Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri na kwa utekelezaji mzuri wa ilani. Nawapongeza pia Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji kwa utendaji mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Rais na Serikali ya Awamu ya Tano kwa utekelezaji wa mkakakti wa ujenzi wa viwanda ili Tanzania ifikie hadhi ya nchi ya uchumi wa kati mwaka 2025. Huu ni ukombozi kwa vijana na wananchi kwa ujumla, vijana shida yao kubwa ni ajira na viwanda ni ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Bagamoyo Serikali imetenga eneo la viwanda kwa awamu mbili; EPZ I hekta 5,722 (= eka 14,355) na EPZ II hekta 4,338; jumla hekta 9,080.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya EPZ I, yamethaminiwa mwaka 2008 na hekta 2,399 zimeshalipwa fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lililopo ni kuwa wananchi 1,025 kati ya 2,180 hawajalipwa fidia zao hadi leo miaka kumi sasa. Namuomba Mheshimiwa Waziri awajulishe wananchi wa Kata za Zinga na Kiromo wanaopisha EPZ ni lini watalipwa fidia zao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la EPZ II - hekta 4,338 linajumuisha maeneo yenye makazi ya wananchi katika vijiji vya Zinga, Kondo, Mlingotini na Kiromo. Vijiji hivi vina jumla ya kaya 3,381 (sensa ya zoezi) zenye watu 12,797. Maeneo haya hayajathaminiwa wala watu hawajalipwa fidia. Suala kuu ni kwamba, wananchi hawaridhii kuhamishwa maeneo yao ya makazi hasa kwa kuzingatia kuwa tayari wameshatoa hekta 5,742 kwa ajili ya EPZ.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali yangu tukufu kuwaachia wananchi maeneo yao ya makazi, wananchi hawa hawana hamu wala hawana nguvu ya kuhama na hawana mahali pa kwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Kijiji cha Pande wanaopisha bandari mpaka sasa hawana eneo la makazi mbadala. Ni utaratibu wa kawaida duniani kwa wananchi wanaopisha miradi mikubwa ya kitaifa kupatiwa makazi mbadala. Wananchi wa Vijiji vya Pande na Mlingotini waliahidiwa na Serikali makazi mbadala. Naiomba Serikali tukufu iruhusu wananchi hao kupatiwa eneo la makazi mbadala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.