Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. LOLESIA M. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Viwanda na Biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watumishi wote wa Wizara kwa kazi kubwa ambayo wamefanya katika Wizara hii ninasema hivyo kwa sababu kuna ongezeko katika pato la Taifa kwa asilimia 0.6 ambalo limechangiwa na sekta ya viwanda. Kwa hii inaonesha jinsi ambavyo Wizara hii inafanya kazi kubwa zaidi katika kuhakikisha kwamba uchumi wetu unaimarika siku hadi siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nikiangalia malengo yenyewe ya Wizara yenyewe ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwanza kabisa inahakikisha viwanda vilivyopo vinafanya kazi zake vizuri, kwa uhakika na kuweza kuongeza zaidi mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, kuhakikisha kwamba viwanda vyote ambavyo vimebinafsishwa ambavyo havifanyi kazi vinafanya kazi vizuri. Vilevile kuhamasisha wananchi ili waweze kushiriki katika kuwekeza na kuanzisha viwanda vipya. Hayo ni malengo matatu ambapo Wizara imejiwekeza.

Mimi nitazungumzia zaidi kwenye kuanzisha viwanda vipya. Lazima Wizara sasa pamoja na Serikali kwa ujumla iweke mikakati ya dhati na kuhakikisha kwamba kupitia mikakati hii itawezesha uwanzishwaji viwanda hivi. Kwa mfano lazima kuwepo na mazingira wezeshi ya uwanzishwaji wa viwanda; kwanza ni kuhusu umeme. Haiwezekani kuanzisha viwanda tusipokuwa na umeme wa uhakikka. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kusimamia msimamo wake wa Stiegler’s Gorge, ule mradi mkubwa wa umeme; kwa sababu anakusudia tuweze kupata umeme wa uhakika. Vile vile mpango wa Serikali wa REA wa kuhakikisha kwamba watanzania mpaka vijiji wanapata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Wizara inayohusika ya Nishati kuhakikisha kwamba suala la umeme linakuwa ni kipaumbele cha umuhimu kabisa kwa sababu wananchi vijijini hawawezi kuanzisha viwanda bila ya kuwa na umeme wa uhakiksha. Katika mpango wa Serikali wa kwamba kufikia mwaka 2020 na 2021 vijiji vyote vya Tanzania vitakuwa vimepata umeme, niombe Serikali hasa kwa REA iweze kuwekeza zaidi fedha nyingi kwenye REA ili kuhakikisha umeme wa uhakika unafika vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo wananchi wameitikia sana na hii Tanzania ya viwanda wengi hasa walioko vijijini wameitikia sana kuanzisha viwanda. Hata mimi katika Mkoa wangu watu wengi wanafuata wanataka kuanzisha viwanda, lakini changamoto kubwa ni upatikanaji wa uhakika wa umeme hasa vijijini ambako wanataka kuanzisha viwanda. Kwa hiyo niiombe Serikali sasa kwamba mwaka huu 2018 itenge bajeti kubwa, hasa kwenye Wizara ya Nishati, kwenye REA ili wananchi hasa wa vijijini waweze kupata umeme wa uhakika.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia jambo la pili la kimkakati ni suala la elimu. Haiwezekani kuanzisha viwanda ikiwa vijana wetu hawana uwezo, hawana ujuzi wa kutosha wa kuweza kufanya kazi viwandani. Kwa hiyo niombe katika sekta ya elimu pia tuangalie hili suala la kuwa na VETA kwenye kila Wilaya kama sera ya taifa inavyosema katika upande wa elimu. Kuna Mikoa mingi ambapo mpaka sasa hatujafikia hatuna vyuo vya VETA na Wilaya nyingine hakuna vyuo vya VETA .

