Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami pia niweze kuchangia hoja hii ya Mheshimiwa Waziri iliyo mbele yetu. Nianze kwa kusema kwamba siungi mkono hoja ikiwa suala la bei ya pamba halitakaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unafahamu vizuri kazi ya kulima inakuwaje. Kama kazi ya kulima zawadi yake ndiyo hii tunayoipata kutoka Serikalini basi nadhani tuhamasishe watu wetu waache kulima. Mwaka jana bei ya pamba ilikuwa Sh.1,200, mwaka huu kama alivyosema ndugu yangu ni Sh.1,100 sababu hazieleweki, haijajulikana kwa nini bei imeshuka? Kuna mambo mengi hapa ambayo yanasikika, moja ni kwamba Sh.33 zinabaki sijui ushirika, Sh.12 zinaenda kuimarisha sijui Chama Kikuu cha Ushirika, Sh.55 zinaenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapofika kwenye masuala yanayogusa watu wengi ni muhimu sana Serikali iwe sikivu sana. Ni vuzuri tuelewane hapa, bei ya pamba kama ilivyotajwa na ndugu yangu Mheshimiwa Ndassa ndivyo ilivyo kwa nini kuondoa Sh.100 kwa wakulima? Si ingebaki angalau Sh.1,200 kama ilivyokuwa mwaka jana, kwa nini tumeiondoa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutataka majibu yaliyo sahihi, lakini jibu lililo sahihi ni kurudisha Sh.100 kwa wakulima wa pamba. Majibu mengine mbali na hayo hayataeleweka na hayaeleweki. Ndugu yangu Mheshimiwa Ndassa amesema vizuri, mazao haya makuu ya pamba, korosho na mazao mengine ni siasa kwenye nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, amesema juu ya ununuzi wa pamba mwaka huu. Msimu wa pamba umekwisha kuanza tarehe 1 Mei, 2018 lakini hakuna tone la pamba iliyonunuliwa mpaka sasa. Kwenye Jimbo na Wilaya yangu hakuna pamba iliyonunuliwa na sababu ni kwamba, umekuja utaratibu mpya wa kununua kupitia ushirika. Ushirika ni mzuri, lakini ulifanya vibaya siku za nyuma na watu hawauamini tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa badala ya Serikali kuhangaika na mafunzo na kuwajengea uwezo watu wetu na ushirika wenyewe ili waelewe dhana mpya ya ushirika kwamba itawasaidiaje wananchi wetu, wamekuja moja kwa moja na kuiweka kwenye utekelezaji. Nadhani ni kosa kwa sababu kama watu walishauona ushirika ni mbaya unapotaka kuanzishwa upya ni muhimu sana kuwaelimisha wananchi waweze kuelewa. Kwa hali ilivyo mimi sijui tutaishia wapi msimu huu wa pamba kwa sababu kama pamba haijanunuliwa, haijaenda kwenye ghala la ushirika, sasa sijui itaenda lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo hayo utaratibu uko hivi, pamba ikusanywe kwenye ghala la ushirika, ghala lenyewe la ushirika kwenye kijiji liko moja na kijiji kina vitongoji zaidi ya kimoja, vitatu, vinne hadi vitano na vingine viko mbali, lakini wakati wa ununuzi wa watu binafsi pamba ilikuwa inanunuliwa mahali karibu na mwenye pamba, maghala yalikuwa mengi. Sasa safari hii ghala liko moja na mahali pengine maghala hayo ya ushirika yaliyopo yamechakaa hayana hadhi ya kuhifadhi pamba, sijui tutafanyaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tatizo lingine kuna utaratibu wa wakulima kulipwa pesa yao kupitia benki. Kwa nini iwe ni lazima? Nafikiri suala la kulipwa kupitia benki ni zuri kama ni kwa hiyari, kwa sababu hii pesa ni ya mkulima. Mimi nauza pamba yangu leo, nina mgonjwa, nina matatizo mtoto wangu hajaenda shule sijanunua uniform za shule, halafu nipeleke pamba yangu nisubiri siku mbili, tatu, nne bado sijalipwa. Halafu ikilipwa niende benki iliyo Makao Makuu ya Wilaya kilometa mia moja na kitu, saa ngapi nakamilisha mahitaji yangu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili linapaswa kuangaliwa vizuri. Halafu ushirika unafanyika kama wakala, wao wanakusanya pamba ya mkulima halafu mnunuzi anakuja pale na pesa yake au pesa yake anawapa watu wa ushirika. Hivi kuna mnunuzi gani binafsi atapeleka pamba yake kwa mshirika ambaye anajulikana alikuwa …

TAARIFA . . .

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naikubali kabisa taarifa yake. Kwa sababu hao viongozi waliochaguliwa nina habari wengine wametoa rushwa sijui kwa kutarajia kupata kitu gani. Kwa hiyo, ni walewale waliokuwa wameharibu ushirika kule nyuma ndiyo wamerudi.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini pamba haijapelekwa sokoni mpaka leo ni kwa sababu wanunuzi na wenyewe wamerudisha mikono nyuma kwa sababu hawana imani na watu wa ushirika waliopewa dhamana ya kuchukua pamba na pesa kwa wanunuzi. Mnunuzi huyu atamwaminije mtu ambaye hajamchagua? Atamwaminije ampe bulungutu la mamilioni ya pesa eti amnunulie pamba wakati hamjui? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama utaratibu wa kununua uko hivyo basi wanunuzi binafsi wapeleke watu wao kwenye gulio pamba ilipo, muuzaji aje pale auze pamba yake alipwe hela yake aondoke lakini mtu atakayekuwepo pale ni yule aliyeaminiwa na mnunuzi wa pamba. Vinginevyo ushirika tuendelee kuujenga upya bado haujapokelewa vizuri kwa sababu ya historia yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bei ya pamba kuwa chini inasababishwa na vitu vingi mojawapo ni soko la hapa ndani ni dogo sana. Takwimu zinaonesha asilimia 20 mpaka asilimia 30 ndiyo tunaweza kutumia hapa ndani. Viwanda vyetu vya pamba vinashindwa kushindana kwa sababu ya ushindani usio haki wa nguo nyingi kutoka Uchina, Malaysia, Uturuki na mahali pengine. Sasa tutapandishaje mazao ya wakulima wetu nchi hii kama hatulindi viwanda vilivyoko kwenye nchi hii? Viwanda vya nchi hii havilindwi vinaachwa tu na wakati mwingine vinashindanishwa na mtu ambaye ana nguvu kuliko yeye, lazima vitakufa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu zao la pamba limelimwa kwa wingi sana. Tunamshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu hata Mheshimiwa Waziri wa Kilimo mweyewe kwa kuhamasisha hivyo, lakini wakulima wetu wamelima pamba hii kwa taabu sana na ndiyo maana nasema kama bei ya pamba hairudi Sh.1,200 siwezi kuunga mkono hoja hii.