Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii lakini la pili nimshukuru sana Rais wangu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuniamini. Kwa kuniamini mimi maana yake ametuamini sisi vijana tuweze kumsaidia. Nataka nimuhakikishie Rais wangu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuniamini kwamba kama kijana naweza kumsaidia katika Wizara hii Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Rais wangu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuniamini kama kijana niweze kumsaidia katika Wizara hii ya Maji. Nataka nimuakinishe Rais wangu Dkt. John Pombe Magufuli kama kijana na kwa niaba ya vijana wengine wote na Waheshimiwa Wabunge sitokuwa kikwazo katika kuhakikisha Watanzania wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii pia kumshukuru sana Makamu wa Rais na Waziri Mkuu kwa ushirikiano wanaoutupa Wizara yetu ya Maji. Kwa namna ya kipekee nimshukuru mzee wangu Isack Kamwelwe kwa ushirikiano anaotupa sisi vijana katika wizara ile, nataka nimwambie waziri wangu ni Waziri jembe, na mimi kama kijana nitahakikisha namsaidia Waziri wangu katika kuhakikisha mipango mizuri inatekelezeka ili Watanzania wapate maji safi na salama na yenye kuwatosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kumshukuru sana Katibu wangu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara ya Maji. Tumejipanga na tuna nia ya dhati katika kuhakikisha tunaenda kumtua mwana mama ndoo kichwani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sikumshukuru mama yangu mzazi, leo nipo naye kwa mafundisho aliyonifundisha mimi pamoja na mzee wangu kufariki na shughuli zake ndogo ndogo za biashara ya mama ntilie, lakini kwa kuamua kunisomesha leo nimesimama hapa kama Naibu Waziri wa Maji na Mkemia. Mama yangu ahsante sana na Mwenyezi Mungu anasema unapaswa kushukuru kwa kila jambo, ahsanteni sana mwenyezi mungu awabariki sana. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda mchache niliokuwa nao naomba sasa nifafanue baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge kwa michango mizuri waliowasilisha katika Wizara yetu, ni michango yenye afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia maji ni rasilimali muhimu na maji hayana itikadi, hayana rangi, hayana dini na wala maji hayana mbadala, si kama wali ukikosa wali utakula ugali au utakula makande. Ukikosa maji tunaingia kwenye matatizo makubwa, hasa katika maradhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii sasa kujielekeza kujibu maswali na hoja za Waheshimiwa Wabunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ilielekezwa katika Wizara yetu ni kuhusu miradi 17 ya Serikali ya India. Nilivyoingia katika Bunge hili zilikuwa zinakuja hoja za miradi 17 mwili ulinisisimka, mwili ulinitetemeka, kwamba naenda kujibu nini; lakini Mheshimiwa Mpango leo nisimame kwa ujasiri umetuvisha nguo sisi Wizara ya Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi kumshukuru Rais wangu Dkt. John Pombe Magufuli kwa jitihada kubwa sana alizozifanya. Sisi kama Wizara ya Maji tunachokisema fedha zile zitakazotoka kwa miradi 17 ya India tutazifatilia shilingi kwa shilingi kuhalikisha kwamba Watanzania wanapata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili hatutamuonea haya mtu kwa sababu wakati mwingine fedha za Serikali zinaliwa kwa sababu ya kuoneana haya au kupeana kazi kiujomba ujomba au kiushemeji shemeji. Kwenye hili hatutakuwa na haya na mkandarasi ambaye atapewa, hata awe mtoto wa kigogo. Kama yeye atakuwa mtoto wa kigogo anatekeleza mradi lakini hana uwezo tunamcharanga ili aweze kuwa kuni akawaahida, wananchi waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine imezungumzwa na Mama yangu Anna Lupembe kuhusu mradi wa Ikolongo One pamoja na Ikolongo Two kwamba maji hayatoshelezi kwa kuwa miundombinu ni mibovu, hivyo maji hayawafikii wananchi kwa makanyagio na majengo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inafanya jitihada kubwa kuhakikisha Mji wa Mpanda unapata huduma ya uhakika ya maji kwa kutekeleza miradi mbalimbali. Kwanza kuna mradi wa Kanonge uliopangwa kujengwa kwa awamu mbili; awamu ya kwanza imekalimika na utekelezaji awamu ya pili unaendelea. Mradi huu ukikamilika utazalisha maji lita za ujazo 1,200,000 kwa siku. Aidha, ujenzi wa maji kutoka Ikolongo Two utaanza mwezi Julai, 2018. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumepokea hoja kutoka kwa dada yangu Esther Bulaya kuhusu DAWASCO kwamba ilishauliwa kununua kifaa cha kupunguza upotevu wa maji agizo hili halijatekelezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumjibu dada yangu Esther Bulaya kuwa vifaa vya kutambua uvujaji chini ya ardhi yaani liquid detector vipo. Vifaa hivyo vilinunuliwa wakati wa mradi wa kupunguza upotevu wa maji Jijini Dar es Salam.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine napenda kujibu hoja ya Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota kuhusu mradi wa Maji Makonde kwamba umechakaa na hivyo kuhitaji ukarabati mkubwa. Nataka nimwambie Mheshimiwa ndugu yangu Chikota ukiona giza linatanda ujue kunakucha. Pamoja na changamoto ambazo wamezipata wananchi wake lakini Mheshimiwa Mpango sasa ameshatupangia mambo yetu yapo vizuri, tunaenda kutekeleza mradi ule ili wananchi waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine inahusu Mheshimiwa Mbunge Maftaha Abdallah Nachuma, amezungumzia mradi wa maji kutoka Mto Ruvuma hadi Mtwara Mjini unaopita vijiji 26 vya Mtwara Vijijini kwamba haujatekelezwa kwa miaka mitatu sasa na wananchi wameshachukuliwa maeneo yao lakini fidia haijalipwa. Nataka nimjibu Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iliandaa mradi wa maji kutoka Mto Ruvuma hadi Mtwara Mjini na kupitia vijiji 26 vilivyopo Mtwara Vijijini. Tayari usanifu wa mradi umekamilika na taratibu za kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi zinaendelea ikiwemo kufanya majadiliano na Exim Bank ya China. Tathmini ya maeneo ya mradi yalishafanyika kwa ajili ya kulipa fidia, lakini wananchi bado hawajaondolewa katika maeneo yao. Kabla ya utekelezaji wa mradi huo kwanza waanchi watalipwa fidia zao. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge sisi kama Wizara hatutakuwa kikwazo katika
kuhakikisha wananchi wako wanalipwa fidia na mradi ule uweze kutekelezeka kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ni ya dada yangu Lucy Owenya, kuhusu ujenzi wa mradi wa maji katika Jimbo la Moshi Vijijini Kata ya Mbokomu kwamba umejengwa chini ya kiwango na kusababisha mradi huu usifanye kazi. Mradi huu ulikuwa chini ya Halmashauri ya Moshi Vijijini ambao uko chini ya TAMISEMI. Baada ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kupata malalamiko haya, imemuagiza Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Moshi Mjini kwa kushirikiana na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Moshi Vijijini kwenda kuangalia tatizo na kuandaa gharama za ukarabati wa chanzo hicho ambacho kitawezesha wananchi wa Kata ya Mbokomu kupata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine imetolewa na kaka yangu Mheshimiwa Ahmed Shabiby kuhusu mradi wa maji kwa mji wa Gairo kwamba ni muda mrefu ambapo mkandarasi amelipwa asilimia 80 lakini mradi huo hautoi maji. Ni kwei mradi wa maji Gairo umechukua muda mrefu kukamilika. Mradi ulianza kutekelezwa tangu tarehe 22 Agosti, 2010 na umetekelezwa kwa asilimia 87 ambapo hadi sasa mkandarasi amelipwa kiasi cha shilingi bilioni 3.844; dola za Kimarekani 1, 071,525 ambazo kwa ujumla ni sawa na asilimia
64 ya gharama za mradi mzima ambazo ni shilingi 5,315,612,551 na dola za Kimarekani 1,919,763.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi haujaanza kutoa maji kwa kuwa unahitaji kufungw amtambo wa kuchuja chumvi yaani reverse osmosis plant kwa kuwa visima vilivyochimbwa maji yake yalionekana kuwa na chumvi zaidi ya viwango vilivyokubalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuonekana mkandarasi ameshindwa kuagiza na kufunga mtambo huo kwa wakati, Serikali iliamua kumnyang’anya kipengele cha uagizaji na ufungaji wa mtambo wa kuchuja chumvi pamoja na pump. Tangazo la kumpata mzabuni kwa ajili ya kazi hizo lilitangazwa tarehe 3 Mei, 2018 ambapo ufunguzi wa zabuni unatarajiwa kufanyika tarehe 5 Juni, 2018. Mradi huu unategemewa kukamilika na kuanza kufanya kazi mwishoni mwa mwezi Novemba, 2018.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kujibu hoja ya Mheshimiwa Zainab Mndolwa Amir kuhusu kwamba Serikali itoe elimu ya kutosha kwa wananchi kuhusu utunzaji wa vyanzo vya maji mfano katika Milima uya Uluguru Morogoro. Ushauri wake umezingatiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia napenda kujibu hoja ya Mheshimiwa Mbunge wa Songea kuhusu suala la wananchi wake kuweza kulipwa fidia. Nataka nimhakikishie Mzee wangu Ndumbaro akae sasa mkao wa kula. Katika bajeti hii ya mwaka 2018/2019 tutawalipa wananchi wale fidia kiasi cha shilingi bilioni sita. Kwa hiyo, jukumu sasa la Mheshimiwa Mbunge kuwasimamia wananchi wale badala ya fedha zile kwenda kuoa, sasa wazitumie katika mipango ya maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu hoja ya Mheshimiwa Elibariki Emmanuel Kingu kwamba Bwawa la Kidunda lijengwe. Wizara ipo katika hatua za mwisho za mazungumzo na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) ili kupata fedha za utekelezaji wa mradi huu muhimu. Matarajio ni kufikia makubaliano haya ya mwezi Juni, 2018 ili zabuni za kumtafuta mkandarasi wa ujenzi ziweze kutangazwa mwezi Julai, 2018.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu hoja ya Mbunge wa Kasulu Mheshimiwa Daniel Nsanzugwanko kuhusu dola za Kimarekani milioni 500, kuna phase one, logic yake ni nini, kwa nini isiwe sambamba kwamba miradi yote ifanyike kwa wakati mmoja. Napenda kujibu hoja hii kwamba mradi wa miji 17 wa dola za Kimarekani kwa maana ya milioni 15 utatekelezwa kwa awamu mbili yaani phase one na phase two. Awamu ya kwanza itahusisha usanifu wa miradi katika miji yote 17 na awamu ya pili itahusisha ujenzi wa miradi husika hivyo mradi yote inategemewa kukamilika bada ya miaka minne.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu hoja ya Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Mrisho Kikwete kuhusu usimamizi wa mradi wa Chalinze uangaliwe kwa makini. Serikali imekuwa ikisimamia mradi wa Chalinze kwa makini kwa kuweka wahandisi maalum kwa ajili ya kufuatilia utekelezaji wa kila siku. Hatua mbalimbali za kimkataba zimekuwa zikichukuliwa kwa mkandarasi kila aliposhindwa kutekeleza matakwa ya mkataba ikiwa ni pamoja na kutoa onyo na kumkata fedha. Hata hivyo, ilipofika tarehe 22 Februari, 2018 Serikali ililazimika kumsimamisha kazi mkandarasi kwa mujibu wa mkataba baada ya kusindwa kutekeleza makubaliano yaliyopo ndani ya mradi. Hivi sasa Serikali inashauriana na mfadhili wa Benki ya Exim ya India jinsi ya kumaliza kazi zilizobaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu hoja ya Mheshimiwa Mary Pius Chatanda wa Korogwe, kwanza anatoa shukrani kwa kupelekewa na Wizara kiasi cha shilingi milioni 500. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba shukrani zake tumezipokea na sisi kama Wizara tutaendelea kumpa ushirikiano ili wananchi wake wa Korogwe waweze kupata maji safi na itakapofika mwaka 2020 waende kumchagua kwa mara nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu hoja ya Mheshimiwa Hamidu Hassan Bobali, Mbunge wa Mchinga kuhusu kuchanganya kwa takwimu za maji. Mfano Dar es Salaam takwimu zinaonesha wakazi wengi wanapata maji lakini maji hayajafika.

Mheshimiwa Naibu Spika, takwimu zilizotolewa ni za ujumla, wananchi wanapata maji ya uhakika ni wale walioko katika maeneo yanayopata maji kutoka Ruvu Juu na Ruvu Chini. Ni kweli kuna maeneo ambayo hayapati maji ya bomba kwa sababu yako mbali na mfumo wa Ruvu Juu na Ruvu Chini au mtandao wa bomba haupo. Maeneo haya ni pamoja na Mbagala, Kongowe, Kigamboni, Chamazi, Chanika, Msongola, Kitunda, Yombo Vituka, Pugu, Gongolamboto na Kinyerezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya 2018/2019 Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuongeza mtandao wa mabomba ili kufikisha maji kwa wananchi wengi zaidi. Pamoja na changamoto katika Wizara yetu ya Maji, Mwenyezi Mungu anasema; “Waama bii neemati rabikka fahadith” (zielezeeni neema za Mwenyezi Mungu kwa kushukuru). Nataka nimwambie kaka yangu Mnyika, moja ya hoja yake alikuwa akilalamika kuhusu eneo lake la Kibamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimwambie Mheshimiwa Mnyika, kazi kubwa sana imefanywa na Wizara hii ya Maji. Kulikuwa na kilio kikubwa sana Dar es Salaam lakini kumekuwa na utekelezaji wa kupanua Ruvu Juu na Ruvu Chini katika kuhakikisha wanaongeza lita kutoka lita 300 mpaka lita 504, Mwenyezi Mungu atupe nini? Atupe donda tufukuze nzi? Zipo changamoto lakini tunachotaka tunaomba ushirikiano ili zile kata zake sita sasa ambazo hazina maji twende kuwapatia maji na hii ni kazi nzuri yote inayofanywa na Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukizaa mtoto anafanya vizuri, jukumu lako ni kumuombea dua. Rais wetu anafanya vizuri Waheshimiwa Wabunge, jukumu letu ni kuhakikisha tunampa ushirikiano wa dhati na sisi wasaidizi wake tutafanya kila linalowezekana ili wananchi tuweze kuwapatia maji safi, salama na yenye kuwatosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu hoja ya Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, kaka yangu kuhusu upungufu wa wataalam katika sekta ya maji na hatua zinazochukuliwa na Wizara kukabiliana na upungufu huo. Ni kweli kuna upungufu wa wataalam katika sekta ya maji hapa nchini, hali ambayo imesababisha baadhi ya mamlaka za Serikali za Mitaa kushindwa kusimamia miradi yake. Wizara imechukua hatua zifuatazo:-

Moja katika mwaka 2017/2018 Wizara ilipata kibali cha kuajiri watumishi 154 wa sekta ya maji ambapo hadi mwezi Mei, 2018 wataalam 106 walipangiwa vituo vya kazi.

Kati ya wataalam hao 37 walipangiwa ofisi za mikoa na Halmashauri za Wilaya na 76 walipangiwa katika Bodi za Maji za Mabonde, Miradi ya Kitaifa na Mamlaka za Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa iliyopo kwenye eneo hili ni kwamba sekta inaendelea kukua, lakini pia kuna upungufu wa wataalam unaotokana na vifo, kustaafu, kuacha kazi na kufukuzwa kazi kutokana na sababu mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu hoja ya kaka yangu Mheshimiwa Dunstan Kitandula kuhusu Makao ya Wilaya ya Mkinga kwamba hakuna maji. Serikali inaendelea kuhakikisha kuwa wananchi wote wanapata huduma bora ya majisafi na salama ikiwa ni pamoja na wananchi waishio katika Makao Makuu ya Wilaya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Aweso, muda wako umekwisha. Dakika mbili malizia.

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nirudie tena kuwaomba Waheshimiwa Wabunge, sisi kama Wizara ya Maji na nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wangu wa Maji nilivyoteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Maji aliniambia nipite maeneo mbalimbali kuangalia hali na utekelezaji wa miradi ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na ninyi, hali ilikuwa hairidhishi. Ipo miradi ambayo imekamilika lakini haitoi maji, hakuna sababu ya kulalamika. Mheshimiwa Waziri amechukua hatua sasa ya kuunda RUWA ili twende kuisimamia ili wananchi waweze kupata maji safi, salama na yenye kuwatosheleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, sina maneno mengi sana. kikubwa tunachoomba Waheshimiwa Wabunge ni ushirikiano, na sisi kama viongozi wa Wizara, tutafanya kazi kwa moyo na michango yenu leo mliyoitoa imetupa ari na moyo katika kuhakikisha tunafanya kazi hizi ili wananchi wetu waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana.