Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja timu yake kwa kazi kubwa wanayoifanya, kwa kuhakikisha tunafikia uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali iwekeze sana katika kilimo ili tuweze kupata malighafi kutoka kwenye mazao yetu ambayo tunayalima sisi wenyewe, kwani bila kuwekeza katika kilimo tutakuwa tunachelewa sana kuwa na viwanda. Niendelee kuishauri Serikali yangu tukufu ipeleke pembejeo za kutosha kwa wakulima na kujenga mabwawa ya kutosha ili wananchi waweze kulima kilimo cha umwagiliaji ili kuongeza tija katika kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia lazima tuhakikishe wananchi wanapata elimu ya ufundi hasa kwa vijana wetu wa Kitanzania ili wawe na uelewa wa kutosha katika suala zima la kusimamia viwanda vyetu tunavyo kusudia kuvijenga. Hivyo basi, Serikali ijenge Vyuo vya VETA kila Jimbo na sio kila Wilaya, kwa mfano Wilaya ya Lushoto tangu ianzishwe haina Chuo cha VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kupoteza rasilimali watu na sio hivyo tu pia tunakosa vijana wenye taaluma ambao hawataweza kusimamia viwanda vyetu. Lakini hatujachelewa tuanze sasa kujenga vyuo hivyo ili vijana wetu waende sawa na ajira ya ushindani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali kuanzisha Viwanda Vidogo Vidogo yaani SIDO kwani viwanda hivi kwanza vitainua kipato cha mtu mmoja mmoja, pili, uchumi katika sehemu husika kilipowekwa utakuwa na tatu, vijana wengi watapata ajira pamoja na kupata ujuzi hapo hapo. Kwa hiyo, niendelee kuishauri Serikali kuanzisha viwanda vidogo vidogo hivi katika kila Kata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanga ulikuwa ni Mkoa wa viwanda lakini sasa viwanda vingi vimekufa. Hivyo basi, niiombe Serikali iweze kurudisha viwanda vile vyote vilivyo kufa hasa kiwanda cha sabuni, nondo na kiwanda cha mbolea. Ni imani yangu viwanda hivi vikifufuliwa Tanga tutakuwa tumepiga hatua kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuongelea uchumi wa viwanda kama barabara zetu ni mbovu, maji hakuna na umeme haupo. Kwa hiyo, hebu tupeleke miundombinu hii, kwani hii ndiyo itatufikisha katika uchumi wa viwanda bila hivyo tutachelewa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Lushoto ni Wilaya inayojulikana kwa kuzalisha matunda na mboga mboga lakini cha kushangaza Serikali haijawahi kufikiria kuweka viwanda Lushoto. Hivyo basi niiombe Serikali yangu iweke viwanda Lushoto hasa viwanda vya matunda na mboga mboga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu wawekezaji, wapo wawekezaji wazuri na wabaya kwa mfano Lushoto kuna Kiwanda cha Miwati. Lakini kiwanda kile hakifanyi vizuri kwa sababu hakiwalipi mishahara wafanyakazi wake. Kwa hiyo, hili linasikitisha sana, kwani sera ya sasa hivi ni ya viwanda lakini kiwanda hiki kimekuwa hakina manufaa kwa wananchi wa Lushoto. Zaidi ya kuwanyanyasa wafanyakazi wake. Kwa hiyo, niiombe Serikali ifuatilie suala hili kwa haraka ili wafanyakazi hawa waweze kulipwa stahiki zao. Pamoja na kujua mwenendo mzima wa uendeshaji wa kiwanda hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali yangu tukufu kwa kuwa tunahitaji wawekezaji kwa wingi na tunawapenda wafanyabiashara wetu. Hivyo basi, ipunguze haya malalamiko yanayo lalamikiwa na wawekezaji pamoja na wafanyabiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.