Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo

MHE. ZUBER M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nichangie na mimi mada iliyopo mbele yetu jioni hii ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka niende moja kwa moja kwenye uchangiaji na mchango wangu niuelekeze kwenye vyama vya ushirika. Ushauri wangu kwenye vyama vya ushirika kuna mambo ya kufanya, aidha, turekebishe Sheria ya Vyama vya Ushirika kwa sababu sheria hii bado ina mgongano mkubwa sana. Mimi mwenyewe nimeshuhudia mwaka huu, kwanza nilikwenda na Mkuu wangu wa Wilaya kukagua ghala tukafungiwa mlangoni tukaambiwa hakuna ruksa, sheria hairuhusu hata kuukaribia mlango wa ghala pale ambapo vyama vya ushirika vinafanya biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, si hivyo tu, kuna mgogoro mkubwa sana kwenye vyama vya ushirika kwa sababu mpaka sasa hivi vyama vya ushirika vimepoteza fedha za wakulima wa korosho takribani zaidi ya shilingi milioni 150. Nilipokwenda kumfuata Afisa Ushirika wa Wilaya majibu anayoniambia anasema yeye hana mamlaka kwa mujibu wa sheria ya kukagua vyama vya msingi, wenye mamlaka hayo ni Tume ya Ushirika. Tume ya Ushirika wako mbali sana na hivi vyama vya msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba Mheshimiwa Waziri ajaribu kauangalia Sheria hizi za Vyama vya Ushirika. Haiwezekani Mkuu wa Wilaya, Mbunge, Mkuu wa Mkoa hawaruhusiwi kukagua ama hata kuingia tu kwenye ghala eti Sheria ya Vyama vya Ushirika inakataza na hili ndilo linalotuletea matatizo makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mwingine, mwaka huu kwenye Vyama vya RUNALI na Lindi Mwambao mpaka leo hii hatujui hatma ya sulphur iko wapi. Ukijaribu kuuliza unaambiwa kuna mgongano kati ya Bodi ya Korosho pamoja na vyama vya ushirika. Vyama vikuu vya ushirika bado wanavutana ni nani mwenye haki ya kuagiza sulphur, jambo hili limetuletea matatizo makubwa sana. Wenzetu Mtwara chama chao cha ushirika walishaagiza sulphur na sasa hivi inafanya kazi lakini sisi bado tunababaishwa tu kwamba kulikuwa na mvutano kati ya Bodi ya Korosho pamoja na Vyama Vikuu vya Ushirika kati ya Lindi Mwambao na RUNALI, nani aagize sulphur. Jambo hili Mheshimiwa Waziri naomba mlifanyie kazi ili sheria hii iletwe kama ni kufanyiwa amendment basi ifanyiwe amendment, ionekane mipaka kwamba Mkuu wa Wilaya mpaka wake ni wapi, Mbunge mpaka wake ni wapi na hiki chama cha ushirika kina kazi gani na Bodi ya Mazao mipaka yake iko namna gani, jambo hili limetuletea shida sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niongelee Maafisa Ugani. Kwa kweli ndani ya Wizara hii Maafisa Ugani wanaonekana kama vile hawana kazi za msingi, wakati huo sisi tunasema kwamba asilimia 80 au 70 ya wananchi wa nchi hii ni wakulima lakini Maafisa Ugani wameonekana kama hawana kazi wamepelekwa tu kule. Kwa mfano, kunapotokea shida ya Maafisa Watendaji wa Vijiji au Kata watu wa kwanza wanaoangaliwa ni Maafisa Ugani. Zamani tulikuwa tunachukua hata Walimu Wakuu lakini sasa hivi kwa sababu imeonekana walimu wakuu ni muhimu sana tukaamua kuwaaacha sasa tumechukua Maafisa Ugani ndiyo tumewafanya Watendaji wa Kata na Vijiji. Tena basi wanafanya kazi ambazo si zao na kwa hiyo ufanisi kwenye utendaji wa vijiji haupo kwa sababu hawajasomea na huku kazi ambayo wamesomea wameiacha haina ufanisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye halmashauri zetu huyakuti mashamba ya mfano kwa sababu Maafisa Ugani wana kazi nyingi, wanakuambia ni muda gani niandae shamba wakati huo huo natakiwa nifanye kazi za utendaji? Kwa nini tumewapeleka huko? Tumewapeleka huko kwa sababu tunawaona hawana kazi, jambo hili linatuharibia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile hata wale wachache waliopo hawana vitendea kazi. Namwomba Mheshimiwa Waziri kama kweli tunataka kusimamia kilimo kitupatie tija basi jambo hili la Maafisa Ugani ni muhimu sana, watengenezewe mazingira na wakafanye kazi ambazo wamesomea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine mimi naona sasa hivi Serikali imeamua kuvuruga kilimo. Zamani mimi wakati nasoma kuna swali unaulizwa pale la jiografia, unatajiwa zao unaambiwa taja mkoa unaolima. Zao la pareto, unataja mkoa unaolima, ukiulizwa chai unaambiwa Rungwe, ukitaja mahindi unaambiwa Iringa lakini leo tumeanza sasa vurugu. Mnataka korosho, pamba na pareto zilimwe nchi nzima, yaani hiyo mnayoanzisha ni vurugu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, navyofahamu Maafisa Ugani wanagawiwa kulingana na taaluma zao. Kuna mtu aliyesomea mambo ya pamba atapelekwa Mwanza na Shinyanga, watu wengine wamesomea alizeti watapelekwa Singida lakini leo hii mnaanza vurugu mnasema korosho na pamba italimwa nchi nzima hii tunaenda kuvuruga, haiwezekani lazima tuwe na mgawanyo wa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana siku zote tunasema hii Serikali muwe na vipaumbele. Maana ya vipaumbele ndiyo hiyo. Sasa haijulikani ninyi korosho, pareto au chai mnalima wapi ni vurugu tu, haiwezekani. Pamoja na kwamba korosho ni fursa lakini alizeti, pamba na kahawa nazo ni fursa lazima mjipange tugawanye tujue. Mimi wakati nasoma jiografia ilikuwa inanieleza hivyo, nikiulizwa tu chai najua Rungwe, mahindi najua Iringa lakini hii vuruga mnayotuletea mimi sikubaliani nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba nijielekeze kwenye upatikanaji wa mbegu. Upatikanaji wa mbegu hasa za mahindi, maana kule kwetu kijijini kwetu kwenye Kata ya Mpigamiti kule sisi ndiyo tunaolisha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)