Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa na mimi niweze kuchangia hotuba hii ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kutoa pongezi zangu za dhati kwa Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kufanya kazi kubwa zinazoonekana. Napenda tu kutoa wito kwa vijana wenzangu na Watanzania wote tumwombee Rais wetu, lakini tumpe nguvu na tumpe moyo ili aweze kuendelea kufanya kazi anayoifanya ambayo imedhihirika kwa kipindi kifupi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi kubwa ambazo wanazifanya. Niseme tuna imani nao, waendelee kufanya kazi zao na wamuombe Mungu awasimamie ili waongeze juhudi na wafanikishe yale ambayo Watanzania wanayategemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kuzungumzia suala la vijana. Sisi tunafahamu kwamba vijana hawapati fursa za kutosha kuajiriwa katika Serikali au sekta binafsi na wanahitaji na kila siku tunasisitiza kwamba vijana waweze kujiajiri wenyewe. Kweli sasa hivi vijana wanajitahidi sana kujiajiri wenyewe kupitia mifumo ya kufanya biashara. Sasa Wizara hii ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kupitia BRELA imeweza kufanikisha kutengeneza Online Business Registration Platform yaani ni mfumo wa kielektroniki au wa kimtandao wa kusajili biashara na makampuni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo huu umeleta urahisishaji mkubwa sana katika usajili wa biashara na makampuni na umeleta urahisi. Kwa hiyo, tunachoomba ni zile changamoto ambazo mfumo huu umeleta Wizara iweze kuziboresha ili kuleta ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa changamoto ni zipi? Naomba Serikali kwanza mzitambue, lakini mtafute njia ya kuzitatua. Changamoto ya kwanza ni kijiografia tu Tanzania yetu hii ni pana na kwa sababu mfumo huu wa Online Business Registration unahitaji matumizi ya mtandao, basi wawasiliane na Wizara husika ili tuweze kuona mtandao unaweza kupatikana hata huko vijijini na katika Tanzania yetu hii yote nzima ili kuweza kuleta manufaa makubwa zaidi ya mfumo huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hivyo tu, kwenye Dawati la Huduma kwa Wateja (Help Desk), ninaiomba sana Serikali iweze kuboresha huduma kwa wateja, kwa sababu mfumo wowote wa kimtandao unahitaji monitoring, unahitaji huduma kwa wateja. Katika huduma kwa wateja katika mtandao huu changamoto ambazo vijana wanazipata katika usajili wa biashara na makampuni ni kwamba unaweza ukapiga simu huduma kwa wateja na ile simu isipokelewe au pale pindi simu inapopokelewa bado kunakuwa hakuna utatuzi wa papo kwa hapo kwa changamoto ile ambayo mtu anayetaka kujisajili anakumbana nayo. Kwa hiyo, naomba Serikali itambue kwanza kuna changamoto hiyo, lakini waweze kuifanyia kazi, kuboresha ili tuwe tuna huduma kwa wateja kama vile tunavyoona katika mitandao ya simu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kupata leseni ya biashara kumewekwa kigezo cha kuwa na Kitambulisho cha Taifa ili uweze kujisajili katika huu mfumo (Online Business Registration Platform) ambayo ipo BRELA, ni lazima uwe na Kitambulisho cha Taifa. Sasa sisi tunajua siyo vijana wote wana Vitambulisho hivi vya Taifa, siyo Watanzania wote ambao wana Vitambulisho hivi vya Taifa na wanahitaji kusajili biashara zao, na sisi tunahitaji kurasimisha biashara za Watanzania ili tuweze kupata kodi, lakini wanakosa kitambulisho hiki na wanakosa uwezo wa kusajili hizi biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu naomba Serikali kwa wakati huu ione utaratibu wa kuweza kutumia kitambulisho kama cha Mpiga Kura ambacho sifa ya kuwa na Kitambulisho cha Mpiga Kura ni sifa kama ile ile ya kuwa na Kitambulisho cha Taifa, yaani kwa maana ni Mtanzania ili tusiweze kuwakwamisha vijana wetu au wafanyabiashara wetu kuweza kusajili makampuni yao na biashara zao.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka Watanzania wafanye biashara kwa kufuata mifumo ya kisheria, kwa sheria zetu ambazo tumezitunga wenyewe hapa Tanzania. Kwa hiyo, tuwawekee mazingira mazuri ili waweze ku-conform. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia imeweka sharti, ili uweze kupata leseni ya biashara lazima upate tax clearance, ulipe kodi ile ya TRA. Sasa hili ni jambo jema, lakini sasa changamoto yake inakuja kwa ile startup businesses, yaani kwa wale wanaoanzisha biashara kwa mara ya kwanza. Kwa sababu hata ukiangalia Sheria ya Kodi (Income Tax Act) inataka na inatambua kwamba kodi ya mapato ni ile kodi inayotokana na biashara halisi. Sasa unataka upate leseni uanzishe biashara, kijana anataka kuanzisha biashara yake ajiajiri, unamwambia aanze kwanza kwa kulipa kodi ambayo hajaifanyia biashara akapata faida, hiki ni kikwazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naishauri Serikali ifanye utaratibu ili kwenye startup business kusiwe kuna hii requirement ya tax clearance kwa ajili ya kupata business license. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine Serikali imekuwa ina ubunifu wa kuwawezesha vijana na wanawake lakini na makundi mengine katika jamii kwa kutumia mifuko mbalimbali kuwawezesha kimtaji. Hili ni jambo jema sana, tumeona vijana na wanawake wengi wananufaika, lakini sisi wote tunatambua kwamba kumekuwa na changamoto ya kusonga mbele yaani kumekuwa na vicious circle. Kwa nini? Kwa sababu wale wanaopewa mikopo, yale makundi ya vijana na wanawake hayajaandaliwa kitaaluma katika uendeshaji wa biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hata kwenye hotuba ukurasa wa 142, utaona wameweka lengo la Wizara ambalo wamesema kwamba ni kuhamasisha na kuelimisha wajasiriamali namna ya kuanzisha na kuendeleza biashara. Kwa hiyo, hili ni lengo mojawapo la Wizara katika sekta ya viwanda vidogo na biashara ndogo ndogo. Kwa hiyo, kuna uhitaji wa kuweza kuwapatia mafunzo ya kuanzisha biashara (to start up their own enterprises) kama ni vijana ama ni wanawake au wajasiriamali wowote waanzishe lakini waweze kuendeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mafunzo haya yanaweza yakapatikana kwa kutumia ile machinery tuliyokuwa nayo. Hata katika Serikali za Mitaa kuna Maafisa Biashara wa Mikoa, lakini kwenye Halmashauri pia kuna Maafisa Biashara. Wao wanaweza wakatumika, kwa sababu hii sera ni ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji. Japokuwa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ndiyo inafanya utekelezaji, lakini jukumu kubwa ni la Wizara hii kusimamia utekelezaji wa ile sera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, waangalie ni namna gani watatumia ile mifumo ili hata hivi vikundi, kwa sababu tunategemea vipate faida na ile mifuko ya kuwasaidia vijana na wanawake iwe ina manufaa, kwa hiyo, wapatiwe haya mafunzo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, twende mbele, hii Serikali iwasiliane, kwa sababu katika Wizara ya Elimu, Serikali ione namna ya kuweka katika mitaala ya elimu mafunzo (Basic Entrepreneur Skills) kuanzia ngazi ya chini ya elimu, kuanzia primary mpaka secondary. Kwa sababu tusiwaandae vijana wetu for white collar jobs, tuwaandae pia waweze kujiajiri. Kwa hiyo, tuwape mafunzo yale basic ya kuanzisha enterprises zao wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Serikali iweze kuchukua maoni hayo na kuyafanyia kazi. Vilevile tusisahau kwamba katika uchumi wa viwanda tunahitaji sana ku-invest katika kilimo. Kwa hiyo, Serikali ione ni kwa namna gani inawekeza katika kilimo, kwa sababu hiki kilimo ndiyo kitakuja kulisha viwanda vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kule kwetu Kigoma, sisi kumekuwa kuna jitihada za kuanzisha hata viwanda vya mafuta ya mawese ili kusikosekane mafuta. Yaani hatuwezi Tanzania tukasema hatuna mafuta ya kutosha wakati kuna nchi kama Malaysia ambayo ilikuja kuchukua mbegu ya mchikichi Kigoma na leo hii ina-produce mafuta ya mchikichi (palm oil) kwa wingi sana halafu sisi kama Tanzania tukashindwa kuwekeza katika mbegu bora itakayozalisha kwa kiwango kikubwa na ikaweza kulisha viwanda vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Wizara hizi ziweze kufanya kazi kwa pamoja kama Wizara ya Kilimo, Wizara ya Viwanda na Biashara kwa sababu mwisho wa siku tunahitaji kilimo ili kije kinufaishe viwanda vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kupongeza jitihada za Serikali katika viwanda, kwa mfano, mradi huu wa Stiegler’s Gorge ambao utazalisha zaidi ya megawati 2100 za umeme ambazo ni jitihada zinazoonekana za kuelekea katika uchumi wa viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.