ya Wilaya ya Mbogwe eneo la Kasosobe ambako alielezwa juu ya uhaba wa maji ulivyo mkubwa kiasi kwamba kila mahali panapochimbwa visima virefu vya maji, maji yamekuwa hayapatikani na matokeo yake ni upotevu wa nguvu, pesa na muda mrefu bila kupata maji ya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi letu la muda mrefu limekuwa ni kuiomba Wizara kutusaidia kupatikana kwa maji toka Ziwa Victoria, maji ambayo tayari yamefikishwa katika Wilaya jirani ya Kahama na Mheshimiwa Waziri kwa uungwana wake aliahidi kulifanyia kazi ombi hili muhimu. Sisi wananchi wa Wilaya ya Mbogwe tunayo matumaini makubwa na Waziri katika kuhakikisha kwamba tunapata maji ya uhakika toka katika chanzo cha KASHWASA. Wananchi wa Wilaya ya Mbogwe hatuna msaada mwingine isipokuwa kwa Waziri na Serikali yetu, tunaomba msaada.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mhandisi wa Maji wa Wilaya ya Mbogwe amewasilisha maombi ya fedha kwa ajili ya kuomba pesa kwa ajili ya kuunganisha umeme katika vyanzo vya maji vya visima virefu katika vijiji vya Bulugala, Lulembela, Shenda na Masumbwe. Imani yetu ni kwamba fedha zitatolewa kwa wakati ili Shirika la Umeme nchini liweze kufunga umeme katika vyanzo hivi vya maji ambavyo vinatumia mashine zinazotumia dizeli, matokeo yake ni gharama kubwa za uendeshaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi mingine ya uchimbaji wa visima katika maeneo ya Luhala, Kabanga, Ilolangula na Iponya iko mbioni kukamilishwa. Tunaiomba Serikali itoe fedha kwa wakati ili vyanzo hivi vya maji katika visima hivi vikamilike na kupunguza kadhia ya uhaba wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho naomba Wizara itusaidie wananchi wa Wilaya ya Mbogwe kupatiwa wataalam na vitendea kazi hasa gari.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja.