Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na mimi kupata nafasi ya kuchangia mjadala huu kuhusu Hotuba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyetupa afya na uzima tumekutana asubuhi ya leo kuchangia Wizara hii muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutupatia viwanda vitatu vipya katika Jimbo letu la Morogoro Kusini Mashariki, Mkulazi One, Philip Morris na Mahashree cha kuchakata mbaazi, nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa sababu kama Magufuli asingekuwa Rais, Mkulazi One isingekuja Mkulazi, kiwanda kile cha sukari kisingekuja pale na leo nitazungumzia hoja hii tu moja mwanzo mwisho, nikipata muda nitazungumzia ya pili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tulikuwa na ziara na Mheshimiwa Rais pale Morogoro na nilimweleza hili, nilimwambia mchakato wa kujengewa Kiwanda cha Sukari Mkulazi kilianza tangu mwaka 2016 mpaka leo Serikali yako ina mchakato, kiwanda hakijaanza kutengenezwa. Nilimwambia wanaokukwamisha wapo ndani ya Serikali na chama chako, tupo Bungeni na sehemu nyingine kwenye taasisi za umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo habari zilikuwa za mtaani, leo nimezipata rasmi kwenye ukurasa wa 32 wa kitabu cha Mheshimiwa Waziri; anasema kiwanda cha kutengeneza sukari cha Mkulazi One kilichokuwa pale Morogoro Jimboni kwangu kitaanza kuzalisha mwaka 2025, miaka saba kuanzia sasa. Kiwanda cha Mkulazi II ambayo ni Mbigiri anasema kitaanza kuzalisha mwaka 2022 baada ya uchaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nilimwambia Dkt. Magufuli juzi kwamba lengo viwanda hivi vianze kuzalisha baada ya uchaguzi ili watu waje na ajenda wakwambie ulisema wewe Tanzania ya viwanda, viko wapi na leo inatimia kwa ushahidi wa kitabu hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa simuelewi Mheshimiwa Rais siku zote anaposema wasaidizi wangu wengine hawanielewi, leo ndiyo nimemuelewa. Tunafahamu siyo wote walifurahia kiwanda hiki kujengwa Morogoro, kuna watu walitaka kijengwe sehemu nyingine. Vilevile tunafahamu kuna wengine hawakupendezwa kiwanda hiki kupewa NSSF na PPF kwa sababu kuna wengine washindani wa hiyo biashara ya sukari walitaka shamba lile waliendeleze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wanapitia mlango wa nyuma kukwamisha kiwanda hiki kuanza kwa wakati ili kutoa ajira kwa Watanzania, kuongeza uchumi wa Watanzania na kuondoa tatizo la sukari nchini. Mungu anawaona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi, walikuja na sababu zote, sababu ya kwanza walisema kwamba wakati Mheshimiwa Rais anaiomba mifuko ya jamii ijiingize kwenye viwanda, wanasema mifuko haina uzoefu wa sukari kwa hiyo kujiingiza kwenye viwanda ni kupoteza hela za wanachama, hilo limepanguliwa limekwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadae wanasema kwamba hapana, mkataba umesainiwa na mtu ambaye ni tofauti, kwenda wakagundua aliyesaini ni mtu sahihi. Mara nyingine wanasema kwamba hapana raw material haijakuwa tayari, hivi kiwanda na raw material kinaanza nini? Tulikuwa na Mheshimiwa Rais juzi Kilombero, wananchi wanalalamika soko la miwa halipo, Mtibwa, Turiani wanalalamika soko la miwa yao halipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wawekezaji wako tayari, walishasaini mkataba tangu mwaka jana na mtengenezaji wa kiwanda kile, kile Kiwanda cha Mbigiri II kilitakiwa kifike mwezi wa kwanza mwaka huu. Kiwanda cha Mkulazi I kilitakiwa kifike Juni mwaka huu na Kiwanda cha Mkulazi II kilitakiwa uzalishaji kianze mwezi huu, lakini mpaka leo Serikali haijatoa kibali kwa mwekezaji. Ndiyo maana tunasema tatizo si pesa wakati mwingine, tatizo ni uzalendo na dhamira ya dhati ya kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua, ni kweli kabisa mbuzi hula kwa urefu wa kamba yake, lakini si lazima kila jani lililopo pale atakula. Tatizo la watumishi wengi huko ndani ya Serikali wanataka kila jambo lazima kuwe na cha juu ili na yeye anufaike, kama jambo hilo hanufaiki yeye yuko radhi lichelewe hata miaka kumi, hata mradi upotee kwa sababu tu yeye hajanufaika, hili halikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wekeni maslahi yenu pembeni, tangulizeni Tanzania kwanza, wekeni uzalendo kama alivyouonesha Dkt. John Pombe Magufuli. Ninayasema haya, nafikiri ananisikia, ajue namna gani kwamba kuna watu wanamkwamisha katika Sera hii ya Viwanda. Nilimwambia na leo nimelirudia baada ya kuona kwenye kitabu hiki kwamba viwanda hivi vitaanza kutekelezwa baada ya uchaguzi 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana watumishi wa Serikali, sisi tulitoka sekta binafsi tulikua tunapimwa kutokana na matokeo, wenzetu wanapimwa kutokana tu na chochote ambacho hakina tija wakati mwingine.

