Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Nuru Awadh Bafadhili

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu muumba mbingu na ardhi kwa kuniwezesha kuchangia machache. Ni kweli awamu hii ni ya uchumi wa viwanda lakini tujiulize viwanda hivyo vinavyoongelewa vitajengwa na kumalizika kwa wakati?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inayo nia thabiti ya ujenzi wa viwanda lakini tatizo lipo kwa watendaji. Wapo baadhi ya watendaji ambao hawana nia nzuri na Taifa hili, wanadumaza maendeleo ya Taifa. Hawa watendaji wanakuwa wepesi wa kuomba rushwa kiasi kwamba hata wawekezaji wanahofia kuwekeza nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanga kulikuwa na Kiwanda cha Mbolea ambacho kimeng’olewa mitambo na habari nilizonazo eti kimehamishiwa Minjingu. Namuomba Waziri aeleze ni sababu zipi zilizosababisha kuhamisha kiwanda hicho ukizingatia kilikuwa karibu na bahari, jambo lililosababisha kupata unafuu wa upokeaji wa malighafi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Kiwanda cha Chuma, kiwanda hiki kimekuwa ni chaka la uhalifu. Kuna watu wanaishi humo kama vivuli vyao vya kujificha. Hata mashine zake zilianza kung’olewa. Mheshimiwa Waziri anatuambia nini kuhusu utendaji kazi wa hiki Kiwanda cha Chuma cha Tanga?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanga kuna viwanda vya wamiliki wa sekta binafsi, viwanda ambavyo vinatoa ajira kwa wananchi wa Tanga hususani vijana. Tunalalamika kuwa vijana wengi wamejiingiza katika dawa za kulevya hii huenda inasababishwa na ukosefu wa kazi za kufanya matokeo yake wanaamua kutumia dawa za kulevya. Serikali iangalie umuhimu wa kuanzisha viwanda ili viweze kutoa ajira hususani kwa vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inasema kuwa wanafunzi wanaomaliza masomo wanaweza wakajiajiri wao wenyewe, siyo kweli kwa vile mtu hawezi kumaliza masomo kisha akawa ana mtaji wa kufanya biashara yoyote, biashara ni mtaji. Je, anayetoka chuoni atapata wapi mtaji wa kumuwezesha kufanya biashara?