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niiombe Serikali ijielekeze katika kuhakisha kwamba ile Mikoa na Wilaya ambayo mpaka sasa hawajapata vyuo vya VETA wahakikishe vyuo hivi zinajengwa kwa haraka ili kuwezesha wanachi hasa vijana kuweza kupata elimu ya ujuzi katika ufundi ili hatimaye waweze kushiriki vizuri katika viwanda kwa sababu Tanzania ya viwanda haitawezekana bila kuwa na ujuzi wa uhakika.

Vilevile niiombe Serikali iweke pia fedha kwa ajili ya kusomesha vijana wetu nje ya nchi. Kwa sababu kuna ujuzi mwingine tunaupata kutokana kupata kwa wenzetu, nilikuwa nikianagalia katika Awamu ya Kwanza ya Mheshimiwa Rais Marehemu Nyerere watu wengi sana walikuwa wanapelekwa nje kwa ajili ya kujifunza teknolojia na ndiyo maana pia hii sekta ya viwanda ilikuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe katika awamu hii Serikali itenge fedha ipeleke vijana hata kama ikiwezekana vijana wapelekwe nje ya nchi ili waweze kujifunza mbinu na ujuzi mbalimbali ili kuweza kufanya kazi na kuweza kuleta teknolojia mpya katika nchi yetu ili kuwawezesha vijana hao kuweza kufanya kazi zao vizuri, la sivyo viwanda hivi ambavyo vinaanzishwa hasa na wageni kama vijana wetu hawatakuwa na teknolijia wanayoijua na ujuzi itakuwa si rahisi kuweza kupata ajira za hali ya juu, watakuwa wanafanyakazi za kada ya chini kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali katika sekta ya elimu iendeleze zaidi Vyuo vya VETA ikiwezekana tufanye kila hata Jimbo, sasa hivi sera ni kila Wilaya lakini niiombe Serikali yaani iwezeshe kila Wilaya sasa ambazo hazijapata VETA ziweze kupata Vyuo vya VETA. Lakini hapo baadae pia ikiwezekana tuangalie hata kila Jimbo liweze kupata Chuo cha VETA kwa sababu vijana wengi sana wanamaliza sekondari, hawana ujuzi yaani hawana uwezo wowote, hawana ujuzi wowote lakini wanapokuwa na stadi za maisha hasa katika Vyuo vya VETA mimi nina uhakika vijana hawa wataweza kushiriki vizuri hasa katika Tanzania ya viwanda katika ujuzi waliokuwa nao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ni muhimu Serikali iwekeze hasa katika kuwezesha mazao ya kiuchumi. Kuna mazao mengi sana na wakulima asilimia 70 ya Watanzania wanaishi vijijini na ndiyo ambao wanashughulika na suala la kilimo. Tunaiomba sasa Serikali iangalie sana suala la kilimo kwa sababu haiwezekani kuweza kupata malighafi tusipowekeza katika suala zima la kilimo. Kwa hiyo, niiombe Serikali iangalie kabisa hata katika maeneo ambapo tumezungukwa na maziwa kwa mfano, Ziwa Victoria na Ziwa Tanganyika na maziwa mengine tuweke hata kilimo cha umwagiliaji ili kuwezesha upataikanaji wa mazao ya malighafi kwa ajili ya viwanda vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kikubwa zaidi wananchi wengi wa Tanzania wamehamasika sana katika hii sera ya Tanzania ya viwanda, watu wengi wamehamasika, wanataka kuanzisha viwanda, changamoto tu ni hizo, mambo muhimu kabisa hilo suala la elimu naomba Serikali izingatie na suala la umeme iwe ni kipaumbele cha uhakika ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanashiriki kikamilifu katika suala zima la viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la biashara, katika biashara ni kweli wafanyabiashara wengi wanazo changamoto nyingi sana. Nilikuwa ninaomba Wizara kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara tuwe na muda wa kwenda kukaa na wafanyabiashara hata katika maeneo yao vijijini. Tumezoea tu mikutano mingi inafanyika mijini, tuombe na vijijini pia wako wafanya biashara ambao wanahitaji pia tukae nao, tuangalie changamotyo zao hatimaye tuweze kutatua kero zao walizonazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwasababu nimekuwa na experience katika Jimbo langu kuna sehemu kubwa kuna centre ya biashara kunaitwa Katoro kulikuwa na changamoto kubwa watu wengi wanafanya biashara nyingi lakini sasa kumekuwa na changamoto za hapa na pale, TRA inasumbua, sijui zimamoto yaani wanakuwa na changamoto nyingi sana lakini Serikali kupitia Wizara husika ikipata fursa kwenda kukaa na hao wafanyabiashara itaweza

