Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JOSEPH L. HAULE. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, awali ya yote nitoe pole sana kwa Mbunge mwenzangu Mheshimiwa Jesca David Kishoa, ambaye amepata ajali mbaya sana asubuhi hii tunamuombea kwa Mungu aweze kumpa nguvu na uponyaji wa mapema aweza kurudi kuendelea kulitumikia Taifa. Lakini pia nitoe pongezi kubwa sana kwa pacha wangu Joseph Mbilinyi a.k.a Sugu kwa kuhitimu mafunzo ya huko ndani ambayo yameongeza sana ujasili na cv yake ya kisiasa natumaini sasa hivi hatokuwa Rais wa Mbeya bali anaenda kwenye mchakato wa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania huko siku za mbeleni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa haraka kidogo, kwenye Wizara hii ya Viwanda kama wenzangu walivyosema Mkoa wa Morogoro ulibarikiwa kuwa na viwanda vingi sana ambavyo vingi vilibinafsishwa, na tukiwa tunategemea wawekezaji waweze kuviboresha kwa zaidi, lakini kwa masikitiko viwanda vingi vya Mkoa wa Morogoro vimekufa. Hapo ninavyoongea na wewe viwanda vya Moproco, Komoa, Canvas, Morogoro Leather Shoes na viwanda vingine kadha wa kadhaa viko ICU na sasa hivi zimekuwa kama Magodauni na vingine vinafugiwa mpaka mbuzi vitu ambavyo kiukweli sidhani kama ni lengo la Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi . (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nikuombe Waziri kabla hatujaenda kwenye viwanda vipya tuangallie wapi tulijikwaa na viwanda vyetu vilifanywaje ili tuweze kuvirudisha na kuangalia jinsi gani ambavyo tunaweza kuirudisha Morogoro kwenye ramani, kwa sababu sasa hivi pia Serikali ilitangaza kwamba muda si mrefu Morogoro inakwenda kuwa ghala la Taifa la chakula. Kwa hiyo, tunahitaji viwanda vingi, tunahitaji kufufua malighafi nyingi, kwa sababu morogoro imebarikiwa sana kilimo na ina ardhi nzuri na kila sifa ambayo inastahili kuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja nijikite katika jimbo langu la Mikumi. Mikumi tumejikita na tuna kiwanda kikubwa sana cha Sukari cha Kilombero, kiwanda hiki kila mmoja anajua kwamba ni moja kati ya viwanda vikubwa sana Tanzania ambavyo vinatoa ajira kubwa na ni tegemeo kubwa sana kwa sukari hapa nchini Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1999 kwenda 2000 wakati kiwanda hiki cha Kilombero Sugar Company kikimilikiwa na Serikali kilipunguza wafanyakazi takribani 3000, na ilipoingia Illovo kwenda kama mwekezaji. Hawa wafanyakazi mpaka leo hawajalipwa fidia zao. Kilio hiki cha wafanyakazi ni kikubwa sana na kimeleta taharuki kubwa. Wazee wetu walitumikia kiwanda hiki kwa nguvu zao zote, kwa uwezo wao wote, kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lakini wengine wamekufa bila kulipwa mafao yao, na wengine wanataabika kupata mafao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, juzi tulikuwa na Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania na nilimuuliza swali hili. Kiwanda hiki ni muhimu sana kwa wakazi wa Mikumi, lakini Jimbo la Kilombero, Jimbo la Mlimba na Wilaya nzima ya Kilosa. Wafanyakazi wengi sana wameajiriwa kwenye kiwanda hiki, ni kiwanda kikubwa tunakipenda na kinaonesha ushirikiano. Lakini tunaomba sana Waziri, Rais alisema kwamba wakati mnabinafsisha kiwanda kwenda Illovo Serikali ilifanya makosa na wawekezaji walifanya makosa, hakusema kwamba wale wafanyakazi wana makosa yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Serikali iwalipe fidia hawa watu walioachishwa kazi zaidi ya watu 3000 ambao kiukweli kabisa inaonesha hii ni haki yao ya msingi. Na niombe kuwaambia kwamba hata Kiwanda cha Makaratasi cha Mgololo na wenyewe walikuwa na kesi hii

lakini wenzetu wamelipwa hivi karibuni niwaombe Serikali mtupie jicho na Mheshimiwa Waziri wewe ni rafiki yangu kila nikikutana na wewe unaniambia nakupiga na kiwanda kimoja hapa nina viwanda kama vitatu mfukoni. Siku utakapokuja kule Ruaha watu wanakusubiri wapate majibu kwamba ni lini Serikali inakwenda kuwalipa fidia hawa wazee wetu ambao wametumikia Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Kiwanda cha Sukari Kilombero.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja hilo, ili tuweze kutunza viwanda vyetu tunahitaji kuwa na mahusiano mazuri tunasema kiwanda cha Ilovo wanafanya vizuri sana wametoa ajira kubwa sana kwa Watanzania pale. Lakini mahusiano yamekuwa mabaya sana kati ya wakulima wa nje pamoja na kiwanda na Ilovo. Bado tunakuwa na matatizo ya mizani, bado wakulima wanalipwa sucrose kwa kiwango kidogo, lakini pia tunasema kwamba ili tuweze kuwa na uwiano ni lazima tuwe na mzani huru kwa sababu mpimaji ni huyo huyo, mpanga bei ni huyo huyo wakulima wetu wanaumia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa hivi kumekuwa na taharuki kubwa sana na changamoto kubwa wale wafanyakzi wa kiwanda cha pale cha Ilovo wamekuwa na mgogoro mkubwa sana na mfuko wa jamii wa NSSF. Kwa sababu wale wafanyakazi wanafanya kazi ki mikataba na kila msimu wanaweza kuajiriwa kwa miezi nane mpaka 10 na ile baada ya miezi 10 inaahirishwa wanakuwa na mapumziko ya miezi miwili na wanaporudi kwenye msimu mpya kiwanda kinaweza kikawaajiri tena au kisiwaajiri. Kwa hiyo, inasababisha wale wafanyakazi ambao wamefanya kazi na hawarudishwi tena kwenye kiwanda hawawezi kupewa pension yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.