Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

Hon. Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwakawa Fedha 2018/2018 – Wizara ya Kilimo

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi. Mimi naamini kuwa kila mtu anapofanya kazi anatakiwa anapopata ujira wake autumie bila ya mtu yeyote kumuingilia katika kipato chake. Wafanyakazi wa nchi hii wanafanya kazi na wanalipwa mshahara hakuna Serikali yoyote ya nchi hii inayokwenda kumpangia matumizi mfanyakazi yule ya mshahara wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa nini wakulima wanalima kwa shida, kwa taabu wanapovuna mazao yao mnataka kuwapangia namna ya kuyatumia mazao yao? Nimwombe Mheshimiwa Waziri akija hapa, pamoja na kwamba zigo hili tunamtwisha lakini yeye ndiye mwenye dhamana na Wizara hii, aje atuambie hivi ni kwa nini wakulima hawa ambao hamuwapi mbegu, wananunua mbegu kwa shida ambazo bei zake ni aghali, pembejeo mnachelewesha na wengine kwa mfano huku Dodoma sisi pembejeo za Serikali hatuzijui kabisa, hamuwasaidii kitu
chochote kile lakini mnataka kuwapangia namna ya kutumia mazao yao pale wanapokuwa wamevuna? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala zima la mbegu za mahindi; kilo mbili ya mbegu ya mahindi inauzwa shilingi 14,000. Mwananchi huyu anapanda mbegu ile ya kilo mbili kwa shilingi 14,000, leo ndani ya Mkoa wa Dodoma, Wilayani kwangu Chemba wakulima wale wanauza debe la mahindi shilingi 2,500. Mbegu kanunua kilo mbili Sh.14,000 lakini debe la mahindi anauza shilingi 2,500. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wakulima tunachowataka ni nini? Yaani hii shilingi 2,500 anayouza hata nusu kilo ya dagaa hana uwezo wa kununua ili aweze kula. Mtu huyu anatakiwa kuuza madebe mawili apate shilingi 5,000 aende akanunue kilo moja ya sukari aweze kunywa chai ama uji na familia yake. Hiki kitu hakikubaliki na Mheshimiwa Waziri ukija mimi nitaomba unisaidie tu, umejipangaje na Wizara yako kuhusiana na upatikanaji wa mbegu ambazo zitapatikana kwa urahisi na kwa gharama ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la pili kuhusiana na migogoro ya ardhi. Tumeona migogoro mingi ya ardhi inayotatuliwa leo ni upande wa maliasili tu. Wakulima hawa pamoja na shida kubwa wanayoipata ya kulima chakula na sisi Wabunge tunakula chakula cha wakulima hao lakini mahali pa kulima nako pia imekuwa ni changamoto. Migogoro ya wakulima watu hao wanakufa kifo huku wakiwa wanajiona wao wenyewe wanakufa na kitanzi chao. Hawana watu wa kuwapigia kelele kwenye migogoro na wakisema wanaonekana ni wakorofi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka Mheshimiwa Waziri akija aniambie suala la migogoro ya ardhi ya wakulima nini mkakati wake kwenye bajeti hii ya fedha ya 2018/2019 ili wananchi wetu wakulima hawa ambao wanafanya kazi kubwa ya kutafuta chakula kwa ajili ya Taifa letu tuweze kuona namna gani migogoro hiyo inakwenda kutatulika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri akija naomba wakulima wangu wa Wilaya ya Chemba, eneo la Sekii pamoja na Champanda nataka aje aniambie mgogoro huu baina ya WMA ya Makame (Kiteto) na wananchi hawa kwenye vijiji hivi hatma yao ni nini? Wananchi hawa wameendelea kunyanyasika, mashamba yale ni ya kwao, Makame WMA wameenda kurudisha mpaka nyuma, matokeo yake watu wetu wanaenda kufyekewa mazao, si sawa sana. Mheshimiwa Waziri akija naomba anisaidie huu mgogoro unakwenda kuishaje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala zima la madeni ya mbolea, wameongea Wabunge wengi. Siku za nyuma huko mwaka 2014 na kurudi nyuma, watu hawa pamoja na kuwa walikuwa wanafuja hizo nyaraka na kadhalika lakini walikuwa wanalipwa. Leo ni mwaka wa nne watu hawa hawajalipwa mnadai kwamba mnafanya uhakiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 mlituambia mnahakiki, mwaka 2017 mnahakiki, leo mnafanya nini? Mtaendelea kuhakiki mpaka lini? Hivi kwa Serikali na vyombo vyake vyote mlivyonavyo mmeshindwa kubaini nani anastahili kulipwa na nani hastahili kulipwa? Mheshimiwa Waziri akija tunaomba... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)