Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili nami niweze kuchangia hoja iliyoko mezani na nianze kwa kuunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijachangia, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anazozifanya. Mheshimiwa Dkt. Hussein amekuwa mfano bora sana katika kazi anazozifanya na atakumbuka nilipoteuliwa kwenye nafasi ya Wizara ya Mambo ya Ndani nilimfuata kumwomba ushauri kwamba ni namna gani anaongoza Wizara hizi za vyombo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na ushauri wake alionipa ndiyo maana nami leo nimeweza kuonekaonekana kufuata hekima anazotumia kuongoza Wizara hizi za vyombo ambazo kimsingi kwa kweli majukumu yao ni tofauti sana na Wizara za kiraia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianzia hapo hapo kwenye pongezi nilizozitoa, naomba niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Wizara hizi za vyombo zikiongozwa na Wizara anayoiongoza Mheshimiwa Dkt. Hussein Mwinyi zina itifaki zake na majukumu yake yanafuata itifaki zao. Pamoja na kufanya kazi kwa kushirikiana lakini kila chombo kina kazi zake za kufanya. Ukihusisha Wizara kama ya Ulinzi na majukumu mengine ambayo yako kwenye idara zingine za vyombo utakuwa umekosea na utakuwa unakiuka itifaki hizo ambazo ziko katika vyombo vyetu vilivyoko katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kwa kuwa vyombo hivi vinafanya kazi kwa kushirikiana yanapokuja masuala ya majukumu ya ulinzi wa nchi yetu, ni makosa makubwa kwa Mbunge kudhania kwamba kuna majukumu ambayo yanahusu masuala ya kiulinzi, kuna vyombo vya dola vinaweza vikaona uhalifu na vikavumilia. Vyombo vya dola viko kazini na hakuna siku utasema vyombo vya dola viko likizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, majukumu haya ambayo Mheshimiwa Mbunge alikuwa anayataja yakihusisha masuala ya intelijensia ya Jeshi la Polisi, niwahakikishie kwamba Jeshi la Polisi pamoja na idara zake halijashindwa kazi, zinafanya kazi nzuri, vinachapa kazi nzuri na hata kazi hizo zinazofanyika zinaonekana. Ndiyo maana Mbunge akisimama akisema intelijensia ya Jeshi la Polisi imeshindwa kazi yake na hata akataja uhalifu, huwa nataka kujua kama anajua idadi ya wahalifu na kama anawajua wale wahalifu na kama huwa wana vikao akutane nao awaulize wamebaki wangapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme Jeshi la Polisi pamoja na vyombo vingine vya ulinzi na usalama havijashindwa kufanya kazi ya kukabiliana na uhalifu na wala hatuwaombi wahalifu kuacha kufanya uhalifu, tutakabiliana nao na tutashughulika na mmoja mmoja na tutahakikisha kwamba uhalifu hauwezi ukatawala hata kwenye mtaa mmoja katika nchi yetu. Sisi tuko kazini na kazi hiyo itafanyika kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ambako uhalifu ulikuwa unajitokeza wanaweza wakasema mazingira ya kazi yakoje na sisi tuko kazini kuhakikisha kwamba tunashughulika na uhalifu na kuhakikisha kwamba hakuna eneo wahalifu watajitamba ama kujigamba kwamba wao wanaweza wakawa washindi. Hatuwezi tukaupa fursa uhalifu katika nchi yetu ukatamalaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo sisi kama Wizara ambazo zinahusu vyombo, tunaendelea kufanya kazi kwa kushirikiana. Hata kwa upande wa mafunzo, tumeendelea kupokea vijana wanaotoka Wizara ya Jeshi la Ulinzi na Kujenga Taifa ambao wametokea JKT. Vijana wale ambao wametokea JKT wanakuwa wameshapata mafunzo makubwa ya awali hivyo wanapochukuliwa kwenye vyombo vingine ambavyo viko Wizara ya Mambo ya Ndani inakuwa ni sehemu ama mwendelezo wa kuweza kupata tu specifications za mafunzo ya kikazi ambayo yana uhitaji mahsusi katika Wizara ama idara zilizoko ndani ya Mambo ya Ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine lilijitokeza ambalo lilikuwa linaongelea vijana ambao wamehitimu JKT pamoja na wale ambao walijenga ukuta. Pamoja na kwamba hatuwezi tukaweka kauli ya kwamba vijana wote waliohitimu Jeshi la Kujenga Taifa watachukuliwa na vyombo ama idara hizi kwa sababu mafunzo wanayopewa yapo na mengine ambayo yanawaruhusu wao kujiajiri, lakini niseme hivi ambavyo tuko kwenye mchakato wa kupata vijana katika idara zetu, tunatarajia kwenda kuchukua vijana wengine ambao wamejenga ukuta na tunatarajia wengine tuwapate ambao wametoka kuhitimu katika kambi mbalimbali za Jeshi la Kujenga Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa column tulizopewa, tutapata zaidi ya vijana kama 1,500 kwa upande wa Jeshi la Polisi, tuna vijana karibu 1,500 kwa upande wa Jeshi la Uhamiaji, hivyo hivyo na kwa Idara ya Magereza pamoja na upande wa Zimamoto. Hao wote kama ambavyo Mheshimiwa Rais alishaelekeza tunategemea kuwapata kutoka Jeshi la Kujenga Taifa. Vijana wote ambao watakuja kwenye idara zetu tunatarajia kuwapata kutoka Jeshi la Kujenga Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile taasisi zetu hizi zinahitaji sana hawa vijana, tutaendelea kupokea hata wengine ambao watakuwa hawajaitwa kwenye awamu ya kwanza wajue tu ni suala la kimafunzo wataitwa tu kadri tutakavyoendelea kuita kwa ajili ya mafunzo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge kwa sababu najua na wao wana vijana wao ambao wanatoka Majimboni mwao wawaelekeze tu watume maombi kupitia kambi walizokuwa, kwa hivi tunavyoongea utaratibu wa awali unaendelea ili kuwapeleka kwenye upande wa Jeshi la Polisi na kidogo Uhamiaji na Zimamoto pamoja na Magereza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo lilisemewa na Mheshimiwa Waziri atalisema ni kuhusu watu wanaova sare za kijeshi na kufanya uhalifu. Wahalifu wana mbinu tofauti tofauti za kufanya uhalifu, lakini kama tulivyosema, sisi tunachofanya ni kukabiliana na watu wanaofanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila leo umekuwa ukisikia watu ambao walikuwa wakijifanya maafisa wakikamatwa na siyo tu waliovaa nguo za Jeshi la Wananchi, kuna wengine wanajifanya Maafisa wa TAKUKURU, TRA na Ardhi, wote wanaofanya uhalifu wa aina hiyo tumeendelea kushughulika nao na tutaendelea kushughulika nao. Kuhusu upande wa mavazi nitamwachia kaka yangu atalisemea zaidi kwa upande wake na jinsi ambavyo sheria zinasema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge na niwaombe tu waendelee kuvipa heshima vyombo hivi. Vyombo vya ulinzi na usalama vinafanya kazi kubwa sana. Ndiyo maana leo hii ukienda duniani kote utaona Jeshi la Wananchi wa Tanzania linatambulika na linaheshimika na sisi tuwe wa kwanza kuenzi heshima hiyo ya jeshi letu na kazi kubwa ambazo zinafanywa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine kama mimi ambao nimeenda kuomba ushauri kwa Mheshimiwa Dkt. Hussein, hata wao kwenye vyombo wanasaidiana na wanapeana ushauri na ndiyo mnaona kazi zikiendelea. Mimi nimtakie tu kazi nzuri Mheshimiwa Dkt. Hussein na kwa kweli tunamtakia kila la kheri ili kazi nzuri hii iendelee kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, nikupe pole, asubuhi niliona ulipata sekeseke, walistahili na kwa kweli nitumie fursa hii kuwapongeza Simba kwa kupata ubingwa. Mimi nilikuwa nawaombea tu wapate kwa sababu ilishaanza kuleta picha mbaya kwenye nchi jirani kwa timu kubwa kama hiyo kukaa zaidi ya misimu mitano hawajashiriki mpaka nchi jirani walishaanza kudhani labda wameshuka daraja, hii ilianza kuharibu utani wa jadi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachowaambia, wanapojisifia sana watambue kwamba wakati Yanga wanapata ubingwa mara tatu mfululizo na wao walikuwepo kwenye ligi hiyo hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mwanangu ana miaka 13, tangu azaliwe hajawahi kuona Simba imepata ubingwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante sana.