kusikiliza kero zao na hatimaye watakuwa na mazingira mazuri kabisa ya kuweza kufanya biashara na hatimaye sasa tutaweza kufikia lengo la taifa la kufikia uchumi wa kati kama ambavyo tumejipangia.

Kwa hiyo, niombe, nituie fursa hii kuomba Wizara tutoke nje kama wezangu walivyosema, tusijifungie tu ofisini, twende field, twende vijijini, twende mijini, tukae na wafanyabiashara tusikilize kero zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia changamoto nyingine katika biashara nimeona kwa sasa hivi watu wengi wamejikita kuchukua bidhaa kutoka Uganda. Sasa nilikuwa najiuliza kwamba kwanini hapa Kariakoo sasa watu hawaendei kuchukua bidhaa? Siku za nyuma tulikuwa tumezoea watu walikuwa wanatoka Zambia na sehemu mbalimbali wanakuja Kariakoo wananunua bidhaa wanakwenda kuuza kwao lakini sasa hivi imekuwa tofauti. Watu wengi wanakwenda kununua bidhaa Uganda kwa hiyo, ninaomba Wizara pia iangalie hili ni kwanini sasa watu wanakwenda Uganda kuliko kwamba watu wa Zambia na watu wa Uganda waje Tanzania kununua bidhaa ili waende wakauze huko kwao.

Kwa hiyo, niombe jambo hili Serikali ilifanyie kazi, ilifanyie utafiti wa kutosha kwamba ni kwanini bidhaa nyingi watu wanakwenda Uganda isiwe Tanzania ambapo Tanzania tuna bandari, tuna kila kitu, tunajenga standard gauge yaani tunafanya vitu vingi. Sasa ni kwa nini badala ya watu kuja Tanzania kununua bidhaa sasa wanakwenda Uganda kununua bidhaa kwa ajili ya kuuza katika nchi yetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu maana yake tunapoteza pato la Taifa, tunapoteza uchumi, tusipolifanyia kazi jambo hili pengine tunaweza tukapoteza watu wengi, tunaweza tukapoteza biashara…

T A A R I F A . . .

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani kama yeye sababu yake ndiyo hiyo lakini ninatoa ushauri kwa Serikali waende walifanyie kazi jambo hili kwa sababu tunaona changamoto ipo na watafute namna sasa kujua, kufanya utafiti wa kutosha ili hatimaye wajiridhishe kwamba ni sababu gani na hatimaye hiyo sababu waweze kuifanyia kazi mwisho wa siku Tanzania basi tuwe hub, tuwe soko ambapo watu wengi watatoka sehemu mbalimbali nje ya nchi kuja kununua bidhaa katika nchi yetu ya Tanzania kama ilivyokuwa zamani. Kariakoo ilikuwa inajulikana ni sehemu ambapo watu walikuwa wanatoka Congo, wanatoka Zambia, wanatoka sehemu mbalimbali kuja kariakoo kwa ajili ya kununua bidhaa mbalimbali.

Kwa hiyo, niiombe Serikali jambo hili ilifanyiekazi na Mheshimiwa Waziri pengine uunde task force ya kuweza kulifanyiakazi jambo hili ili kuhakikisha kwamba uchumi wa Tanzania uendelee kwenda juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.