Naomba majibu ukija kufunga hoja yako, kiwanda hiki tayari hela zipo na mwekezaji ameshawekeza, Kiwanda cha Mbigiri II mwekezaji ameshalima zaidi ya hekta 1000 za miwa, tunavuna kuanzia Juni, 2018. Lakini pia outgrowers (wakulima wadogo) walishapata mkopo kutoka Benki ya Azania zaidi ya 4.9 billion na wameshalima zaidi ya hekta 600, hawa wote baada ya kuvuna watapeleka wapi bila kiwanda hiki?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali toeni kibali haraka iwezekanavyo, kiwanda hiki kiagizwe kianze uzalishaji Mbigiri II mwaka huu na Mbigiri I mwakani; zaidi ya hapo hatutaelewana, nafuatilia mradi huu kwa karibu sana. Siku ile nilimwambia kama hatutapata kibali haraka nitaenda tena Ikulu kwenda kumueleza Mheshimiwa Rais na tutawataja hata kwa majina wale wanaomkwamisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya pili, Morogoro ndio uliokuwa mji wa viwanda na ninataka nimwambie Dkt. John Pombe Magufuli, nampongeza sana kwa sababu anatekeleza ndoto zote za Mwalimu, anajenga Stiegler’s, anajenga Kidunda, amehamisha Makao Makuu kuja Dodoma, lakini sasa kama alivyosema juzi, kuwa katikati kuna raha yake, lakini katikati hiyo Mwalimu Nyerere alimaanisha Morogoro ndiyo uwe mji wa viwanda. Na wakati ule aliunganisha na Pwani kwa sababu sehemu kubwa ya Pwani ilikuwa ni sehemu ya Mkoa wa Morogoro, hatukuwa na Mkoa wa Pwani, tulikuwa na Dar es Salaam na Morogoro na ndiyo maana alisema kwamba Morogoro uwe mji wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tulikuwa na viwanda vyetu zaidi ya 11 vile vya kimkakati, leo vinavyofanya kazi ni vinne tu. Vinavyofanya kazi ni Kilombero Sugar, Mtibwa pamoja na kile cha tumbaku, pia kinachechemea hiki cha 21st Century ambacho kinafanya kazi na Moproko imeanza.

Nataka majibu ya kina, nini hatima ya viwanda saba vilivyobaki? Morogoro Ceramic ambayo raw material ilikuwa inatumia mchanga tu, lakini mnafahamu mmewauzia watu kwa bei ndogo kwa kupeana kiujomba ujomba, matokeo yake wale waliochukua viwanda vile wakang’oa mashine kwenda kuuza kama scraper, naona kwa sababu wamenunua kwa bei rahisi, hata akiuza scraper yeye anapata faida kuliko ku-run kiwanda. Nataka mniambie Morogoro Ceramic iko wapi, Kiwanda cha Magunia kiko wapi? Mniambie Kiwanda cha Ngozi kiko wapi na mna mkakati gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mpaka kile la Mang’ula, kiwanda ambacho ndiyo uhai wa Reli ya TAZARA, na mnafahamu mpaka leo, Mang’ula hakipo, leo TAZARA tutaiendeshaje? Ilikuwa chuma chochote, spare yoyote ya gari au ya namna gani usipoipata mahali popote unaenda kuchongesha pale Mang’ula, leo Serikali kama hamuoni lolote, hamuoni umuhimu huo Wachina tafuteni namna gani ya kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana mlete majibu mazuri. Nilisikitika sana, nilitamani kulia siku ile wakati anaongea Mzee Kasori kuhusu historia na umuhimu wa kiwanda kile. Leo tupo tumepata Rais, Dkt. John Pombe Magufuli, mzalendo, msaidieni. Kiwanda hiki ndio uhai wa TAZARA, nchi maskini kama hii Tanzania haiwezi kununua kila spare part kutoka China bila kukifufua kiwanda hiki kukirudisha katika hali yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nayasema haya najua mpaka uwe na roho ngumu kuyasema, na watu watanichukia lakini lazima ukweli niyazungumze kwa sababu mimi natoka Morogoro, viwanda hivi viko Morogoro, vina faida kubwa sana kwa watu wa Morogoro, kwa taifa, lazima tuambiane ukweli. Bila kuambiana ukweli hatutoki hapa tulipokwama. (Makofi)